16   MISUKOSUKO YA MADINA

713
Alipoona H'abibu
Ni mji wote qaribu
Kati ya wale Warabu
Wamekwisha shuhudiya

714
Kawataka Mayahudi
Waache yao i'nadi
Wamrejee Wadudi
Waifwate bora njiya

715
Waache mambo machafu
Yalo watia upofu
Wajifanye manadhifu
Watakase yao niya

716
Waingiwe na Imani
Mtume wamuamini
Wamwelekee Manani
Bwana wa wote jamiya

717
Wazitupe khitilafu
Na kila uharibifu
Waifwate ins'afu
Kweli ilo washukiya

718
Kwani kweli waijuwa
Musa alivyo ambiwa
Mtume tateuliwa
Kwa ndu zao A'rabiya

719
Zinatoa ithibati
Zaburi na Taurati
Msitie lenu kati
Na mengine kubaniya

720
Wachache kati ya hao
Khasa hao u'lamao
Wanyooka nyoyo zao
Kusilimu waridhiya

721
Lakini walo kathiri
Walizidi ukafiri
Wafanya wazi na siri
Kumpindua Nabiya

722
Juu ya kuwa Madina
Watu wengi Waumina
Msidhani kuwa tena
Yalikwisha ya udhiya

723
Kwani Shet'ani watuwe
Yafaa haya tujuwe
Hawamwachi apumuwe
Muongozi wa duniya

724
Mangapi wakiyatenda
Ya fisadi na ya inda
Hata lau ninapenda
Siwezi yote wambiya

725
Lakini tayadhukuri
Machache mukhtas'ari
Kama kuwapa nadhari
Mfano yalo tokeya

726
Walikuja watukufu
Wa qabila maa'rufu
Wakamtaka Sharifu
Walimu kuwaidhiya

727
Walidai wana hamu
Watu wao kusilimu
Ili wapate walimu
Wa kuwaonyesha njiya

728
Na Mtume akatowa
Watu sita wano juwa
Na hao wageukiwa
Kwa kamba wawafungiya

729
Kwa kamba wawatatiza
Wende Maka kuwauza
Maqureshi wataweza
Kuwauwa maridhawa

730
Wane walio kataa
Wawauwa kwa fadhaa'
Na wawili walo saa
Maka walis'ulibiwa

731
Hilo jambo la karaha
Kwao ni kuu furah'a
Kuuwa kwao mzaha
Na mateso wachezeya

732
Bwana A'mri kasilimu
Kwa mwenyewe Mua'dhamu
Kasema: Nipe walimu
Nami hapa tasaliya

733
Nipe watu sabii'ni
Wakafunze watu Dini
Tawandikia nyumbani
Kwa wema kuwapokeya

734
Tumwa wetu Muh'amadi
Kheri kamba inazidi
Kumbe wale mashahidi
Si watu wa kubaqiya

735
Aliye pata baruwa
Kinyume alo ambiwa
Akaamuru kuuwa
Kama kuku nakwambiya

736
Walichinjwa hao wote
Pasisalie yeyote
Qiasi kutema mate
Hapana ndudu mmoya

737
Mara ngapi Makafiri
Viunga wavikhasiri
Bilh'adidi-wa-nari
Kuudhi na kuoneya

738
Binti yake Rasuli
Wamtesa Majahili
Kwa fumo achomwa mwili
Pamwe na wake ngamiya

739
Ngamia alo mbeba
Kamtupa Zainaba
Mja mzito na mimba
Na mwishowe kajifiya

740
Na yeye yuwatoroka
Akimbia huko Maka
Babaye anamtaka
Madina akimbiliya

741
Na hao walio tenda
Si wahuni si manunda
Waungwana wa kushinda
Mabwana wa Qureshiya

742
Mara ngapi wazuu'mu
Makafiri kusilimu
Kumbe kuu yao hamu
Wakamuuwe Nabiya

743
Pengine hujia shari
Hugeuka kuwa kheri
Ni kama hii khabari
Ambayo tawelezeya

744
Siku moja huko Maka
Makafiri waso shaka
Waketi wasikitika
Isilamu kwendeleya

745
U'meri akabaini
Laitani si madeni
Na watoto wa nyumbani
Zamani ngejitoleya

746
Ningelikwenda Madina
Muh'amadi kamuona
Kamuuwa nami tena
Haidhuru kuuliwa

747
Na mwenzake kamjibu:
Nenda katende wajibu
Yote uliyo t'ulubu
Mimi nitakuqidhiya

748
Alinena S'afwani:
Enenda wangu mwendani
Kamwondoe duniani
Ano jidai Nabiya

749
Haja zako tazitimu
Tawatazama ghulamu
Deni zako tasilimu
Zote nitakulipiya

750
Akajituta U'meri
Madina akadhihiri
Lakini wetu U'mari
Shaka ikamzidiya

751
Madina akawas'ili
Na upangawe mkali
Na wenye sumu qatili
Maovu kaqus'udiya

752
Kufika msikitini
Kataka ingia ndani
Ana haja na Amini
U'mari kamzuiya

753
Kwanza ampe khabari
Tumwa wake Mukhtari
Inakujia khat'ari
Na mimi nakukhofiya

754
Muh'amadi kamwambiya:
Mwachieni kuingiya
Yupo nasi Maulaya

a mimi namngojeya
755
Lakini naye U'mari
Mja mwingi wa hadhari
Akamshika hodari
Yeye naye waingiya

756
Mtume akamtaka:
Haja gani unataka?
U'meri akaropoka:
Mwanangu nimemjiya

757
Nimekuju kut'ulubu
Mwana wangu mah'abubu
Alo tekwa kwa h'arubu
Mekuja kumkombowa

758
Ni nini ulilo panga
Hata kwingia kwa panga?
Kauliza wa Muwanga
Mtume wetu Nabiya

759
Kwingia msikitini
Na upanga mkononi
Haya mambo tangu lini
Kwa anaye aridhiya?

760
U'meri akabaini:
Nilikuwa ghaflani
Kanena tena Amini
La kweli utanambiya

761
A'hadi mlo peana
Na hata mkapatana
Pamoja na S'afwana
Na mliyo azimiya

762
U'meri kababaika
Mtume yakimtoka
Mambo yote yalo zuka
Ni kama kahudhuriya

763
Mambo yote babu-babu
Kayaeleza H'abibu
U'meri kataa'jabu
Na hapo kaangukiya

764
Ikamtoka qauli:
Nashuhudia kikweli
Kwamba wewe ni Rasuli
Na Mngu wetu Mmoya

765
Tangu hapo huyo Bwana
Akawa na Sayidana
Ni watu wano pendana
Na Isilamu jamiya

766
Ni hayo na yalo fana
Yawapata zetu bwana
Walio kuwa Madina
Wamemfwata Nabiya

MAFUNZO:

Tuone na tusistaajabu tukiona nasi tukitokea kuhama nchi kwa ajili ya dhulma na mateso, na kukimbilia nchi nyengine, tukaona wale madhaalimu tulio wakimbia wakatufatia huko huko uhamishoni kwa ajili ya kuendeleza madhila yao, na fitna zao. Huo ndio mwendo wa makafiri na wanaafiqi, ambao wamefanya dhulma ndio biashara yao. Tunakumbuka vipi kiongozi wa dhulma alivyo kuwa akijitapa kwa kusema kwa kutishia: "Mkono wangu mrefu unafika hata huko waliko." Yaani mkono wake ulio jaa damu anaweza kuwauwa hao walio ondoka popote walipo kimbilia. Lakini:
 Akushutao  mama sihutuke
 Yupi awezao  kukwetea lake
 Watu wana yao  Mungu ana yake
Anaye dai kuwa mkono wake mrefu, siku yake ikifika hutambua kuwa hata kujikuna hawezi.