951
Sasa hivi naturudi
Huko Madina biladi
Tutazame Mayahudi
Vitendo vyao na niya
952
Mtume wetu karimu
Daima awah'ishimu
Akiwaita isimu
Ya h'ishima na muruwa
953
Aliwaita H'abibu
Enyi Watu wa Kitabu
Hakuwapa chembe tabu
Kufwata yao shariya
954
Na mno kasisitiza
Kwa wema kuwasemeza
Ni mno akikataza
Kuwatendea udhiya
955
Lakini yao fadhila
Ni kufanya kila h'ila
Kumchimba Mursala
Maovu wanuiliya
956
Walipoona Uh'udi
Alishindwa Muh'amadi
Wakaona Mayahudi
Wakati umeadiya
957
Sasa huu ni wakati
Wa kutengeza umati
Wapange wajizatiti
Kumvuruga Nabiya
958
Wakatoka watu wao
Watukufu wenye vyeo
Ni khamsa kubarao
Maqureshi wawendeya
959
Wakasema waa'dhamu:
Tuna mpango mtamu
Kuwasaga Isilamu
Kufumba na kufumbua
960
Sasa wao taa'bani
Tujiunge ikhwani
Tukusanye na wendani
Tuwasage mara moya
961
Tafuteni as'ih'abu
Na sisi tutat'ulubu
Na wengine Waa'rabu
Tuwe sote tu pamoya
962
Na sisi tulio ndani
Ni mchwa wa chini chini
Twaupekecha wat'ani
Siku yetu twangojeya
963
Tunao wetu rafiki
Wawaita wanafiqi
Sisi tunawas'adiqi
Kwa letu watusikiya
964
Na siku itapo fika
Na majeshi yakashuka
Sisi hapo tutazuka
Kwa ndani kushambuliya
965
Maqureshi wakasema:
Hilo ni shauri jema
Tutafanya hima hima
Hilo mlilo lijiya
966
Wakapeana mia'di
Ya kukutana junudi
Wakatoka Mayahudi
Wakashika yao njiya
967
Wakafika majangwani
Kwao Bani A't'afani
Na wao kuwarubuni
Njama zao kuingiya
968
Tena hao maqubeli
Hawakutoa qibali
Mpaka kwa mengi mali
Baa'dhi waliridhiya
969
Alipo pata khabari
Bwana wetu Mukhtari
Watuwe kawashauri
Kwa hayo yalo tokeya
970
Wakapigwa mshangao
Zaemewa bongo zao
Kazuka mmoja wao
Muajemi nawambiya
971
Huyo Bwana Salmani
Alikuwa Nas'rani
Na khalafu kaamini
Kubai'thiwa Nabiya
972
Mwanafunzi wa Bahira
Aliye toa bishara
Ni s'ah'aba wa bus'ara
Mtume kamsikiya
973
Kanena huyo rafiki:
Natulichimbe handaki
Na hilo halipitiki
Hawawezi kutujiya
974
Hii ni rai jadidi
Haijui Muh'amadi
Furaha yake shadidi
Mambo yalipo mweleya
975
Hilo shimo likachimbwa
Na huku nyimbo zaimbwa
Na huku Mungu aombwa
Nus'ura kuwaleteya
976
Huku hali wanachimba
Wakakutana na mwamba
Mtume wakamuomba:
Ni jiwe latuemeya
977
Mtume kateremka
Na mtarimbo kashika
Kapiga pakametuka
Kusini kuelekeya
978
Mtume akatamka
Yamani yatuitika
Karibuni bila shaka
Na hayo ninawambiya
979
Mara nyingine kagonga
Pakachomoza muanga
Kaona hata mjinga
Kaskazi waendeya
980
Tumwa tena kakabiri
Akanena: Nabashiri
Kaskazi ya Nasari
Itakuja twandamiya
981
Mara ya tatu kupiga
Jiwe akalivuruga
Nuru pale akimega
Shariqi yachomozeya
982
Na Mtume kakariri
Ile yake takbiri
Kanena bila kiburi:
Ajemi yashuhudiya
983
Na hayo mambo yazuka
Kama Tumwa kutamka
Nchi hizo zawitika
Wito wa Muhamadiya
984
Kwa mpango huo huo
Alo nena mwenye cheo
Ndiye huyo anenao
Akinena neno huwa
985
Kuchimba wakimaliza
Wamshukuru Muweza
Wabaki wajitengeza
A'dui kumngojeya
986
Hata kwisha Ramadhani
Waona vumbi angani
Wakitazama kusini
Wageni wawajiliya
987
Ni arbaa'ta alaafu
Maqureshi watukufu
Lakini ni wapotofu
Waja mji kuvamiya
988
Hapo hapo wawas'ili
A't'afana Majahili
Lajipanga jeshi hili
Kaskazi shariqiya
989
Na hao watu matata
Wafika elfu sita
S'afu zao zilikuta
Zile za Maqureshiya
990
Ni hao elfu kumi
Waja msaga Mtumi
Ambaye wake qaumi
Elfu tatu kwishiya
991
Tena bado huku ndani
Wapo watu makhaini
Mayahudi maluu'ni
Walo zua yote haya
992
Wangojea siku yao
Ndiyo hii hii leo
Waqidhi muradi wao
Hawa wana wa hizaya
993
Maa'dui wakifika
Nyoyo zao zashituka
Shimo lilivyo zunguka
Hapana pa kupenyeya
994
Ikawa watazamana
Isilamu na watwana
Wabaki wapopoana
Mishale ya kutupiya
995
Mmoja mja mashaka
Alijaribu kuruka
Shingoye ikavunjika
Shimoni katumbukiya
996
Kati ya hao junudi
Kuna shujaa' shadidi
Etwa A'mru Abdu Wudi
Na mwanawe naye piya
997
Ni hao watu wawili
Na Mwana Abu Jahali
Waliruka shimo hili
Na huko wakachupiya
998
Walipima wakaqisi
Wakaruka kwa farasi
Waja waso wasiwasi
Vita wamevizoweya
999
A'mru akajinaki:
Ni nani wakunilaqi
Au nambe hamtaki
Papano kunitokeya
1000
Bwa A'li kainuka
Mtume kenda mtaka
A'mru kumuitika
Kwa anayo waitiya
1001
Mtume kamkataza
Watu wote wanyamaza
A'mru akaongeza
Kuringa na kupaniya
1002
Akazidisha maneno
Hata mwisho yawa mno
A'li asiye kifano
Hakuweza jizuiya
1003
Akanena Bwana A'li:
Ewe wa Mngu Rasuli
Nakuomba jambo hili
Na Mtume kamwachiya
1004
Walipo qabiliana
Na nyuso zikaonana
Bwana A'li alinena:
A'mru
wanisikiya?
1005
Kumbuka yako qauli
Kwamba hutakwi mawili
Ila moja wakubali
Kwa hilo waitikiya?
1006
Aliponena: Naamu
Kasema wetu Imamu:
Nakutaka usilimu
Umkubali Nabiya
1007
A'mru
akabaini:
Siitaki yenu dini
Basi haya shuka chini
Bwana A'li kamwambiya
1008
A'mru
hapo kanena:
Kukuuwa ewe mwana
Sitamani mimi tena
Mwengine namzengeya
1009
Kajibu nduye Amini:
Kukuuwa natamani
Teremka hapa chini
Au nambe wakhofiya?
1010
A'mru
kakasirika
Na farasi kamshuka
Na mapovu yamfoka
Kijana amwangaliya
1011
Wakawa wakitegana
Na huku waoteana
Na mwishowe Sayidana
Dharuba kasukumiya
1012
Dharuba hiyo ni kavu
Kampiga mshupavu
Akamkata ubavu
Maiti ametuliya
1013
Hapo nduye
Muh'amadi
Akampanda jawadi
Kumfwatia waladi
Wa yule alo jifiya
1014
Dakika haikupita
Kichwa chake kakikata
A'liy ajua vita
Jamani ninawambiya
1015
Mwana wa Abu Jahali
Kapachukia pahali
Akaona ni h'alali
Mwanamume kukimbiya
1016
Apate kuwa mwepesi
Juu ya wake farasi
Silaha kaona basi
Vumbini kazitupiya
1017
Baa'da ya hayo kwisha
Hapakuwa mshawasha
Makafiri yawat'osha
Waliyo yaangaliya
1018
Zikapita juma tatu
Za kuketi wale watu
Kuwazingia wenzetu
Hapana pa kuingiya
1019
Wakaanza kugombana
Na wenyewe kusutana
Na Mola wetu Rabana
Kimbunga kaweleteya
1020
Ule usiku wa kiza
Upepo kaupuliza
Mwenyezi Mungu Muweza
Wabaki wawayawaya
1021
Hapana kilichokaa
Kila kitu kinapaa
Watu wote washangaa
Kwa fujo lilo tokeya
1022
Kanadi Bu Sufiyani
Nakwenda zangu nyumbani
Nawambia ikhwani
Hapana la kukaliya
1023
Na kulipo pambazuka
Isilamu kuamka
Waona pames'afika
A'dui amepoteya
1024
Mtume akabashiri
Mji huu Munawari
Hautaona khat'ari
Kafiri kuuleteya
MAFUNZO:
Tunaona kuwa Uislamu ulisimamishwa na watu mbali mbali, wa Bara zote.
Huyu mtu wa Asia, Muajemi Salman Al Farisy, ambaye Mtume s.a.w. jinsi ya
kumpenda kwake hata alisema: Salman minna ahli-l-beit, "Salman ni katika
ukoo wetu." Yeye aliuokoa Uislamu katika uchanga wake kwa kuzua hikima ya
kuchimba handaki kuilinda Madina na Waislamu wachache. Na pia tunaona ushujaa
wa ajabu wa Imam Ali (karama Llahu wajhahu), hali naye kijana wa kiasi labda
miaka 24 kwenda pambana na mijabari hiyo ya kikafiri wajuzi wa vita peke yake.
Huu si ushujaa tu, bali ni Imani ya moyo aliyo kuwa nayo huyu nduguye Mtume
s.a.w. Mtu huyu ndiye aliye itoa roho yake kwa kulalia kitanda cha Mtume,
akajifunika shuka ya Mtume, ili achinjwe yeye badala ya Mtume, pale Mtume alipo
kimbia Makka! Watu kama hao ndio alio kuwa nao Muhammad s.a.w. Ndio maana
Uislamu ukasimama tangu mwanzo, na ukapata nguvu za kutufikia sisi hii leo.