17  JIHADI YARUHUSIWA

767
Udugu wa Waumina
Walio kuwa Madina
Mfano wake hapana
Tangu kuumbwa duniya

768
Na sote tunamaizi
Kwamba wale wakimbizi
Walikuwa hawawezi
Lolote kujitendeya

769
Walipo acha makwao
Walitupa kila chao
Wabaqi na nguo zao
Mwilini walizo jiya

770
Walikuja kwa Lillahi
Si kuyajia ya jahi
Wakabeba makruhi
Kuitafuta h'uriya

771
Kwa uh'uru wa i'bada
Wakubali kila shida
Wakimbia zile inda
Za wale Majahiliya

772
Na huku Ma-Ans'ari
Kwa kila jema na kheri
Wakawapa Wahajiri
Vitu vyote bisawiya

773
Wakawapa yao mali
Kila kitu pande mbili
Na wenye wake wawili
Na hao wawagawiya

774
Walikuwa na usawa
Usawa uso na towa
Huwezi kumtambuwa
Faqiri na aghaniya

775
Mwenendo huu mtamu
Wanga nao Isilamu
Mgeni kumkirimu
H'ishima kumfanyia

776
Twashukuru hata leo
Ni wengi tuwaonao
Kamayo wayatendao
Lillahi wajitoleya

777
Lakini wako qalili
Wavunjao jina hili
Wasahau ya as'ili
Dini ilivyo anziya

778
Yafaa tujisemeze
Mazuri tujizoeze
Maovu tusokomeze
Tuache mbovu t'abiya

779
Ni s'ifa ya Isilamu
Kukithiri ukarimu
Kwa mnyonge urah'imu
Mgeni kumpokeya

780
Khas'a huyo mkimbizi
Ndiye mgeni a'zizi
Apendwaye na Mwenyezi
Ni Suna yake Nabiya

781
Atazamwe kwa huruma
Alo kimbia dhuluma
Ana mengi yamuuma
Huwezi kuyaqisiya

782
Tukumbuke si muhali
Mambo kwenda kubadili
Mwenye leo leso mbili
Kesho moja kuzengeya

783
Tuujue ukosefu
Si wa mtu maa'rufu
Kila mtu maus'ufu
Kupata na kukoseya

784
Si a'jabu wewe leo
Wachezea chako cheo
Kesho uko kwa mwenzio
Riziqi wairondeya

785
Sasa hapa tayanena
Yaliyo kuwa Madina
Watu wote jamii'na
Mtume wamwitikiya

786
Hata hao Mayahudi
Wakawa hawana budi
Kumwendea Muh'amadi
Wakiwa nayo qadhiya

787
Akawa yeye h'akimu
Pasiwe wa kudhulumu
Kafiri na Isilamu
Hukumu yao sawiya

788
Na hayo kayasomeni
Isemavyo Qur'ani:
Sihukumu nuqus'ani
Kwa mtu kumchukiya

789
Lakini wale wabishi
Majeuri Maqureshi
Wakaona hayat'oshi
Isilamu kukimbiya

790
Watoka huko waliko
Kuwaletea vituko
Na mingi misukosuko
Mekwisha waelezeya

791
Wakatoka kwao Maka
Na Madina wakafika
Mateka wakiwashika
Na kuharibu mimeya

792
Wakizitia fitina
Huko nje ya Madina
Maqabila mengi tena
Wakawa wayachocheya

793
Ikawa Waisilamu
Hawana la tabasamu
Kwani ni wengi qaumu
Ambao wawachukiya

794
Tena Mwenyezi Qahari
Akaona ni khat'ari
Watu wake mahaqiri
Watakuja angamiya

795
Ni nani wa kutangaza
Huu mwenge wa mwangaza
Likisha ingia giza
Hawa wakaangamiya?

796
Huu Utume wa mwisho
Sileti mwengine kesho
Itakuwa sikitisho
Na ms'iba wa duniya

797
Sioni kuwa wekevu
Bali huo upotovu
Kutoa la pili shavu
Ni nani atasikiya?

798
Huu wakati wa kweli
Wa Muh'amadi Rasuli
Jambo lilio muh'ali
Si Mie wa kuwambiya

799
Akaona aweleze
Wasimame wajikaze
Watu wake wajiweze
Haqi kuipiganiya

800
Ruhusa akaitoa
Ya mja kujigomboa
Dhuluma kuiondoa
Na nguvu kuzitumiya

801
Akaamuru Wadudi
Kumwambia Muh'amadi:
Sasa pigana Jihadi
Na anaye kuoneya

802
Mtu anaye jilinda
Mtu huyo nampenda
Akishindwa akishinda
Peponi nitamtiya

803
Lakini mwenye kuanza
Uchokozi kufanza
Mtu huyo tamtanza
Kwa kuwa amevamiya

804
Walo fukuzwa mijini
Bila kitu nuqus'ani
Ila kuwa Waumini
Ni h'aqi kujiteteya

805
Walo pokwa vitu vyao
Wakachinjwa watu wao
Watendeje watu hao?
Jawabu naingojeya

806
Na wengine mah'aqiri
Wasoweza kusafiri
Wafanyiwa ujeuri
Hawawezi kukimbiya

807
Hao watu madhulumu
Basi kwao si h'aramu
Kupigana na qaumu
Walio leta udhiya

808
Lakini wakikubali
Kuacha hichi qitali
Hima hima simuhuli
Suluh'u kukubaliya

809
Dini jambo la khiari
Halih'itaji qahari
Lakini usis'ubiri
Dhuluma ikaeneya

810
Dhuluma kama mtoto
Ichanatwe kwa ufito
Ikiona uchonoto
A'qili zitatuliya

MAFUNZO:

Haikuwa wepesi kwa Mtume s.a.w. kuingia vitani kwa ajili ya kujilinda na kwa ajili ya kuilinda Haqi. Lakini ilipo kuwa ni lazima, hakusita ila alifanya kwa kila alilo weza kuipinga dhulma kwa kutumia nguvu. Kwa muda wa miaka kumi na nne alistahamili kila maonevu, na kila madhila. Katukanwa, kafukuzwa, kauliwa watu wake, kanyang'anywa kila chake, na mwisho katolewa kwao. Naye kastahamili yote. Ni mwisho tena ilipo kuwa hapana hila ila kujitetea, ndio akapewa ruhusa na Mwenyezi Mungu apigane na ajilinde kwa ajili ya kuipinga dhulma.