Utangulizi

wa Marehemu Sheikh Abdulla Saleh Farsy

Kwa kweli maisha ya Mtume Muhammad s.a.w. yameandikwa kwa mashairi ya Kiswahili na watu kadhaa  wa kadhaa, miongoni mwao ni Sayyid Abu Bakar bin Abdulrahman (Mwenye Mansabu) aliye kuwa mwanazuoni mkubwa, Kadhi na mshairi mkubwa wa Lamu, Sheikh Mzee bin Ali Comorian wa Dar es Salaam na Shekh Saidi Musa wa Dar es Salaam. Lakini hao wote wameifasiri ile ile Maulidi ya Barzanji.     Zipo na tenzi nyengine ambazo hazikutegemezwa juu ya Maulidi ya Barzanji lakini nazo ni fupi kabisa.

Utenzi huu wa Ruwaza Njema (Uswatun Hasana) ni wa kwanza katika tenzi juu ya maisha ya Mtume s.a.w. ulioandikwa kwa urefu na ukamilifu kama ilivyomkinika, na kwa mpango usiotegemezwa Maulidi ya Barzanji au mengineyo yoyote. Mwenyewe mtungaji amesema kuwa ametegemeza utenzi wake juu ya kitabu changu Maisha ya Nabii Muhammad.     Hayo ni kweli, na mengine aliyoyaongeza pia ameyapata kwenye vitabu vya kutegemewa.

Sifa kuu ya utenzi huu ni jitihada ya mtungaji kuandika ambalo ameyakinika nalo kuwa ni sahihi, la kweli tu, na halina khtilafu.     Hilo si jambo jepesi kwa watungaji tenzi, kwani wao mara nyingi huvutika kwa utamu wa ushairi wakapita mpaka katika kusifu au kushutumu.     Mwenye kusoma utenzi huu, kama mwenye kusoma kitabu changu Maisha ya Nabii Muhammad naayakinike kuwa anasoma mambo yaliyothibiti katka taarikh (historia), wala hapana uzushi.

Kitabu changu kimepigwa chapa mara nyingi, na kila mara nakla zote zilimalizika.     Nina tamaa kubwa kuwa utenzi huu utapendwa kama kilivyopendwa kitabu changu, au pengine na kuzidi, kwani nudhumu ya mashairi huvutia zaidi kuliko maandishi ya sesa (ya "nathari").

Katika sifa za utenzi huu ni kuwa umezidi kuweka wazi na kutiltia mkazo yale mambo katika maisha ya Mtume s.a.w. ambayo ni muhimu sana katika kutuongoza sawa sisi Waislamu katika maisha yetu ya Afrika Mashariki.    Ustahamilvu, kusubiri kwa misiba, ushujaa kwa kupigania haki, uadilifu katika kutawala na kuhukumu, kuondoa ubaguzi wa rangi na kabila, kujenga umoja, ukarimu na kuwania kheri ya wenzako kuliko kuwania maslaha ya binafsi - yote haya, na kama haya, yafaa sana sisi tujifunze katika maisha ya mtu huyu wa ajabu, Nabii Muhammad s.a.w.

Katika kitabu hichi tuna bahati nzuri kuwa mwenyewe mtungaji ametuwekea maelezo yake, kwa hivyo tunaweza kuyaelewa makusudio yake bila ya taabu. Katika hayo maelezo pia ametia ushahidi na uthibitisho kwa lolote katika fikra zake ambazo huenda zikaleta makindano yoyote. Kwa fikra zake ambazo huenda zikakhitalifiana na maoni yangu pia namhishimu, kwa sababu amezitolea hoja kwa kadri ya uwezo wake. Na Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi kabisa.

Aghlabu ya Waafrika ni wafuasi wa Mtume Muhammad s.a.w.     Uislamu umeliathiri Bara hili kuliko mabara yote.     Na haya si ajabu, kwani Uislamu ulifika Afrika Mashariki kabla ya kuenda Arabuni kote, bali hata kabla ya kufika Madina.    Kwani walipokuwa wanateswa sana Waislamu, Mtume s.a.w. aliwaamuru baadhi ya wafuasi wanyonge wakimbilie Uhabeshi.    Hapo ilikuwa ni miaka minane kabla ya Madina kusilimu.    Pia miongoni mwa Waislamu wa mwanzo ni Waafrika Mashariki, kama Bwana Bilal r.a. na Mama Baraka r.a. mlezi wake Mtume s.a.w.    Kwa hivyo ni kweli asemavyo mtungaji kuwa Waafrika wanayo haki kudai kuwa dini yao ya asili ni Dini ya Kiislamu.    Hakika ni kuwa wanaadamu wote wanayo haki ya kudai hayo.    Mwenyezi Mungu Anasema katika aya ya 30 ya Suuratir Rum:

Basi uelekeze uso wako katika dini aliyo sawasawa - ndilo umbile Mweyezi Mungu Alilowaumbia watu; hakuna mabadiliko katika maumbile ya viumbe wa Mwenyezi Mungu. Hiyo ndiyo dini iliyo haki, lakini watu wengi hawajui.

Mwenye kutunga utenzi huu ni ndugu kwangu kwa mengi.    Namjua tangu utoto wake, kwani baba yake ni mmoja katika mashekhe zangu wakubwa.    Marehemu Sheikh Muhsin alikuwa mwanafunzi mkubwa wa Sheikh Abdulla Baakathir, na ndiye aliyerithi pahala pake.    Mwanawe Sheikh Muhsin, huyu mtungaji, juu ya kuwa sehemu kubwa ya masomo yake ya dini ameipata kwa baba yake, amesomeshwa pia na wengine; na miongoni mwao ni mimi.    Vile vile kwa miaka isiyopungua kumi na tano, tulishirikiana katika gazeti mashuhuri la zamani la Zanzibar liliokuwa likiitwa Mwongozi, ambalo lilianzishwa na Mabwana Ahmed Seif na Masoud Muhammed.    Mimi nilikuwa ni muhariri wa sahifa ya dini, na yeye alikuwa Muhariri Mkuu wa gazeti.

Abdulla Saleh Farsy
Kadhi Mkuu wa Kenya
Mombasa, Kenya.