5.   UJANA

 121
Kufika kumi na mbili
U'mri wake Rasuli
Mtume alikubali
Kwenda Shamu kutembeya

122
Alifwatana na a'mi
Kwendea nchi ya Shami
Kama a'da ya qaumi
Qureshi wano zoweya

123
Ulikuwa mwendo wao
Na ndio uchumi wao
Watu wote wawezao
Riziqi kwenda zengeya

124
Joto linapo shitadi
Ni Shamu hapana budi
Na kipupwe kikizidi
Kusini waelekeya

125
Wakifika mipakani
Wamkuta Nas'arani
Qasisi mwanachuoni
Jinale nitawambiya

126
Bahira huyo Nas'ari
Kanena: Kuna khat'ari
Nakwambia tahadhari
Vitabu vinanambiya

127
Mwanao ni mtukufu
Mteule wa Lat'ifu
Moyo wangu una khofu
Yahudi kuja muuwa

128
Ni bora urudi naye
Au mpe ende naye
Yeyote umwaminiye
Maka aliko tokeya

129
Na yeye Abu T'alibu
Akamtwaa H'abibu
Akawaaga s'ahibu
Nyumbani wakarejeya

130
Mwanafunzi wa padiri
Alikuja kuikiri
Dini yake Mukhtari
Padiri kamuus'iya

131
Aliacha Unas'ara
Kiona Nuru yang'ara
Kaona zote ishara
Bahira alo mwambiya

132
Ndiye Huyo
Salmani
Muajemi wa Irani
Ni S'ahaba mwenye kani
Diniye kupiganiya

133
Muungwana alo bora
Kupita
khamustaa'shara
Kaingia bia'shara
Kuuza na kununua

134
Hali yeye masikini
Wote walimuamini
Wakamuita Amini
S'ifaze zikaeneya

135
Akasikia tajiri
Mwanamke mashuhuri
Kamtaka asafiri
Yamani kusafiriya

136
Amuuzie bidhaa'
Qalili ziso khadaa'
Akaona manufaa'
Faida zikazidiya

137
Huyo bibi mah'ashumu
Faida kaona tamu
Kamtaka ende Shamu
Na mali kamwongezeya

138
Akampa mtumishi
Mtoto kama tarishi
Maisara asoghishi
Wa kwitwa kuitikiya

139
Na huko alipo fika
Mapadiri wamtaka
Tarishi akawitika
S'ifaze kawelezeya

140
Waliyo taka kujuwa
S'ifaze wetu Rasuwa
Na h'ali bado hajawa
Mtume wala Nabiya

141
Na hayo kwisha ambiwa
Mapadiri watambuwa
H'amadi tateuliwa
Kijana wewe sikiya

 142
Dalili zake twaona
Mteuliwa wa Bwana
Vitabu vyetu vyanena
Ni huyu twamngojeya

143
Mambo yote ya a'jabu
Yalo zuka kwa H'abibu
Maisara kakhutubu
Bibiye akamwambiya

144
Maisara kaeleza
Bibiye akasikiza
Mambo hayo akatuza
Moyoni yakamwingiya

145
Na bibi yamuathiri
Walonena mapadiri
Na faida kukithiri
Bibiya kafurahiya

146
Bibi huyu mtukufu
Akaona ni
sharafu
Kuolewa na mwongofu
Apate mtumikiya

147
Na huyo Bibi Khadija
Mtukufu wa
wambeja
Hakukiona
kiroja
Mahari yeye kutoa

148
Kamtuma
shoga yake
Muhamadi amtake
Ampose kwa babake
Na yeye ataridhiya

149
Muh'amadi alipenda
Jambo hilo kulitenda
Mwenyewe yangemshinda
Mahari kujipatiya

150
Wazee kote kuwili
Wafurah'ia mawili
Kupata mke Rasuli
Na Khadija kuolewa

151
Waliketi kwa vizuri
Kwa furah'a na
sururi
Robo qarini
kujiri
Pasi chuki na udhiya

152
Na Bibi huyu mkweli
Alimzaa Batuli
Fat'uma biti Rasuli
Ndiye Bibi wetu piya

153
Wa kwanza wa kusilimu
Katika wote
h'uramu
Wa kwanza wa binadamu
Kums'adiqi Nabiya

154 Watoto wake Rasuli
Wametoka tumbo hili
Ila mmoja
t'ifuli
Kwa Mariya
Qibt'iya

155
Watukufu wa nasaba
Walikuwa wote saba
Yakapita ya ms'iba
Kufa mbee ya Rasuwa

156
Ni jaa'la ya Jalali
Yalo mpata Rasuli
Kufiliwa na
i'yali
Na huku awangaliya

157
Alo baqi baa'daye
Ni Bi Fat'uma pekeye
Ni kutokana na yeye
Wakazaliwa dhuriya

158
Ni yeye Biti Amini
Alo tupa
ithineni
Hasani wal Huseini
Mashahidi wa duniya

159
Fat'uma na Bi Khadija
Watukufu wa wambeja
Ni kweli yashinda hoja
Haya ninayo kwambiya

160
Watukufu kama hao
Wametukuza wenzao
Wanawake wengineo
Wote walio baqiya

161
Mtume wetu kasema:
Chini ya nyayo za mama
Pepo yenu mtachuma
Ndivyo alivyo twambiya

162
Na tena kwetu muh'ali
Pepo kuwa ni halali
Ila tuwe na ahali
Mema tunawatendeya  

MAFUNZO:

Utoto wake na ujana wake Muhammad s.a.w. ni wa kupigiwa mfano. Hata kabla ya kupewa Utume alionyesha kwa wote walio kaa naye kuwa huyu kijana si mtu wa kawaida. Mwendo wake wote ulikuwa ni sawa kabisa. Chambilecho Waswahili: Siku njema huonekana asubuhi. Wenziwe walio kuwa wanamjua vyema walimpanga jina: Assadiq-Al-Amin, yaani Mkweli Muaminifu.
Basi vijana na watoto yawapasa wajaribu kumuiga Mtume Muhammad s.a.w. tangu alivyo kuwa utotoni kwake na ujanani kwake.