453
Sasa kidogo twasita
Tuyatatue matata
Tutazame yalo pita
Mtume alipo fiwa
454
Alipo fiwa Mtumi
Na mlinzi wake a'mi
Na mbora wa h'urami
Bi Khadija maridhiya
455
Alitoka Muh'amadi
Kafwatana na Zaidi
Alo kuwa ni waladi
Kijana wa kumleya
456
Wende mji wa T'aifu
Mji wa Bani Thaqifu
Ulomlea Sharifu
Kwa H'alima Saa'diya
457
Ili ende akhubiri
Awape njema khabari
Ya Dini yake Ghafari
Wapate nao hidaya
458
Kaonana na mababa
Kaeleza mat'ilaba
Aliyo pata si haba
Mazito kuvumiliya
459
Akarudi kwa wadogo
Wakamwambia: Mrongo
Wampopoa madongo
Na mawe yamfwatiya
460
Wahuni wote mjini
Wampopoa Amini
Pamwe na wake mwendani
Na huku wamzomeya
461
Madamu yachururika
Mwili wote wapasuka
Wakichoka wawashika
Wamwambia: Tokomeya
562
Walipo choka watwana
Kuwatesa waungwana
Wakapata hapo tena
Kutua na kupumua
463
Pana kivuli cha mti
Wakatua wakaketi
Wenye shamba kwa bahati
Huruma wawaoneya
464
Hao watu Maqureshi
Nao h'ali ni wabishi
Walituma mtumishi
Chakula kuwagawiya
465
Mtumishi kasaili
Akamjibu Rasuli
Hapo hapo filh'ali
Mtumwa kashuhudiya
466
Mabwana wakaudhika
Kwa hayo yaliyo zuka
Na Mtume kaondoka
Jibrili kamjiya
467
Jibrili ashauri:
Nitoe
Walio kutenda shari?
Sasa wataangamiya
468
Muh'amadi kakataa
Kanena: Hao a'saa
Wakaona unang'aa
Muanga wakafwatiya
469
Hawa sasa hawajui
Ndio hivyo wawa wawi
Na zuri hawatambui
Ndio waona wabaya
470
Wao na wao ghulamu
Watapo kuja fahamu
Kitu gani Isilamu
Ni wao watateteya
471
Mwalimu kataa'jabu
Kwa hii yake jawabu
Kanena: Kweli Wahabu
Sifa alo kusifiya
472
Mwenyezi alivyo sema
Kitabuni tunasoma
Wewe Tumwa wa Reh'ema
Kwa viumbe vyote piya
473
Sasa Tumwa akifika
Huko karibu na Maka
Khabari ikamfika
Hana ruhusa kwingiya
474
Hana ruhusa kurudi
Mjini kwake kwa jadi
Aambiwa Muh'amadi
Mzalendo mzaliya
475
Na nini yake lawama?
Kwa kuwa ataka mema
Na kuondoa dhuluma
Na H'aqi apiganiya
476
Na haya tuyaonao
H'ata duniya ya leo
Wale wema watendao
Ndio wanao umiya
477
Wanafukuzwa makwao
Wanyang'anywa kila chao
Wauliwa watu wao
Na wao wavumiliya
478
Kila aliye qatili
Atalipwa na Jalali
Kila aliye dhalili
Malipwa yamngojeya
479
Aliwaomba wajomba
Na Suheli kamuomba
Hunyonya hata la mbwa
La mama ukikoseya
480
Kama a'da ya Warabu
Mtume kenda t'ulubu
Na akapata jawabu
Kukataliwa h'imaya
481
Mut'i'mu kamtaka
Aliye pinga waraqa
Na yeye akamwitika
Akamwambia: Ingiya
482
Mut'i'mu akanadi:
Namlinda Muh'amadi
Naye sasa yuwarudi
Nanyi mtamwangaliya
483
Akaingia mjini
Naye anayo amani
Kama ya a'mi zamani
Qabula hajajifiya
484
Akabaki hii h'ali
Kwa muda myaka miwili
Akikhubiri Rasuli
Dini bila ya udhiya
485
Mii'raji kuja kuwa
Mut'i'mu kachukiwa
H'imaya akayondowa
Maudhi yakarejeya
486
Lakini wetu Rasuli
Fikira hakubadili
Daima yake qauli
Kwa wema humtajiya
487
Japo kuwa Mut'i'mu
Hakuwa Muisilamu
Walakini Mua'dhamu
Wemawe hukumbukiya
488
Yakimfika mauti
Alis'ifiwa kwa beti
Na H'asani wa Thabiti
Kwa amri ya Nabiya
MAFUNZO:
Tunaona kila ambapo mtu wa kawaida anatarajiwa awe na hamaki, na
bughdha, aapize, alipize kisasi, Mwongozi wa kweli huonyesha subira, na huruma
na usamehevu. Na Mtume s.a.w. ni rahimu hata katika shida.