9  KUSILIMU KWA U'MARI

 341
Sasa tawapa khabari
Za huyo Bwana U'mari
Alikuwa ni kafiri
Qatili kupindukiya

342
Alikuwa mwenye nguvu
Hukusa watu ziovu
Alikuwa kwa mabavu
Hapana wa kumwingiya

343
Na h'adi aliudhika
Mambo yalivyo chafuka
Dini mpya ilo zuka
Ni mno kaichukiya

344
Alikuwa na a'qili
Lakini hakukubali
Kusikiliza la kweli
Hakutaka kusikiya

345
Hasira ilikithiri
Alipo pata khabari
Isilamu wahajiri
Wenda nchi H'abushiya

346
Akaona uvunjifu
Kwa watuwe watukufu
Kuingia khitilafu
Na wengine kukimbiya

347
Kama watu hawawezi
Yeye takata mzizi
Akomeshe upuuzi
Huo ulio eneya

348
Akainoa h'adidi
Kumchinjia H'amadi
Akampanda jawadi
Maovu kaqus'udiya

349
Na huku amea'zimu
Akamkuta Nua'imu
Huyo bwana kasilimu
Lakini hujifichiya

350
Akiipata khabari
Kaona akifu shari
Akamwambia U'mari:
U'mari nakukhofiya

351
Unadhani watu wake
Watamwacha peke yake
Wataka watu wacheke
A'ibu ikikujiya?

352
Angalia uendako
Sitengeze kwa wenzako
Ukaacha huko kwako
Hali kunateketeya

353
Kwani kwangu kuna nini?
Dadiyo ameamini
Na shemejiyo yaqini
Saidi amefwatiya

354
U'mari hakujijua
Wala hakujitambua
Kwa chuki ya kupasua
Moyoni ilo mwingiya

355
Akaona afulize
Ende nyumbani kwa nduze
La kweli wamueleze
Ajue la kutendeya

356
Akifika mlangoni
Asikia Qur'ani
Akajua kwa yaqini
Ni kweli alo sikiya

357
Kufika Bin Khat'abu
Walikisoma Kitabu
Na mwalimu ni Khababu
Upesi kajifichiya

358
Akija ingia ndani
Shemeji katupwa chini
Mkono uko kooni
Na Fat'uma kaumiya

359
Na dada katakalamu
Na huku atoja damu:
Ni kweli tumesilimu
Tenda utalo tendeya

360
U'mari kamwacha mume
Apumue na aheme
Kanena: Nipe nisome
Mlio kijisomeya

361
Kutupa yake nadhari
Maneno kayakariri
Aliona kama nuri
Ambayo hakudhaniya

362
Aliona muu'jiza
Ambao wamshangaza
Akaapa kwa Muweza:
Amini hatungi haya

363
Hawezi bini Adamu
Kama haya kunudhumu
Sijaonapo utamu
Mithili ya hizi Aya

364
Hapo mwalimu katoka
Na maneno katamka:
Jana Tumwa akitaka
Na mimi kimsikiya

365
Aliomba Mukhtaru:
Rabi Mola unus'uru
Wisilamu kwa U'maru
Ni wewe natarajiy

366
Na hapo Bin Khat'abu
Aliitoa jawabu
Kumuambia Khababu
Nayo ni hii sikiya:

367
Sasa mimi nas'adiqi
Muh'amadi ni wa h'aqi
Nionesheni t'ariqi
Niende kushuhudiya

368
Kunena hayo U'mari
Maovu yawa mazuri
Na hayo yaliyo jiri
Kana kwamba hayakuwa

369
Kalekezwa mah'ashumu
Nyumba yake Arqamu
Was'alipo Isilamu
Na huko wakutaniya

370
Alipo fika U'mari
Wkaona: Hiyo shari
Anakuja tua'ziri
Na balaa tuleteya

371
H'amza alia'zimu:
Nitamtoa wazimu
Jeuri akizuu'mu
Naliwe litalo kuwa

372
Mtume kamkataza
Kwani yeye anaweza
Kwa nguoze kamkaza
Na huku amkemeya:

373
U'mari wataka nini?
Hutwachi na yetu Dini?
Watufwatia nyumbani?
Utakuja angamiya

374
U'mari yake qauli
Sikiza wangu Rasuli
Mimi sijii qitali
Mimi naja shuhudiya

375
Mtume alikabiri
Kumdhukuru Jabari
Walo baqi wakariri
Mayowe kote yeneya

376
Ilikuwa ni
sururi
Kwa Isilamu
h'aqiri
Kwani nguvu za U'mari
Maa'rufu kote piya

377
Yeye si mtu wa kucha
Wala hajui kuficha
Aliapa hatoacha
H'aqi kuitangaziya

378
Kaondoka hapo hapo
Akapita ajuapo
Kwenye watu waketipo
Yalo jiri kuwambiya

379
Kanena bila muh'ali:
Nimemfwata Rasuli
Ndiye Mtume wa kweli
Na Mngu wetu Mmoya

380
Hii ni Dini ya H'aqi
Musitaqimu T'ariqi
Siutaki unafiqi
La kweli taliteteya

381
Makafiri wakazuka
Hapo hapo wambaka
Ikawa ni pata shika
Kila mtu avamiya

382
Yeye ni mtu hodari
Ni mtesi na jabari
Utadhani ni namiri
Majibwa yamkemeya

383
Lakini ni wengi wape
H'ata ingawa mapepe
Yakikithiri matope
Hulishinda jiwe moya

384
Kapigana kwa Imani
H'ata kawa taa'bani
Kabaki aketi chini
Maneno kiwatupiya

385
Haya yote kumfika
Na yeye hakut'osheka
Mtume kenda mtaka:
Ya nini kujifichiya

386
Tuonyeshe Dini yetu
Waijue wote watu
Ni nani wa kuthubutu
Kwa yetu kutuzuiya?

387
Sisi kweli twaifwata
Tusiogope matata
Lolote likitupata
Ni H'aqi twashikiliya

388
Akaona Mua'dhamu
Waridhika Isilamu
Akaongoza qaumu
H'aramuni kwelekeya

389
Wafika Msikitini
Na makafiri pomoni
Wakas'ali Waumini
Na huku wawangaliya

390
Hapo ni kwanza kuweza
Wanyonge kujitokeza
Kumua'budu Muweza
Mbele ya watu jamiya

391
Kiwango kimesha fika
Cha kweli nje kutoka
Hayakuwa kwa haraka
Haya yaliyo tokeya

392
Na mimi tawapa neno
Msikie mlo pano
Huu ni mwaka wa tano
Tangu kuja Unabiya
 
MAFUNZO:

Zingatia ilichukua miaka mitano ya kueneza Uislamu kisirisiri kwa unyonge walio kuwa nao Waumini. Ni majaaliwa ya kupata kusilimu mtu shujaa na mkali kama Sayyidna Umar r.a. ndipo wakaweza kujidhihirisha wazi kwa watu wote. Jambo muhimu lolote lafaa kuanziwa kwa mbinu zake, kisirisiri, mpaka itakapo fika wakati wa kulitangaza. Ubingwa ni kujua lini kuficha, na lini kutangaza.