1077
Mtume kajitahidi
Kutekeleza a'hadi
Lakini wale fisadi
Walishindwa jizuiya
1078
Maqureshi watu shari
Pamwe na Bani Bakiri
Usiku kisirisiri
Wauwa Bani Khuzaa'
1079
Na kulipo pambazuka
Bani Khuzaa' wafika
Kwa Mtume atamka
Wao malenga sikiya
1080
Kakumbusha kwa shai'ri
Ya zamani walo kiri
Itakapo zuka shari
Waje kuwasaidiya
1081
Maqureshi wamekuja
Mji wao kuufuja
Wameuwa afwaja
1082
Alijibu Muh'amadi
Iandaliwe Jihadi
Kutimiliza a'hadi
A'hadi walo itoa
1083
Walitoka Isilamu
Elfu kumi qaumu
Na wote wamea'zimu
Maka kwenda igomboa
1084
Zingatia tas'awari
Ewe mja wa nadhari
Tangu Tumwa kuhajiri
Mjiwe kuukimbiya
1085
Dhiqi alizo zipata
Mai'sha yake matata
Kila endapo ni vita
A'dui wamfwatiya
1086
Pa kupumua hanako
Kila pahali endako
Aambiwa: Huku siko
Kwa mawe wampopoa
1087
Wakumbuka Muh'amadi
Pamwe na wake Zaidi
T'aifu walipo rudi
Madamu yawaeneya
1088
Na huku kwao nyumbani
Wanaambiwa: Tokeni
Msingie as'ilani
Mtafute pa kwendeya
1089
Pale walipo fukuzwa
Bondeni watokomezwa
Wasile wala kuozwa
Wapate kuteketeya
1090
Kwa muda myaka mitatu
Walipo tengwa na watu
Wasipewe h'ata kitu
Majani wakajiliya
1091
Watuwe wabeuliwa
Watuwe waa'dhibiwa
Watuwe wanauliwa
Mazito wavumiliya
1092
Kulipozidi kutisha
Watuwe kawatorosha
Na wao walipo kwisha
Mwenyewe akakimbiya
1093
Na huko uhamishoni
Wawafwata maluu'ni
Na mjini makhaini
Wachimba wakichocheya
1094
Siku hizo zimepita
Za unyonge na ukata
Za kulazimishwa vita
Wachache wa kuwaniya
1095
Leo hii Mtukufu
Ana umati uluufu
Na wote ni wat'iifu
Anenalo wangojeya
1096
Zamani walo mpiga
Aweza kuwavuruga
Zamani walo mpinga
Aweza kuwavamiya
1097
Walio kimtukana
Hawanalo la kunena
Walio wakijivuna
Kwa leo wanyenyekeya
1098
Sasa yuko milangoni
Hapo nje ya mjini
Na nduguze Waumini
Wote ni kitu kimoya
1099
Kawambia wake umma:
Leo hapa twasimama
Na tuyapige makhema
Na kesho tutaingiya
1100
Maqureshi walo Maka
Nyoyo zao zashituka
Waona nyoto zawaka
Zimetanda kote piya
1101
Waona leo ni leo
Na hapana mengineo
Hii siku ya kilio
Hapana ato saliya
1102
Wakikumbuka maa's'i
Wakazidi wasiwasi
Wajua kuna qis'as'i
Na hicho kitawajiya
1103
Walakini Bwana wetu
Hana uchungu na mtu
Hakutaka fanya kitu
Maovu kuyalipiya
1104
Aliitoa amri
Kwa wote Majamadari:
Msiifanye jeuri
Yeyote kunigusiya
1105
Sitaki mtu kuguswa
Sitaki mtu kupigwa
Sitaki mtu kufyonywa
Ujuba sitoridhiya
1106
Mtume aliyagawa
Majeshi yake kwa sawa
Sehemu nne zikawa
Kila pembe kuingiya
1107
Yeye kangia mjini
Kutoka kaskazini
Walipanda ithineni
Juu ya wake ngamiya
1108
Aliye panda mwenziwe
Ni Usama kijanawe
Ni mtoto wa mwanawe
Mwanawe wa kumleya
1109
Ni mtoto wa Zaidi
Kijana cha Muh'amadi
Aliye kuwa uledi
Nyumbani akakuliya
1110
Kama huu utukufu
Uko wapi tuushufu
Mbora wa Masharifu
Kumtukuza s'abiya?
1111
Na baa'dae Rasuli
Kamfanya Jenerali
Chini yake maqubeli
Warabu wamfwatiya
1112
Aliamuru Mtumi
Awaqabili Warumi
Walo toka kule Shami
Wataka tushambuliya
1113
Naye h'ali ni kijana
Kumi na nane sinina
Nyuma yake waungwana
Usama atanguliya
1114
Tunapewa taa'luma
Kwamba huu wetu Umma
Wa ulimwengu mzima
Na Dini ni ya duniya
1115
Ndiyo Dini ya mapendo
Ndiyo Dini ya mwenendo
Ndiyo Dini ya vitendo
Si maneno kutumiya
1116
Na hapo wetu Rasuli
Pamwe na wake t'ifuli
Juu ya wake ibili
Mjini wakaingiya
1117
Na tena naye Sharifu
Akimaliza kut'ufu
Akanena kwa lut'ufu
Umati kakhut'ubiya
1118
Kamshukuru Rabana
Kuiondoa laa'na
Ya Qureshi kujivuna
Jeuri za Jahiliya
1119
Majivuno ya nasabu
Aliyakanya H'abibu
Si mbora Mua'rabu
Na mwengine naye piya
1120
Mweupe hana ukwasi
Kwa kumshinda mweusi
Sote bila wasiwasi
Ni wa Adamu dhuriya
1121
Na Adamu ni mchanga
Basi huo si ujinga
Kujivuna na kuringa
Udongo ulo anziya?
1122
Na tena hapo Amini
Alisoma Qur'ani
Aya inayo baini
Wote watu ni sawiya
1123
Tumwa tena kauliza:
Ni nini mnalo waza
Kulitenda naliweza?
Qureshi mtanambiya
1124
Wakajibu Makafiri:
Twataraji kwako kheri
Wewe ndugu Mukhtari
Na babiyo naye piya
1125
Mtume tena kasema
Kama Yusufu wa zama:
Hapana kwenu lawama
Ndu zangu Maqureshiya
1126
Tuyasahau ya kale
Tuyasahau milele
Tuyatazame ya mbele
Mola tawaghufiriya
1127
Na tena basi Rasuli
Kamuamuru Bilali:
Adhini tupate s'ali
Na Kaa'ba hiyo kweya
1128
Qureshi wakitazama
Walimuona Usama
Kijana msiriama
Amepanda na Nabiya
1129
Wakitupa macho tena
Bilali wanamuona
Anaitoa adhana
Na watu alinganiya
1130
Wakajua hapo hapo
Ya kale leo hayapo
Mja hulipwa malipo
Kwa analo jitendeya
1131
Hapana tena ugozi
Umekwisha ubaguzi
Hii Dini ya Mwenyezi
Usawa sawa sawiya
1132
Na wengi hapo qaumu
Kuuona ukarimu
Hapo hapo wasilimu
Wachache walibaqiya
1133
Walio baqi Kufari
Hawakutendwa qahari
Kwa ya wenyewe khiari
Wakaja kushuhudiya
1134
Alo kuwa maluu'ni
H'ata akala maini
Ya a'mi yake Amini
Bi Hindi naye kangiya
1135
Kaambiwa na Sharifu:
Mimi dada nakua'fu
Wa zamani upotofu
Umekwisha twondokeya
1136
Naye bibi akataja:
Na hapa nilipo kuja
Kati ya jamii waja
Ni wewe kikuchukiya
1137
Na hivi sasa natoka
Ninakwambia h'aqiqa
Sinaye kumchunuka
Kamawe ewe Nabiya
1138
Ninakupenda yaqini
Kwa dhati yangu moyoni
Akamjibu Amini
Inshalla utazidiya
1139
Ni kwa wema na upole
Alo tenda Mteule
Kawavuta watu wale
Na wote wamwitikiya
1140
Akisha kutengeneza
Na mambo yote kutuza
Njia yake kageuza
Madina akarejeya
MAFUNZO:
Tunajifunza hapa kuwa ahadi ni ahadi. Ukifungana na mtu lazima utekeleze
maagano yenu. Na hapana khitilafu ikiwa uliye fungamana naye ni Muumini mwenzio
au ni kafiri. Mtume s.a.w. amefanya mapatano ya kusaidiana kwa hali na mali na
makafiri Bani Khuzaa ambao ni washirikina. Na kwa ajili yao akatoka kwenda kwa
azma ya kupigana na Maqureshi wa kabila yake, kwa ajili ya kutekeleza ahadi.
Uislamu unatutaka tupiganie uhuru wa watu wote, pasiwepo maonevu. Hiyo ni amri
ya Mwenyezi Mungu kama ilivyo simuliwa katika Qur'ani: "Na lau kuwa
Mwenyezi Mungu hawakingi watu kwa watu, basi hapana shaka zingeli vunjwa nyumba
za wat'awa, na makanisa, na masinagogi, na misikiti ambamo ndani yake jina la
Mwenyezi Mungu linatajwa kwa wingi." (22.40)
Kutenganisha Dini na siasa sio mwendo wa Mtume Muhammad s.a.w. Lakini siasa
ifuate uwongozi wa Dini, sio Dini kufuata siasa.