6.   UTUME

163
Mtume tangu udogo
Akichukia urongo
Mas'anamu ya udongo
Huwaje kusujudiya

164
Vitendo vy a kikafiri
Vikimuudhi
kathiri
Na kila akifikiri
Huzidi kuvichukiya

165
Akiona uqatili
Watendavyo majahili
Kuwazika
at'ifali
Watoto kuwafukiya

166
Akiona majeuri
Watenda watu
qahari
Hushindwa na kus'ubiri
Na kuweza vumiliya

167
Akiona na ulevi
Na unyang'anyi na wivi
Hunena huwaje hivi
Watu wakajitendeya

168
Akiona h'asharati
Wanaume na banati
Humkauka s'auti
Qauli humpoteya

169
Na u'mri ukizidi
Bwana wetu Muh'amadi
Chuki yake yashitadi
Kuchukia maa's'iya

170
Akionea huruma
Mpotofu wake umma
Akaungana na chama
Cha dhuluma kuzuiya

171
Chama hichi ni cha kheri
Kazua A'mi Zuberi
Akangia Mukhtari
Na mno kafurahiya

172
Lakini hakikut'osha
Watu wake kuamsha
Maovu kuyakomesha
Wanyonge kupiganiya

173
Na mambo yakimzidi
Hutoka nje H'amadi
Huacha mji
bai'di
Pekee hujitokeya

174
Hwenda huko majangwani
Kangia ndani pangoni
Kimwelekea Manani
Kuwaza na kus'aliya

175
Mambo
akiyadabiri
Hawezi
kuyas'awiri
Atendeje Mukhtari
Na mambo yamuemeya

176
Akiwa hivyo Amini
U'mri arubaini
Na mwezi wa Ramadhani
Vituko vyamtukiya

177
Kamuona hapo mbele
Kasimama mtu pale
Atamka kwa kelele:
Soma alivyo mwambiya

178
Sijui soma kajibu
Mtu akaja qaribu
Akambana H'abibu
Mayowe ampigiya  

179
Kawa hivyo mara tatu
Atendavyo huyo mtu
Amshika Bwana wetu
Ni kama amkemeya

180
Tena hapo katamka
Aya zisiyo na shaka
Iqra Bismi Rabbika
Mtume akafwatiya

181
Tas'awari haya basi
Tusiwe na wasiwasi
Tuyajue sote nasi
Yafaa kuzingatiya

182
Jambo lake la awali
Alilo tumwa Rasuli
Si S'aumu si Kus'ali
Si Zaka kujitoleya

183
Hakuambiwa Kuh'iji
Watumwa kuwafariji
Hakwambiwa kunywa maji
Na tembo kulisusiya

 184
Hakuus'iwa kwa mama
Na wana kuwatazama
Aliambiwa: Kusoma
Ndilo alilo anziya

185
Qauli yake awali
Alo itoa Jalali
Mja kwanza kuratili
Kusoma ni kuanziya

186
Mwenyezi Mungu Mwalimu
Kajipa bora isimu
Ni
Mfunzi kwa qalamu
Kupinga
ujahiliya

187
Muu'jiza wa kusoma
Ni a'jabu ya daima
Washinda ile ya zama
Zamani zilo pitiya

188
Fimbo kuja kuwa nyoka
Na moto ukazimika
Na watu wakafufuka
Ni h'adithi twasikiya

189
Lakini ya kuyaona
Si maneno ya kunena
Ni hayo ya wetu Bwana
Milele twayangaliya

190
Muu'jiza wa qalamu
Ndio huu wa kudumu
Qur'ani ilo timu
Daima itasaliya

191
Enzi mpya imefika
Ya i'limu kuinuka
Hii Ishara h'aqiqa
Tuone na kusikiya

192
Mtume kwisha kwitika
Mtu yule katoweka
Endako au kutoka
Mtume kwamuemeya

193
Akaondoka Sharifu
Na moyo wajaa khofu
Kizengea
takhafifu
Nyumbani akarejeya

194
Bi Khadija kutazama
Akadhani ana homa
Akamfunika vyema
Mumewe alo mjiya

195
Akawa awaweseka
Hajui ano tamka
Hata joto likishuka
Mtume kasimuliya

196
Bibi huyu
mbas'iri
Kupata yote khabari
Kamtuza Mukhtari
Akamwambia: Tuliya

197
Lolote lenye madhara
Sidhani
litakudara
Hujapata hata mara
Maovu kututendeya

198
Tangu wako utotoni
Wajulikana Amini
Wanyonge na masikini
Daima wahurumiya

199
Ni yaqini Maulaya
Hatokutenda vibaya
Tauliza yote haya
Kwa ndu yangu tamwendeya

200
Ndugu yangu Bunu A'mu
Waraqa mtaa'lamu
Anazo jua i'limu
Za vitabu samawiya

201
Waraqa ni Mnas'ara
Masih'i mwenye imara
Akasema: Aje mara
Nataka kumsikiya

202
Muh'amadi akafika
Kaeleza yalo zuka
Kaambiwa: Malaika
Ndiye aliye kujiya

203
Ni Roho Mtakatifu
Huwajia watukufu
Kawajia
wa salafu
Na wewe umefwatiya

204
Kamjia Nabii Musa
Na pia Nabii I'sa
Na wewe ni hivi sasa
Ndiwe alo kutokeya

205
Sasa wewe Mukhtari
Ni Mtume jibashiri
Mola wetu kakhiari
Uongoze watu Njiya

206
Natamani aniweke
Mola wangu nikwitike
Dini yako niishike
Kwa mkono wa kuliya

207
Mtume wetu wa shani
Kajaa hapo Imani
Akaa'zimu pangoni
Atakwenda kurejeya

208
Alitamani Rasuli
Tena Molawe Jalali
Amtume Jibrili
Apate kumsikiya

209
Apate pata maneno
Ya utamu mwingi mno
Yaso andikwa kwa wino
Ya Mola kumshukiya

210
Siku chache si kathiri
Ikashuka
Muddathiri
Kaambiwa as'ubiri
Kwa dhiqi zitomjiya

211
Kaambiwa abashiri
Kua'budiwa Qahari
Jinale alikabiri
Na watu kuwelezeya

212
Naye Mbashiri bora
Hakuruka kwa papara
Aliirai bus'ara
Na njia za kupitiya  

 MAFUNZO:

Mwenyezi Mungu humpa utukufu amtakaye, lakini utukufu ni jukumu vile vile. Na mtu hupewa huo utukufu akiwa ni mwenye kustahiki, naye akatambua jukumu lilio juu yake. Tunaona hapo vipi Bwana wetu Muhammad s.a.w. alivyo uchukua utukufu wa Unabii, na mzigo ulio ambatana nao. Na kadhaalika Makhalifa walio kuwa waongofu. Ama hao ambao walio pewa utukufu wakaona wastarehe nao utukufu, wakaghafilika na jukumu linalo ambatana na utukufu na uwongozi, wamefeli na wamefedheheka. Pia hapa tunajifunza vipi sisi Waislamu inatupasa kuwatukuza wake zetu. Mke mwema ni kama huyo Bi Khadija alivyo kuwa kwa mumewe, Mtume s.a.w. Na kama alivyo kuwa Mwana Fatma binti Rasuli Llahi kwa mumewe Sayyidna Ali, Mwenyezi Mungu, awape amani na radhi zake. Wazungu wana usemi: Nyuma ya kila mwanamume mkubwa yupo mwanamke mkubwa.