7  WAISLAMU WA KWANZA

 213
Bwana Mungu alifunza
Watu gani wa kuanza
Isije kuwa ni chonza
Wengine kuwaanziya

214
Aanzie ikhwani
Na wapenzi na wendani
Wa rikale na wa chini
Si watu ajinabiya

215
Kaambiwa Bi Khadija
Hakusita mara moja
K awashinda wote waja
Kums'adiqi Nabiya

216
Bibi huyu mtukufu
Kaongoza uwongofu
Tukafuata uluufu
Na sote twamwandamiya

217
Ameanza kwa baraka
Baraka isiyo shaka
Dini hii kutukuka
Bi Khadija kaanziya

218
Tumeona Isilamu
Wametushinda h'uramu
Kumwitika Mua'dhamu
Ni wao watanguliya

219
Ndio hivyo hii Dini
Hutukuza niswani
Tangu hapa duniani
Na Akhera kuingiya 

220
Ndio wao wa kulindwa
Ndio wao wa kupendwa
Ndio wao wa kutendwa
Kwa huruma na muruwa

221
Siku ile wakis'ali
Bi Khadija na Rasuli
Kawaona Bwana A'li
Akabaki ashangaa

222
Kanena: Mwafanya nini?
I'bada hii ni gani?
Sijaonapo zamani
Nijuvye nipate juwa

223
Na huyo Sidi A'lii
Bado mtoto s'abii
Myaka kumi hapitii
Bin A'mi wa Nabiya

224
Mtume akabaini:
Ni i'bada ya Manani
Katufunza hii Dini
Tufwate nakuus'iya

225
Kijana akadhukuri
Nenda baba kushauri
Na yeye atapo kiri
Nitakuja kufwatiya

226
Mtume hakuyapenda
Hayo mtoto kutenda
Haneni mwenye kuunda
H'adi mambo kutimiya

227
Akamwambia: Fikiri
Kata mwenyewe shauri
Ukiona ndiyo kheri
Ni mwenyewe a'zimiya

228
Usiku katika kiza
Mtoto alikiwaza
Akaona muangaza
Wamuonyesha ya Njiya

229
Akaona kwa yaqini
Kuwa hii ndiyo Dini
Kakaye kamuamini
Kuwa kweli ni Nabiya

230
Qiasi kupambazuka
Mbee za Tumwa kafika
Uso wake unawaka
Kwa nuru ilo mwingiya

231
Akamwambia Amini:
Nashuhudia Manani
Na wewe nakuamini
Wewe kweli ni Rasuwa

232
Basi huyu Bwana A'li
Ni Isilamu wa pili
Kwa vijana ni awali
Ni yeye katanguliya

233
Mngu kampa wajihi
Uso kuwa mshabahi
Kumwelekea Ilahi
Tangu utoto s'abiya

234
Uso wake hapo tangu
Umetukuzwa na Mngu
Hakuijua miungu
Ya watu wa jahiliya

235
Ndugu huyu etwa Simba
Asiye jua ruu'ba
Ndiye mwingi wa mah'aba
Kwa Isilamu jamiya

236
Ndiye huyu ni Imamu
Na Mlango wa I'limu
Ni ndugu wa Mua'dhamu
Mkonowe wa kuliya

237
Siku alio kubali
Kusilimu Bwana A'li
Alisilimu wa pili
Mtume alo mleya

238
Wa kulelewa waladi
Nyumbani kwa Muh'amadi
Jinale etwa Zaidi
Na mkewe kafwatiya

239
Mkewe etwa Baraka
Mlezi wa Rasulaka
Baraka Muafirika
Yuko mbele nakwambiya

240
Zingatia utukufu
Kuupata uwongofu
Siku hiyo ya sharafu
Ni siku ya kuanziya

241
Si ajabu hapo basi
Kuvikwa njema libasi
Wote walio weusi
Kutukuzwa na Nabiya

242
Baraka ndiye mamaye
Na Zaidi ni mwanaye
Akamwoza dadaye
Mwanamke Qureshiya

243
Mtume wetu kanena:
Qabila hapana tena
Kuja mtu kujivuna
Na watu kuwaoneya

244
Hapana aliye bora
Kwa ngozi yake kung'ara
Rangi zetu si ishara
Kutukuka kwa Jaliya

245
Mtu yake ni a'mali
Aipendayo Jalali
Kufaulu na kufeli
Mwenyewe kujitendeya

246
Na mambo hayo kujiri
Bwana wetu Bubakari
Alikuwa kasafiri
Yamani ndio kendeya

247
Siku tatu zilipita
Tangu Utume kupata
Hakusita kuja fwata
Mara akiwas'iliya

248
Alipo pata khabari
Kwa mwenyewe Mukhtari
Hapo hapo alikiri
Na hapo kashuhudiya

249
Huyu ni wake rafiqi
Abubakari S'adiqi
Mtetea kila h'aqi
Mwenye s'afi yake niya

250
Tangu wao utotoni
Bubakari na Amini
Walikuwa ni wendani
Waso kuwa na mithaa

251
Hapana wa kuwashinda
Kwa mapenzi ya kupenda
Mfano pete na chanda
Daima wako pamoya

252
Walio silimu naye
Ni mtukufu mamaye
Na pamoja na mwenziye
Mkewe na wana piya

253
Wengine walo amini
A'thumani wa A'fani
Mzalendo Liwat'ani
Kati ya Bani Umeya

254
S'ifa zake ni tukufu
Mwendo wake ni mwongofu
Watu wote huzisifu
Rai zake na t'abiya

255
Alitoa yake mali
Ovyo bila ya kujali
Kwa ajili ya Rasuli
Na Mola wake Jaliya

256
Watumwa na waungwana
Walio mfuata Bwana
Sitoweza kuwanena
Kwa majina moya moya

257
Walikuwa si qalili
Wabora wenye a'qili
Lakini hao juhali
Ni wengi wa kupitiya

258
Kwa hivyo walo amini
Walifanya chini chini
Kutangaza yao Dini
Na huku wakikhofiya

259
Kila mtu Muumini
Hukhubiri kwa wendani
Au sema ikhiwani
Ambao wamsikiya

260
Na wakifanya i'bada
Hutoka nje bai'da
Walikitenda kwa shida
Hawakuwa na h'uriya

261
Walipo gundulikana
Kwamba huko wakutana
Wakaacha hapo tena
Majangwani kujendeya

262
Ikawa tena dharuri
Nyumbani kujisitiri
Ikawa kisirisiri
Wakutanika jamiya

263
Ndugu hao Isilamu
Walio shika khat'amu
Nyumbani kwa Arqamu
Ndiko wakikutaniya

264
Huingia mbali mbali
Kwa vikundi ni muh'ali
Wasiwaone juhali
Wakaja washambuliya

265
Muda wa myaka mitatu
Wakijificha kwa watu
Hapana alo thubutu
Nje kujitangaziya

266
Jambo kuu ukiwaza
Ifwate hii ruwaza
Usiwe kulieneza
Ila kwa mbinu na njiya
 

MAFUNZO:

Tunaona, basi, kuwa Dini hii ya Islamu tangu mwanzo ni Dini ya watu wote, wanaume na wanawake, watoto na watu wazima, matajiri na masikini, watu wa kabila zote. Tangu siku ya kwanza walikuwamo Waafrika. Kwa Muafrika hii ndiyo Dini yake ya jadi.