1189
Aliyo khofu Bakari
Ni hivyo yalivyo jiri
Alitawafu Bashiri
Robo mwaka ukisiya
1190
Kurudi kutoka Maka
H'aliye yadhoo'fika
Kila siku inashuka
H'ata mwisho yamwemeya
1191
Maradhi aliyo mpa
Molawe yalimtupa
Ndiye Yeye wa kutupa
Ndiye Yeye wa kutwaa
1192
Hivyo hivyo ni mgonjwa
Na yeye hujikongoja
Kuzitenda zake h'aja
Za utu na Unabiya
1193
Mzigo wawa thaqili
Aliamuru Rasuli:
Bubukari naas'ali
As'alishe namwambiya
1194
Na siku moja jioni
Ajikongoja Amini
Afika msikitini
Watu wesha jis'aliya
1195
Kwisha s'ali kaeleza
Kwamba Molake Muweza
Mtu alimuuliza:
Waikhiari duniya?
1196
Na mtu hakuqas'iri
Akamjibu Ghafari:
Kuja kwako nakhiari
Ulimwengu nasusiya
1197
Bubakari kafahamu
Madhumuni ya Hashimu
Akaona ni vigumu
Kilio kukizuiya
1198
Akasema kwa uchungu:
Ewe Mtume wa Mungu
Roh'o yangu na wenzangu
Kwako wewe ni fidiya
1199
Tena Mtume kanena:
Wema wake huyu bwana
Washinda ajmai'na
Kwa mali na nafsiya
1200
Enyi wangu Wahajiri
Watunzeni Ans'ari
Vyangu vipenzi khiyari
Ni kwao twakimbiliya
1201
Awatendao h'isani
Huyo mema mlipeni
Na pia msameh'eni
Awatendao mabaya
1202
Tena hapo akarudi
Bwana wetu Muh'amadi
Hakutoka ila h'adi
Siku aliyo zaliwa
1203
Ni siku ya Maulidi
Alifika masjidi
Na watu wai'taqidi
Kaziye atarejeya
1204
Kwisha S'ala kumaliza
Abaqi azungumza
H'adi jua kuchomoza
Na saa zikapitiya
1205
Katika aliyo nena:
Usoni kuna fitina
Na zikisha zipo tena
Na mengi aliwambiya
1206
Ya mwisho yake qauli:
Ya h'aramu na h'alali
Kabisa sikubadili
Kitabu chavyo twambiya
1207
Sinalo la kuongeza
Sinalo la kupunguza
Mwengine akigeuza
Huyo amenizuliya
1208
Alipo rudi nyumbani
Kawa tena taa'bani
Akamwita Rah'amani
Na yeye kamwitikiya
1209
H'ali huku atawafu
Anena wetu Sharifu
Kwa Rafiqi Mtukufu
Hivi sasa namwendeya
1210
Na walio mzunguka
Wakeze wat'ahirika
Naye A'li hakutoka
Kimuuguza Nabiya
1211
Ni yeye na Bi Fat'uma
Kwa upole na huruma
Mtume wamtazama
H'ata mwisho kajifiya
1212
Watu wote wadawaa
Watu wote washangaa
Kuliingia fazaa'
Madina yote jamiya
1213
Bwana A'li hajiwezi
Apigwa na bumbuwazi
Wengine kama wa juzi
Wamekwisha ng'ang'anaa
1214
Shujaa' Bwana U'maru
A'qili zilimduru
H'ata mwisho akufuru
Akanya kufa Nabiya
1215
Aliufuta upanga
Anena: Nitamtwanga
Yeyote ataye pinga
Haya ninaho wambiya
1216
Alinena: Ni muh'ali
Kutawafu Mursali
Na Usilamu ungali
Bado kwenea duniya
1217
Bubakari kiwas'ili
Nyumbani akadukhuli
Kamfunua Rasuli
Usoni kamnoneya
1218
Uso wake una nuri
Wanukia kwa u't'uri
Amuona ni mzuri
Kama walivyo zoeya
1219
Kanena: Sisi shahidi
Kwamba wewe Muh'amadi
Alo kutuma Wadudi
Yote umetimiziya
1220
Na amana ya Karimu
Na h'aqi za wanadamu
Zote hizo ni timamu
Na sisi twashuhudiya
1221
Amani za Mola wetu
Na pia na Rah'amatu
Zishuke kwako mwenzetu
Bukrata wa a'shiya
1222
Alipo toka nyumbani
Kafuza msikitini
Akapanda mimbarini
Na watu kakhut'ubiya
1223
Aliwambia rijali:
Amwabudie Rasuli
Ninawambia la kweli
Muh'amadi kapitiya
1224
Lakini mwenye nadhari
Kumua'budu Qahari
Na zingapita dahari
Moletu atabaqiya
1225
Akasoma Qur'ani
Aya inayo baini
Kutawafu kwa Amini
Na hii nawasomeya

1226
Na nyinyi jama pimeni
Kitabu hichi ni gani
Kila kitu mbayani
Hapana kilo saliya?
1227
Hapo wote wakajuwa
Kwamba kweli yalo kuwa
Kipenzi chao Rasuwa
Amekwisha tanguliya
1228
Ni Mitume wote wale
Wa zamani zile kale
Hawakuishi milele
Wote walisha jifiya
1229
U'mari kajua kweli
Zikamtua a'qili
Karegea wote mwili
Hawezi kujiinua
1230
Na mama yetu Baraka
Alia asikitika
Anena: Zimekatika
H'adithi za samawiya
1231
Na wapi tutayapata
Kama haya yalo pita?
Mwenyezi Mngu
kakata
Aliyo akimwambiya
1232
Huu ms'iba thaqili
Uso kuwa na mithali
Kufa wetu Mursali
Shafii' wa watu piya
1233
Liliwele hali budi
Kutawafu Muh'amadi
Ni kwake Yeye Wadudi
Ndiko aliko kwendeya
1234
Huko sote twakutana
Inshalla tutaonana
Tumuone Sayidana
Kipenzi chetu Nabiya
1235
Na huko tatuongoza
Mbee za Mola Muweza
Tupate yetu majaza
Akhera kama duniya
1236
Sasa hapa twakhitimu
Tums'alie Hashimu
Na S'ahaba mah'ashumu
Na ali zake jamiya
1237
Atuwezeshe Muweza
Kufwata hiyo Ruwaza
Mtume alo maliza
Risala ilo timiya
1238
Wa kwanza wa utukufu
Na kwisha ndio kuqifu
Baa'da yake Sharifu
Hatuh'itaji nabiya
1239
Wano dai nawaseme
Wanaodai ufalume
Wanodai na utume
Si kama waufikiya
1240
Adaivyo ni mzushi
Kudai kwake ubishi
Nao ubishi hawishi
Ndio a'da ya duniya
MAFUNZO:
Mauti ni faradhi. Kila kitu kitateketea ila Mwenyewe Muweza. Mtume
Muhammad s.a.w. Mpenzi wetu, Mwongozi wetu amekufa. Lakini ni kiwiliwili chake
kilicho kufa. Mafunzo yake yako milele, hayafi. Katwachia Qur'ani na Mwenendo
wake. Waajibu wetu tumsome mtu huyu wa ajabu. Kumjua mtu huyu ni mafunzo kwa
kila mwanaadamu. Kwake yeye tunapata uwongozi ambao hatuwezi kuupata popote
penginepo.