1. Alif Lam Mim: Mwenyezi Mungu Subhanahu wa Taala ameanzia kwa harufi hizi kuashiria moja katika miujiza ya Qur'ani Tukufu iliyo tungwa kwa harufi zile zile ambazo Waarabu wakitungia maneno yao, na juu ya hivyo wao wameemewa hawakuweza kuleta kitu mfano wa Qur'ani hii. Pia juu ya hivyo hizi harufi zinazindua ili upate kuzingatia yasemwayo.
Rudi kwenye Sura

 2. Hichi ndicho Kitabu kilicho kamilika, kisicho kuwa na towa, nacho ni Qur'ani tunayo iteremsha isiyo tiliwa shaka yoyote na kila mwenye akili na mwenye insafu akajua kuwa inatoka kwa Mwenyezi Mungu. Wala haitilii shaka kuwa yasemwayo juu ya mambo na hukumu ni ya kweli tupu. Ndani ya Kitabu hichi upo uwongofu ulio kamilika kwa walio kuwa tayari kuitafuta Kweli, na wanajikinga na madhara na mambo ya kuwaletea adhabu.

Rudi kwenye Sura

 3. Na hawa ndio ambao, kwa kuazimia na kunyenyekea, wanayasadiki yale ya ghaibu wasio yaona kwa macho, wala kuyahisi kwa viungo, ambayo ni ya kuitakidiwa na kuaminiwa, kama mambo ya Malaika, Siku ya Akhera. Kwani msingi wa kushika Dini ni kuamini yaliyo ya ghaibu. Pia wakashika Sala vilivyo, kwa kumwelekea Mwenyezi Mungu na kumnyenyekea kikweli, na wale ambao wanatoa katika yale alio waruzuku Mwenyezi Mungu kwa ajili ya  mambo ya kheri na mema.

Rudi kwenye Sura

 4. Na wale wanao isadiki Qur'ani ulio teremshiwa wewe (Muhammad) kutoka kwa Mwenyezi Mungu, na yote yaliomo ndani yake katika mambo ya hukumu na khabari, na wakatenda yatakikanayo, na wakavisadiki Vitabu vya Mwenyezi Mungu walivyo teremshiwa Manabii na Mitume wa kabla yako, kama Taurati na Injili na vyenginevyo. Kwani risala za Mwenyezi Mungu zote zina asli moja, na hao wanatambulikana kuwa wanaamini Imani moja isiyo legalega ya Siku ya Kiyama na yatayo tokea ya Hisabu na Thawabu na Adhabu.

Rudi kwenye Sura

 5. Hawa walio sifiwa kwa sifa zilizo tangulia, wametua kwa kupata sababu za uwongofu wa Mwenyezi Mungu, na wamekaa imara juu ya hayo. Wao peke yao ndio walio fuzu watakao pata wayatakayo, na wayatamaniayo, nayo ni malipwa kwa kazi yao na juhudi yao, na kutimiza amri na kuepuka waliyo katazwa.

Rudi kwenye Sura

 6. Hii ndiyo hali ya waongofu.  Ama wajinga, majaahili, walio acha kujitayarisha  kwa  Imani  kwa  mapuuza na  kufanya inda,  wasimwitikie Mwenyezi Mungu,  basi  ni sawa kwao ukiwaonya au usiwaonye.

Rudi kwenye Sura

 7. Ukafiri umesaki kwa watu hao, hata imekuwa kama nyoyo zao zimetiwa muhuri, zimezibwa kwa vizibo, haziingii kitu chochote zaidi ya kiliomo ndani yake. Na kama kwamba masikio yao pia yamezibwa, hayasikii onyo lake la kweli, na kama kadhaalika wamefunikwa kwa vitanga vya macho. Hawazioni ishara za Mwenyezi Mungu zenye kuonyesha Imani. Kwa hivyo basi imekuwa  wanastahiki kuwafikilia adhabu iliyo kali.

Rudi kwenye Sura

 8. Na miongoni mwa makafiri wapo watu ambao husema kwa ndimi zao yasiyo kuwamo nyoyoni mwao. Hudhihirisha imani na kusema: "Sisi tunamuamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Kiyama," na wala hawasemi kweli. Basi hao hawaingii katika kundi la Waumini.

Rudi kwenye Sura

 9. Hao makafiri wadanganyifu huwakhadaa Waumini kwa wanayo yafanya, na wao hudhania kuwa wanamdanganya Mwenyezi Mungu. Wanafikiri kuwa Yeye hayajui wanayo yaficha, na kumbe Yeye anayajua ya siri na yanayo non'gonwa. Basi wao kwa hakika wanajikhadaa wenyewe, kwa sababu madhara ya vitendo vyao yatawapata wao, sasa au baadae.  Mwenye kumkhadaa mtu, na akadhani kuwa huyo mtu hajui naye kumbe anajua, basi inakuwa anajikhadaa mwenyewe nafsi yake.

Rudi kwenye Sura

 10. Katika nyoyo za watu hawa mna maradhi ya uhasidi na chuki kwa watu wa Imani, na itikadi zao zimefisidika.  Mwenyezi Mungu basi anawazidishia hayo maradhi yao, kwa ajili ya kuinusuru Haki, kwani hayo yanawaudhi wao kwa sababu ya uhasidi wao, na chuki yao, na inadi yao. Watu hao watapata adhabu iliyo chungu duniani na Akhera kwa sababu ya uwongo wao na upinzani wao.

Rudi kwenye Sura

 11. Na pindi mmojawapo wa walio ongoka akiwaambia hawa wanaafiki:  "Msifanye  uharibifu katika nchi kwa kuipinga Njia ya Mwenyezi  Mungu,  na kueneza fitna, na kuwasha moto wa vita," wao hujitoa  makosani  mwa  uharibifu,   na  husema:   "Kee sisi ndio tunao  tengeneza." Na hayo ni kwa  kuwa  ghururi  yao  imepita mpaka. Huu ndio mwendo wa kila mharibifu, khabithi mwenye ghururi.  Yeye  hudai  kuwa ule uharibifu wake ndio matengenezo na maendeleo.

Rudi kwenye Sura

 12. Enyi  Waumini! Amkeni, mtanabahi, muwatambue kuwa hao ndio mafisadi wa kweli, lakini wenyewe hawautambui ufisadi wao kwa ajili ya ghururi walio nayo, wala hawaitambui adhabu kali watakayo ipata kwa unaafiki wao huu.

Rudi kwenye Sura

 13. Akitokea mtu kuwanasihi na kuwaongoza kwa kuwaambia:"Kubalini yalio waajibu."  Nako ni kuwa muamini Imani safi kama wanavyo amini watu wakamilifu wanao itikia wito wa akili, wao hufanya maskhara na kejeli na husema: "Si laiki yetu sisi kuwafuata hawa wajinga, wapungufu wa akili." Mwenyezi Mungu anawarudi kwa ule ubishi wao na kuwahukumia kuwa ni wao tu ndio wajinga, wapumbavu, lakini wao hawajui kwa ujuzi wa yakini kuwa ujinga na kukosa kuelewa ni kwao wao tu.

Rudi kwenye Sura

 14. Hawa wanaafiki wakiwakuta Waumini wa kweli husema: "Sisi tunaamini hayo hayo mnayo amini nyinyi," yaani kumkubali Mtume na wito wake, "na sisi tu pamoja nanyi katika itikadi."  Wakisha ondoka wakakutana na wenzao wanao shabihiana  na mashetani kwa fitina na ufisadi, huwaambia: "Sisi tu pamoja nanyi katika njia yenu na kazi yenu, lakini tukiwaambia yale hao Waumini kwa ajili ya kuwalazia na kuwadhihaki tu."

Rudi kwenye Sura

 15.  Mwenyezi Mungu Subhana atawalipa kwa huko kudhihaki kwao, na atawaandikia uangamifu unao lingana na hayo maskhara yao na dharau zao. Atawatendea inavyo stahili kutendewa mwenye kudhihaki, na anawapa muhula tu katika dhulma yao iliyo ovu, inayo watia upofu wasiione haki. Kisha khatimaye ndipo atapo watia mkononi kwa adhabu yake.

Rudi kwenye Sura

 16. Na hawa (wanaafiki) kwa kukhiari upotofu badala ya uwongofu wamekuwa kama mfanya biashara aliye khiari kwa biashara yake bidhaa mbovu ya kuchina, basi hafanikiwi kupata faida yoyote. Hupoteza rasilmali yake. Na wao basi hawaongokewi katika 'amali yao.

Rudi kwenye Sura

 17. Hali ya watu hawa katika unaafiki wao ni kama hali ya mwenye kuwasha moto apate nafuu yeye na watu wake. Moto ukisha waka ukatoa mwangaza kunawiri kote, Mwenyezi Mungu  huwaondolea nuru wenye kuwasha wakawa katika giza zito, hawaoni chochote. Kwa sababu Mwenyezi Mungu aliwatunukia sababu za kuongoka, nao hawakuzishika. Kwa hivyo macho yao yakazibwa, wakastahiki kubaki katika kuemewa  na upotovu.

Rudi kwenye Sura

 18. Watu hawa ni kama viziwi, kwani wamepoteza manufaa ya kusikia; hawaisikii Haki kwa msikio wa kuikubali na kuitikia. Nao ni kama bubu, kwa sababu hawatamki la uwongofu au la Haki. Na wao kama vipofu, kwani hawanufaiki kwa macho yao. Hawazingatii na kujikataza. Basi hao hawaachi upotovu wao.

Rudi kwenye Sura

 19. Au mfano wa hali yao katika kubabaika kwao, na hadi ya mambo yanavyo waemea, na kutokufahamu nini liwafaalo na nini linalo wadhuru, ni kama hali ya watu walio teremkiwa na mvua kutoka mbinguni, yenye radi na mingurumo, wanatia ncha za vidole vyao masikioni mwao ili ati wasisikie sauti za mingurumo, na huku wanaogopa kufa, wakidhani kuwa kule kujiziba kwa vidole kutawalinda na mauti.
Watu hao ikiteremka Qur'ani - na ndani yake ikabainisha giza la ukafiri na ikatoa maonyo ya juu yake, na ikabainisha Imani na mwangaza wake unao meremeta, na yakabainishwa mahadharisho na namna mbali mbali za adhabu - wao hujitenga nayo na wakajaribu kuepukana nayo kwa kudai kuwa ati kwa kujitenga nayo wataepukana na adhabu. Lakini Mwenyezi Mungu amewazunguka makafiri kila upande kwa ujuzi wake na uwezo wake.

Rudi kwenye Sura

 20. Huu umeme mkali wa kuonya unakaribia kunyakua macho yao  kwa ukali wake, nao kwa hakika unawamurikia njia kidogo wapate kwenda khatua chache kwa mwangaza wake, na unapo katika umeme kiza kinazidi, basi wao husimama hawajui watendeje, wamepotea. Basi hawa wanaafiki dalili na ishara zinapo watolea mwangaza huwa na hamu ya kutaka kuongoka, lakini mara punde hurejea kule kule kwenye ukafiri na unaafiki.
    Mwenyezi Mungu, Mkunjufu wa uwezo akitaka kitu hukitenda tu, haemewi na chochote katika ardhi wala katika mbingu.

Rudi kwenye Sura

 21. Enyi watu! Muabuduni Mola wenu Mlezi aliye kuanzeni, akakuumbeni akakuleeni, kama alivyo waumba walio kutangulieni. Kwani Yeye ndiye Muumba wa kila kitu. Haya ni hivyo ili mpate kuzitayarisha nafsi zenu, na mzitengeneze kwa ajili ya utukufu wa Mwenyezi Mungu na uangalizi  wake. Kwa hivyo nafsi zenu zitahirike na zipate kuifuata Haki, na ziogope mwisho muovu.

Rudi kwenye Sura

 22. Ni Yeye Mwenyezi Mungu peke yake ndiye aliye itandika ardhi kwa kudra yake, na akaikunjua ili isahilike kwenu kuweza kuikalia na kunafiika kwayo. Akajaalia juu yenu mbingu zilio nyanyuka na sayari zake mfano wa jengo lililo jengwa vilivyo (1), na akakuleteeni njia za uhai na neema - nayo ni maji - aliyo yateremsha kutoka mbinguni, akayafanya ndiyo sababu ya kutoa mimea na miti ya matunda ambayo amekuruzukuni faida yake. Basi haifai baada ya haya mkawaza kuwa Mwenyezi Mungu ana washirika mkawaabudu kama kumuabudu Yeye, kwani Yeye hana mfano wake wala mshirika. Na nyinyi kwa maumbile yenu mnajua kwa yakini kuwa Yeye hana mfano wala mshirika.  Basi msiyaharibu maumbile haya.
(1) Katika Aya hii ipo sehemu ya kuonesha muujiza wa Qur'ani Tukufu: nayo ni kauli yake Mtukufu "mbingu kama paa". Haya asingeyajua Nabii asiyejua kusoma ila kwa ufunuo wa Mwenyezi Mungu, nayo ni kuwa mbingu kwa kisayansi ni kila kilicho izunguka dunia pande zote, na kwa ukomo wowote, na kwa yoyote katika anga, mpaka huko juu kabisa kwenye sayari nyenginezo, zilizoenea zisio na mwisho. Zote hizo zinazunguka kwa mpango wa ajabu, na sisi tunapata uvukuto na mn'gao wake, nazo zinakwenda kwa nguvu ya mvutano kama smaku. Katika sehemu ya mwanzo ya mbingu iliyo tuzunguka lipo anga linalo tukinga kama paa na mianga inayo dhuru kutokana na hizo sayari. Na tabaka hizo huachilia mianga yenye faida tu, ndipo penye mawingu yaletayo mvua. 

Rudi kwenye Sura

 23. Na ikiwa mna shaka kuisadiki hii Qur'ani tunayo mteremshia mja wetu Muhammad, basi mnayo hoja iliyo dhaahiri itayo kubainishieni haki: jaribuni kuleta kama hizi za Qur'ani katika ufasihi wake, na hukumu zake, na ilimu zake, na uwongofu wake wote, na muwaite watakao shuhudia kwamba mmeleta mfano wake, mtake msaada kwao, na wala hamtowapata. Na mashahidi hao ni mbali na Mwenyezi Mungu, kwani Mwenyezi Mungu anamuunga mkono mja wake kwa hichi  Kitabu chake, na anamshuhudia kwa vitendo vyake.  Haya ikiwa ni kweli nyinyi mnaitilia shaka hii Qur'ani.

Rudi kwenye Sura

 24. Basi ikiwa hamtoweza kuleta moja mfano wa hizi za Qur'ani - na kabisa hamtoweza kwa njia yoyote, kwani viumbe hawawezi hayo kwa kuwa Qura'ani ni maneno ya Muumba - basi waajibu wenu mziepuke sababu zitazo kuleteeni adhabu ya akhera, nayo ni Moto ambao utakuwa kuni zake za kuwashia ni hao makafiri na masanamu yao. Moto huu umetengenezwa kwa ajili ya kuwaadhibu wapinzani wenye inda.

Rudi kwenye Sura

 25. Ikiwa hizi ni adhabu za waovu wapinzani, basi Pepo ndio makao ya Waumini.  Waambie wenye kumuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake na Kitabu chake, na wakaikubali haki bila ya kutia shaka au wasiwasi, na wakatenda vitendo vyema - waambie khabari ya kuwafurahisha na kukunjua vifua vyao; nayo ni kuwa Mwenyezi Mungu amewaandalia mabustani yenye mazao, yapitayo mito chini ya miti yake na majumba yake. Kila Mwenyezi Mungu akiwaruzuku matunda ya hizo bustani wao husema: "Haya yamefanana na yale tuliyo pewa kabla."  Kwani matunda haya yanashabihiana kwa , lakini yanakhitalifiana kwa utamu na ladha. Na watakuwa nao humo pia wake walio kamilika walio safi, wasio kuwa na ila yoyote. Na katika Pepo hii wataishi maisha ya milele wala hawatotoka humo.

Rudi kwenye Sura

 26. Mwenyezi Mungu huwaletea mifano watu kueleza hakika ya mambo yalivyo juu, kwa kufananisha na vidudu vidogo na pia vitu vikubwa. Wasio amini waliikejeli hiyo mifano ya vijidudu vidogo kama nzi na buibui. Basi Mwenyezi Mungu aliye takasika haoni aibu kama wanavyo aibika watu kwa kuona haya. Hana la kumzuia asiwape waja wake mfano wowote autakao hata ukiwa mdogo vipi. Kwa hivyo ni sawa kabisa kupiga mfano wa mbu na kilio zaidi kuliko hivyo. Na walio amini wanajua kuwa hii ni mifano, na kuwa huu ni ukweli utokao kwa Mwenyezi Mungu. Ama walio kufuru hawapendi hayo, na husema: "Mwenyezi Mungu anataka nini kwa mfano huu?"  Na mfano kama huu huwa ni sababu ya kupotea wale wasio tafuta haki wala hawaitaki, na huwa ni sababu ya kuwaongoa wenye kuamini na kuitaka haki. Basi hawapotei ila waasi walio kwisha potea.

Rudi kwenye Sura

 27. Na hao walio kwisha potea ni wale ambao wanaivunja ahadi ya Mwenyezi Mungu, na wao ndio wasio ishika vilivyo ahadi ya Mwenyezi Mungu aliyo iweka katika nafsi zao tangu kuumbwa, kuwa ni fungamano la akili yenye kutambua na yenye kuunga mkono Utume, na wakayakata yale aliyo yaamrisha Mwenyezi Mungu yaungwe, kama vile kuwaangalia jamaa, na kupendana na kutendeana mema, na kuoneana hurumu watu kwa watu; na wakafanya fisadi katika nchi kwa mambo maovu na kuzua fitna na kuchochea vita na kuharibu majenzi. Hao ndio wenye kuleta khasara kwa kufisidi khulka yao walio umbwa nayo, na wakawagawa watu mapande mapande, badala ya kuleta mapenzi na kuoneana huruma kama inavyo stahiki. Kwa vitendo vyao hivyo watapata hizaya duniani na adhabu huko Akhera.

Rudi kwenye Sura

 28. Hakika hali yenu instaajabisha! Vipi mnakufuru na wala hapana sababu yoyote ya kutegemewa katika kukufuru kwenu? Ukiangalia hali yenu utaona inakataa ukafiri huu wala hamna udhuru wowote. Kwani nyinyi mlikuwa maiti, hamna uhai, akakuumbeni Mwenyezi Mungu na akakupeni uhai na umbo zuri. Kisha ni Yeye atakaye kurejezeni muwe maiti baada ya kutimia wakati wenu. Kisha atakufufueni muwe hai mara nyingine kwa ajili ya hisabu na malipo.  Kisha mtarejea kwake, wala hamwendi kwa mwenginewe, mtarejea, kwa ajili ya hisabu na malipwa kwa vitendo vyenu.

Rudi kwenye Sura

 29. Mwenyezi Mungu anaye pasa kuabudiwa na kut'iiwa ndiye aliye kufadhilini. Akaumba kwa ajili ya manufaa na faida yenu kila neema inayo patikana duniani, kisha baadae akazielekea mbingu akaziumba mbingu saba kwa mpango. Katika hayo yapo mnayo yaona na msiyo yaona. Na Mwenyezi Mungu amevizunguka vitu vyote, na anavijua vyote.

Rudi kwenye Sura

 30. Mwenyezi Mungu, Subhanahu, Aliye Takasika, amebainisha kuwa ni Yeye ndiye aliyempa uhai mtu, na akamweka duniani. Kisha amebainisha vile vile asli ya kumweka mwanaadamu na ujuzi aliyo mpa, na akakumbushwa hayo. Basi kumbuka, ewe Muhammad, neema nyingine ya Mola wako Mlezi kumpa mtu, nayo ni pale alipo waambia Malaika: Mimi nitajaalia awepo katika ardhi mfwatizi, ambaye nitamweka hapo, na nimpe madaraka, naye ni Adam na vizazi vyake. Mwenyezi Mungu atamweka kama Khalifa, au naibu wa kuimarisha dunia, na kutekeleza amri, na kuzitengeneza nafsi. Malaika wakauliza kutaka kujua nini siri ya hayo, wakasema: Je, utaweka katika ardhi atakaye leta uharibifu humo kwa maasi, na atakaye mwaga damu kwa uadui na mauwaji kwa kufuata tabia yake ya matamanio, na ilhali sisi tunakutakasa na yasiyo laiki na utukufu wako, na tunasafisha kumbusho lako, na tunakutukuza?  Mola wao Mlezi akajibu: Mimi ninajua maslaha ya hayo msiyo yajua nyinyi.

Rudi kwenye Sura

 31. Na baada ya Mwenyezi Mungu kwisha kumuumba Adam na akamfundisha majina ya vitu vyote na sifa zao ili atue katika ardhi na anufaike navyo, aliwaletea hivyo vitu Malaika na akawaambia: Niambieni majina ya vitu hivi na sifa zao kama kweli nynyi ndivyo kama mnavyo dhani kuwa mnastahiki kupewa madaraka katika ardhi, na kuwa hapana aliye bora kuliko nyinyi kwa sababu ya ut'iifu wenu na ibada zenu.

Rudi kwenye Sura

 32. Malaika wakatambua upungufu wao, wakasema: Sisi tunakutakasa Ewe Mola wetu Mlezi kwa mtakaso ulio laiki nawe. Tunakiri kuwa tumeshindwa, na hatuwezi kupinga. Kwani hatuna ilimu kuliko uliyotupa Wewe, na Wewe ndiye Mjuzi wa kila kitu, na Mwenye hikima na hukumu katika kila jambo ulitendalo.

Rudi kwenye Sura

 33. Mwenyezi Mungu alimwambia Adam: Watajie Malaika khabari za vitu hivi. Akataja; na ukadhihiri ubora wake juu yao. Na hapo Mwenyezi Mungu akawaambia kuwakumbusha vipi ujuzi wake ulivyo enea: Sikukwambieni kuwa Mimi ninajua siri za mbingu na ardhi, na hapana ajuae hayo isipo kuwa Mimi, na Mimi ninajua mnayo yadhihirisha katika kauli yenu, na mnayo yaficha katika nafsi zenu.

Rudi kwenye Sura

 34. Na kumbuka Ewe Nabii! Tulipo waambia Malaika: Mnyenyekeeni Adamu kwa kumwamkia na kuukiri ubora wake. Wakat'ii Malaika wote ila Iblis. Yeye alikataa kusujudu akawa miongoni mwa walio asi, walio zikataa neema za Mwenyezi Mungu, na hikima yake, na ujuzi wake.

Rudi kwenye Sura

 35. Kisha Mwenyezi Mungu alimuumba Adam na mkewe, na akawaamrisha wakae katika Bustani ya neema. Akamwambia: Kaa wewe na mkeo katika Bustani hii na kuleni humo mtakavyo vya kutosha bila ya kutaabika, na kaeni mtakapo, mle mtakacho. Lakini Mwenyezi Mungu aliwatajia mti maalumu na akawahadharisha wasiule, na akawaambia: Msiukaribie mti huu, wala msile matunda yake. Mkifanya hivyo mtakuwa miongoni mwa walio dhulumu, na mtakuwa waasi.

Rudi kwenye Sura

 36. Lakini Iblis, anaye mhusudu na kumchukia Adam, alimfanyia    vitimbi, akawadanganya mpaka wakateleza wakala mti walio katazwa.  Mwenyezi Mungu akawatoa katika ile neema na ukarimu walio kuwa nayo. Mwenyezi Mungu Mtukufu akawaamrisha washukie kwenye ardhi waishi humo wao na vizazi vyao, na wawe na uadui baina yao kwa wao kwa sababu ya ushindani na kupotozwa na Shetani. Na huko kwenye ardhi pawe pahali pa kukaa kwao na kupata maisha, na kustarehe kutako kwisha kwa kutimia wakati.

Rudi kwenye Sura

 37. Adam na mkewe walitambua  makosa yao na kujidhulumu nafsi zao. Mwenyezi Mungu Mtukufu alimfunza Adam baadhi ya maneno ya kutubia na kuomba msamaha na akayasema. Mwenyezi Mungu alimkubalia toba yake, na akamsamehe, kwani Yeye ni mwingi wa kukubali toba, naye ni Mwenye kuwarehemu waja wake wanyonge.

Rudi kwenye Sura

 38. Tukamwambia Adam na mkewe na vizazi vyao vijavyo na Iblis: Shukeni katika ardhi, na huko mtalazimishwa mambo.  Yakikujieni hayo kutokana na Mimi - na hapana shaka yatakujieni - basi wale watakao itikia amri yangu, na wakafuata uwongofu wangu hawataona khofu yoyote, na hawatopata huzuni, kwa kukosa thawabu, kwa sababu Mwenyezi Mungu hapotezi ujira wa atendaye mema.

Rudi kwenye Sura

 39. Na wale ambao watapinga na watawakanusha Mitume wa Mwenyezi Mungu na Vitabu vyake, hao ni watu wa Motoni, watabaki huko milele, wala hawatatoka wala hawatakufa.

Rudi kwenye Sura

 40. Enyi Wana wa Israili kumbukeni neema zangu nilizo kutunukieni nyinyi na wazee wenu kwa kuzifikiri na kushukuru na kutimiza agano langu nililo lichukua kwenu (1) , na nyinyi nafsi zenu mkalikiri, nalo ni Imani, na Vitendo vyema, na kuwasadiki Manabii wajao baada ya Musa, ili Nami nitimize ahadi yangu kwenu, nayo ni kukulipeni malipo mema, na neema ya kudumu.  Na wala msimwogope mtu yeyote isipo kuwa Mimi, na tahadharini na kufanya mambo yatakayo nifanya nikasirike nanyi.
(1) Aya hii inaonyesha kuwa ahadi, au agano, ni waajibu wa pande zote mbili zilizo ahidiana kutimiza lilio lazimika. Akiacha mmojapo basi haimlazimu wa pili kutimiza agano lake.

Rudi kwenye Sura

 41. Na isadikini Qur'ani iliyo teremshwa kusadikisha vile vitabu mlivyo navyo, na kufunza Tawhidi (kuwa Mwenyezi Mungu ni mmoja) na kumwabudu Mwenyezi Mungu, na uadilifu baina ya watu.  Wala msikimbilie kutaka kuipinga Qur'ani msije mkawa ndio wa mwanzo kuikanya, na ilhali ifaavyo nyinyi ndio muwe wa mwanzo kuiamini.  Wala msiziache Ishara za Mwenyezi Mungu mkenda badala yake mkachukua chenginecho kipitacho njia katika starehe za uhai wa dunia. Na niogopeni Mimi tu, na fuateni Njia yangu, na wacheni upotovu.

Rudi kwenye Sura

 42. Wala msichanganye Haki iliyo toka kwangu na upotovu mlio uzua  nyinyi,  hata ikawa halijuulikani la kweli na la uwongo.  Wala msiifiche Haki, na katika hiyo Haki ni kumsadiki Muhammad, na nyinyi mnajua kuwa yeye ni wa kweli na wa kusadikiwa.

Rudi kwenye Sura

 43.  Itikieni  Imani.   Shikeni  Sala  yenye  nguzo  zilizo simama baraabara. Na toeni Zaka muwape wanao stahiki. Na salini pamoja na jamaa wa Kiislamu ili mpate malipo ya Sala na thawabu za kusali jamaa. Na haya yanalazimu kuwa muwe Waislamu.

Rudi kwenye Sura

 44. Je, mnawataka watu wafanye kheri, na wajilazimishe ut'iifu, na waache maasia, kisha nyinyi hamtendi myasemayo, wala hamjilazimishi nafsi zenu kwa yale myatakayo?  Kwa hivi mnajipoteza nafsi zenu, kama kwamba mmezisahau, na ilhali nyinyi mnasoma Taurati na ndani yake pana maonyo na mikemeo kwa mwenye kusema asilo litenda. Basi nyinyi hamna akili ya kukuzuieni na kwenda mwendo huu wa kutukanisha?

Rudi kwenye Sura

 45.  Na tafuteni msaada wa kutekeleza waajibu kwa subira na kuizuia nafsi isitende  yanayo udhi. Katika hayo ni kwa kufunga Saumu, na kwa Sala ambalo ni jambo kubwa lenye kuusafisha moyo na kuzuia kutenda machafu na maovu, na kwa hivyo ndio yakawa mazito ila kwa wenye kupenda ut'iifu ambao nyoyo zao zimetulia kwa kumkumbuka Mwenyezi Mungu.

Rudi kwenye Sura

 46. Hao ndio wanyenyekevu walio tulia nyoyo zao, ambao wanaiamini Siku ya mwisho, na wana yakini kuwa watakutana na Mola wao Mlezi wakati wa kufufuliwa, na kwake Yeye pekee ndio watarejea ili awahisabie kwa yale waliyo yatenda na awalipe kwayo.

Rudi kwenye Sura

 47. Enyi Wana wa Israili!  Kumbukeni neema zangu nilizo kuneemesheni kwa kukutoeni katika dhulma ya Firauni, na nikakuongoeni na nikakuwekeni imara katika nchi baada ya kuwa mlikuwa mkionewa humo.  Mshukuruni kwa kumt'ii Mwenye kukutunukieni hayo. Na kumbukeni kuwa Mimi niliwapa baba zenu mlio zalikana kutoka kwao nisiyo wapa wowote wengineo wakati wenu. Haya wanaambiwa taifa la Mayahudi walio kuwako zama za Mtume.

Rudi kwenye Sura

 48. Iogopeni Siku ya Hisabu kali, Siku ya Kiyama, siku ambayo hapana mtu ataeweza kumtetea mtu, na wala hapana mtu ataye mfaa mtu, wala hakubaliwi mtu kuleta mwombezi, kama ilivyokuwa hatokubaliwa mtu kutoa fidia ya dhambi, wala hapana mtu ataye weza kuizuia adhabu isimpate mwenye kustahiki.

Rudi kwenye Sura

 49. Na kumbukeni katika neema zetu juu yenu kuwa tumekuokoeni kutokana na mateso ya Firauni na wasaidizi wake walio kuwa wakikuonjesheni adhabu kali kabisa, kwa kuwa wakiwachinja wana wenu wanaume - kwa khofu kuwa miongoni mwao atatokea wa kupindua utawala wa Firauni - na wakiwabakisha wanawake ili wawafanye wajakazi wao wa kuwatuma.  Na katika adhabu hizi na uteketezaji huu wa umma ni majaribio makuu kutokana kwa Mola wenu, na ni mtihani mkuu kwenu.

Rudi kwenye Sura

 50. Kumbukeni vile vile katika neema alizo kuneemesheni Mwenyezi Mungu pale tulipo kupasulieni bahari - na tukayagawa maji katikati ili mpate kupita - mkaokoka, Firauni na askari wake wasikupateni. Na kwa fadhila yetu mkavuka na tukawapatiliza adui zenu kwa sababu yenu, tukawazamisha mbele ya macho yenu. Nyinyi mkawa mnawaona wanazama, na bahari ikiwafunika baada ya nyinyi kwisha vuka salama.

Rudi kwenye Sura

 51. Na  kumbukeni  wakati  Mola  wenu alipo agana na Musa muda wa masiku (1) arubaini kwa ajili ya mazungumzo. Alipo kwenda walipo agana na akarejea alikukuteni mmekwisha geuka, na mkamfanya ndama aliye muunda Saamiriyu ndiye wa kuabudiwa. Mkawa kwa hivyo ni wenye  kudhulumu  kwa  kumfanyia Mwenyezi Mungu aliye kuumbeni na kukuokoeni ana mshirika wake.
(1) ("Masiku" ni wingi wa Usiku. Wingi wa siku ni siku, kama ilivyo sahani, sabuni, silaha, sinia, sungura, saa. Ni makosa kwa Kiswahili kusema "masiku" kuwa ni wingi wa siku; "Masiku" ni wingi wa "Usiku". Kutumia "Masaa" kuwa ni wingi wa "Saa" ni makosa.)

Rudi kwenye Sura

 52. Kisha tukakusameheni na tukaifuta adhabu yenu mlipo tubu na mkapata  msamaha kwa dhambi zenu, ili mpate kumshukuru Mola Mlezi wenu kwa huko kufuta kwake makosa yenu, na kusamehe kwake, na fadhila zake.

Rudi kwenye Sura

 53. Na kumbukeni tulipo kuneemesheni kwa kukumteremshia Nabii wenu Musa Kitabu chetu Taurati, Kitabu ambacho kinafarikisha baina ya Haki na baat'ili, na kinabainisha baina ya Halali na Haramu, ili mpate kupata uwongozi kwa nuru yake na muongoke kutokana na upotovu kwa kuzingatia yaliyomo ndani yake.

Rudi kwenye Sura

 54.  Ikumbukeni  siku  alipo kwambieni Mtume wenu Musa: Enyi watu wangu! Mmejidhulumu  kwa kumchukua ndama wa Saamiriyu mkamuabudu. Basi tubuni kwa Mola wenu aliye kuumbeni kabla hamjawa kitu, kwa kuzighadhibikia nafsi zenu ovu zenye kuamrisha maovu, na zifanyeni hizo nafsi ziwe nyonge, ili mpate nafsi mpya zilio safi. Mwenyezi Mungu alikusaidieni kwa hayo na akakuwezesheni mkaweza, na hiyo ni kheri itokayo kwa Muumba wenu. Na haya ni kabla ya kutubu kwenu, Naye akakusameheni. Kwani Yeye ni mwingi wa kukubali toba kwa waja wake, na mwingi wa kuwarehemu.

Rudi kwenye Sura

 55. Na kumbukeni kauli yenu mlio mwambia Musa: Kwamba sisi hatukukubali wewe mpaka tumwone Mwenyezi Mungu waziwazi hivi hivi kwa macho bila ya kificho. Ikakuchukueni radi na moto kutoka mbinguni, ikakutikiseni  kuwa  ni  malipo ya inadi yenu na dhulma zenu,  na  kutaka  kwenu  jambo  ambalo  ni muhali kutokea kwenu. Nanyi mnaiona hali yenu na balaa na adhabu zilizo kusibuni kwa mpigo wa radi hiyo.

Rudi kwenye Sura

 56. Kisha tukakuzindueni kutokana na huko kudawaa kwenu na kupwelewa, na tukakufundisheni ili mpate kuishukuru neema yetu kwa hayo, na mpate kuiunga mkono Haki ya Mwenyezi Mungu kwa kupitia njia ya shukrani hii.

Rudi kwenye Sura

 57. Na katika fadhila zetu juu yenu ni kuwa tumekuleteeni mawingu yawe kama ni kivuli kukulindeni na mwako wa jua kali, na tukakuteremshieni Manna, nacho ni kitu kitamu kama asali kinaanguka juu ya miti linapo chomoza jua. Kadhaalika tumekuteremshieni Salwa, naye ni ndege aliye nona, nao wakikujieni kwa makundi asubuhi na jioni ili mle mstarehe. Na tukakwambieni: Kuleni vilivyo vyema katika riziki yetu.   Hawa watu wakaikufuru neema. Na haya hayakutudhuru Sisi, lakini wamejidhulumu nafsi zao. Kwani madhara ya uasi unawarejea wao watendao.
Katika kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu: "Na tukakuteremshieni Manna na Salwa" imetajwa kwa uhakika wa kisayansi, kwani hivi mwishoni imevumbuliwa kuwa madda za "Protein" zenye asli ya vinyama kama vile nyama na ndege ni bora kumfaa mtu kwa chakula kuliko "Protein" zinazotoka katika mimea na mboga. Na katika Manna mna sukari ya kumpa mtu nguvu na uchangamfu wa kufanyia kazi na kutaharaki huku na huku.

Rudi kwenye Sura

 58. Na kumbukeni enyi Wana wa Israili! Tulipo kwambieni: Ingieni katika mji mkubwa aliyo kutajieni Nabii wenu Musa na mle katika viliomo humo kama mnacho kitaka, kwa wingi na kwa wasaa, kwa sharti lakini kuwe kuingia kwenu kwa upole na unyenyekevu, kupitia mlango aliyo utaja Nabii wenu. Na kwamba hapo mumuombe Mwenyezi Mungu akusameheni makosa yenu. Kwani mwenye kufanya hayo kwa ikhlasi, usafi wa niya, tunamfutia makosa yake. Na mwenye kuwa mtenda mema aliye mt'iifu tunamzidishia thawabu na ukarimu juu ya kumsamehe na kumfutia dhambi.

Rudi kwenye Sura

 59. Lakini walio dhulumu walikwenda kinyume na amri za Mola wao Mlezi, waksema sio walio amrishwa wayaseme, kwa kudhihaki na kuasi. Basi jaza yao ni kuwa Mwenyezi Mungu aliwateremshia juu yao adhabu kuwa ndiyo malipo ya ukosefu wao na kuzivunja amri za Mola wao Mlezi.

Rudi kwenye Sura

 60. Na kumbukeni, enyi Wana wa Israili, siku Nabii wenu Musa alipo taka maji kutokana na Mola wake Mlezi kiliposhtadi kiu jangwani, Nasi tukakurehemuni.  Tukamwambia Musa: Lipige jiwe kwa fimbo yako, yakatimbuka maji kutoka chemchem kumi na mbili. Kila kikundi na chemchem yake, na walikuwa makundi thinaashara.  Basi kila kabila ikawa na pahala pake pa kunywea. Na tukakwambieni: Kuleni Manna na Salwa, na kunyweni maji haya yanayo timbuka, na muwache mlio nayo, wala msipite mipaka kwa uharibifu katika nchi, bali wacheni maasia.

Rudi kwenye Sura

 61. Na kumbukeni pia, enyi Mayahudi, pale wale wazee wenu walio tangulia walipo zidi jeuri zao, wasiipe neema ya Mwenyezi Mungu haki yake, wakamwambia Musa:  Sisi hatutovumilia chakula hicho kwa hicho (nacho ni Manna na Salwa). Basi muombe Mola wako atutolee katika ardhi mboga, na matango, na adesi, na thom na vitunguu. Musa aliyastaajabia haya na wala hakupendezewa nayo. Akawaambia: Hivyo nyinyi mnafadhilisha vyakula namna hii kuliko vilivyo kuwa bora zaidi na vizuri zaidi, navyo ni Manna na Salwa? Basi shukeni kutoka Sinai, na ingieni katika mji mmojawapo na huko mtapata hivyo mnavyo vitaka.  Na kwa sababu ya kutoridhika kwao huko na inda yao hao Mayahudi walipigwa na madhila, na ufakiri na unyonge, wakastahiki kupata ghadhabu ya Mwenyezi kwa ule mtindo wao wa inda na uasi, kukanusha ishara za Mwenyezi Mungu, na kuwauwa Manabii. Kwa haya ikawa wanaacha Haki iliyo kwisha thibiti na kukubalika. Yaliyo wapelekea hata wakaingia katika ukafiri ule na mauwaji yale ni kule kuziachia nafsi zao kupanda maasi na kufanya uadui na kupindukia mipaka katika maasia.

Rudi kwenye Sura

 62. Wale walio amini, nao ni Manabii wa zamani, na Mayahudi, na Wakristo, na wanao tukuza nyota na malaika, na wanao uamini ujumbe wa Muhammad baada ya kuteuliwa kuwa ni Mtume, na wakaamini kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu ni Mmoja wa pekee, na wakaamini kuwa kupo kufufuliwa na kuhisabiwa Siku ya Kiyama, na wakatenda vitendo vyema duniani, basi watu hawa wana malipwa yao yaliyo wekewa kwa Mola wao Mlezi.  Wala haitowapata khofu ya kuadhibiwa, na wala haitowafika huzuni kwa kukosa thawabu.  Na Mwenyezi Mungu haupotezi ujira wa mwenye kutenda mema.

Rudi kwenye Sura

 63. Kumbukeni pale tulipo chukua ahadi na agano juu yenu, tukaunyanyua mlima wa T'uur, tukaufanya kwa uwezo wetu kama kivuli juu yenu mpaka mkaogopa mkanyenyekea, tukakwambieni: Shikeni uwongofu na uwongozi tulio kupeni kwa nguvu na jitihadi, na mkumbuke kwa kutekeleza na kutenda yaliyo tajwa ndani ili mpate kujilinda nafsi zenu msipate adhabu.

Rudi kwenye Sura

 64. Tena baada ya hayo yote mkageuka.   Na lau kuwa si fadhila na rehema ya Mwenyezi Mungu juu yenu kuiakhirisha adhabu kwenu mngeli kwisha kuwa miongoni walio potea na kuangamia.

Rudi kwenye Sura

 65. Na  nyinyi  bila  ya  shaka  mliwajua  wale walio pindukia mipaka katika siku ya Sabato, siku ya ibada na mapumziko, siku ya Jumaamosi.  Pale walipo  kwenda  kuvua  samaki siku hiyo na ilhali siku hiyo ilikuwa imetengwa iwe ni siku ya mapumziko na siku kuu, na kufanya kazi siku hiyo ilikatazwa. Mwenyezi Mungu alizipotoa nyoyo za wakosefu wale, wakawa kama  manyani katika pumbao lao na matamanio yao.  Tukawaweka  mbali  na  rehema ya Mwenyezi Mungu, wakifukuzwa kama mijibwa, watu hawataki kukaa nao, na wanawanyanyapaa kuchanganyika nao.

Rudi kwenye Sura

 66. Mwenyezi Mungu ameifanya hali yao namna hii waliyo ifikia ili iwe ni kama funzo na onyo kwa wengineo, wasitende  kitendo kama  hichi. Ameyafanya haya ili yazingatiwe na watu wa nyakati zao na watakao kuja baada yao, kama tulivyo yafanya kuwa ni mawaidha kwa wale wanao mcha Mola wao Mlezi, kwani wao ndio wanao nafiika kwa maonyo ya mawaidha na mazingatio.

Rudi kwenye Sura

 67. Na kumbukeni pale alipo uliwa mtu na asijuulikane muuwaji, Musa akawaambia watu wake: Mwenyezi Mungu anakuamrisheni mchinje ng'ombe ili iwe ndio ufunguo wa kumgundua muuwaji. Lakini wakaona hayo ni mageni, baina ya yale mauwaji na kumchinja ng'ombe. Wakasema: Unatufanyia maskhara wewe Musa? Yeye akawajibu: Mimi najilinda kwa Mwenyezi Mungu asinipatilize kwa kuwa katika wajinga wanao wadhihaki waja wake.

Rudi kwenye Sura

 68. Tena wakamwambia Musa wakirejea lile shauri la ng'ombe: Tutakie kwa Mola wako Mlezi atubainishie sifa za huyo ng'ombe. Akawaambia: Mwenyezi Mungu ameniambia huyo ng'ombe si mkubwa wala si mdogo, bali yu katikati baina ya upevu na uchanga. Basi hebu tekelezeni alivyo kuamrisheni Mwenyezi Mungu

Rudi kwenye Sura

 69. Lakini walikakamia katika kutaradadi kwao, wakasema: Tutakie kwa Mola wako Mlezi  atupambanulie nini rangi yake. Akawajibu: Mwenyezi Mungu anasema: Ng'ombe huyo ni wa rangi ya manjano iliyo koza, na safi. Ukimtazama anapendeza kwa usafi wa rangi yake ilivyo zagaa.

Rudi kwenye Sura

 70. Tena wakashikilia kuuliza kwao, wakasema: Tuombee kwa Mola wako Mlezi atupambanulie khasa huyo ni yupi? Kwani ng'ombe wanatudanganyikia sisi, hatujui. Na Inshallah, Mwenyezi Mungu akipenda, sisi tutaongokewa tumjue.

Rudi kwenye Sura

 71. Musa akawambia: Mwenyezi Mungu anasema kuwa ng'ombe huyo bado hajatiwa kazini kwa kulima wala kumwagia maji shambani kwa ajili ya makulima. Naye hana ila yoyote, mzima kabisa, wala katika mwili wake hana kibaka chochote, wote ni wa rangi moja. Hapo tena wakamwambia: Sasa umepambanua vilivyo. Wakamtafuta ng'ombe mwenye sifa hizo wakamchinja. Na walikuwa wamekaribia wasifanye hayo kwa kukithiri masuala yao na wingi wa kushikilia kwao.

Rudi kwenye Sura

 72. Na kumbukeni siku mlipo muuwa mtu, mkakhasimiana wenyewe kwa wenyewe, mkautetea ukhalifu, mkawa mkituhumiana kwa mauwaji, na hali Mwenyezi Mungu anaijua hakika, na ataikashifu na kuidhihirisha juu ya kuificha kwenu.

Rudi kwenye Sura

 73. Tukakwambieni kwa ulimi wa Musa: Chukueni kipande cha nyama ya huyo ng'ombe mumpige nacho, nanyi mkafanya hivyo.  Mwenyezi Mungu akamfufua huyo aliye uliwa akataja jina la aliye muuwa, na kisha akafa tena. Na huo ulikuwa ni muujiza wa Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Musa (1).
Kwani Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu, na kwa uwezo wake huu ndivyo anavyo huisha maiti Siku ya Kiama. Na anakuonyesheni dalili za uwezo wake ili mpate kufahamu na kuzingatia haya.
(1) Mwandishi mmoja wa zama zetu, marehemu Sh. Abdul Wahhab Annajjar ametaja kwamba kauli ya Mwenyezi Mungu: "Mpigeni kwa kipande chake" maana yake kipande cha aliye uwawa. Na makusudio ya kufufuka kwake ni kumtolea kisasi, kwa kuwa kupigwa kwa kiungo cha mwenye kuuliwa humpelekea muuwaji kuungama, na mara nyingi kumwona tu aliye uwawa humpelekea mwenye kuuwa kuungama. Na inakuwa kisa hichi ni mbali na lile jambo la kuchinja, na kuamrisha Mwenyezi Mungu Mtukufu kuchinja; na kwamba kuamrisha Mwenyezi Mungu Mtukufu wamchinje ng'ombe ni kwa ajili ya kumla. Na katika haya pana mafunzo ya nafsi kwao, kwani hawa walikuwa pamoja na Wamisri ambao wakimwona ng'ombe ni mtakatifu, na yalikuwa kwao mabaki ya haya ya kumtukuza ng'ombe kwa dalili ya kuwa waliabudu sanamu la ndama baada ya hayo. Ikawa hapana budi kung'oa mabaki yake katika nafsi zao kwa kuwalazimisha kumchinja ng'ombe. Ndio ikawa ile amri ya kuchinja, na yakatokea majadiliano na kukawa kule kusitasita kwao, na mwisho wakamchinja, na walikaribia wasichinje.

Rudi kwenye Sura

 74. Tena nyinyi baada ya miujiza na ishara hizi zote hamkukubali wala hamkunyooka, wala nyoyo zenu hazikulainika na kunyenyekea. Bali zikawa zimekacha na ngumu, na zikabakia vile vile na ugumu wake na ushupavu wake, kama jiwe gumu katika ule ukakamavu wake, bali hizo nyoyo zenu zimeshinda jiwe kwa ugumu. Kwani yapo mawe yanayo athirika na kulainika. Yapo mawe yanayo timbuka maji yakawa mito, na yapo mawe yanayo pasuka na yakatoka maji kama chemchem, na yapo mawe kwa uwezo wa Mwenyezi yanayo nyenyekea kufuata mapenzi ya Mwenyezi Mungu yakaporomoka kutoka juu ya milima kama apendavyo Mwenyezi Mungu Mtukufu. Ama hizo nyoyo zenu,nyinyi Mayahudi, haziathiriki wala hazilainiki. Ole wenu kwa hayo! Mwenyezi Mungu si mwenye kughafilika na vitendo vyenu, naye atakupeni adabu kwa namna mbali mbali za adhabu, ikiwa hamtoshukuru kwa neema mlizo pewa.

Rudi kwenye Sura

 75. Haikufaliini enyi Waumini kutumai ya kuwa Mayahudi wataiamini Dini yenu na wakufuateni nyinyi, na ilhali katika makundi yao mbali mbali zimekusanyika sifa mbovu zinazo waweka mbali na kuiamini Haki. Walikuwapo baadhi miongoni mwao (nao ni wale Makohani) walio kuwa wakiyasikia maneno ya Mwenyezi Mungu katika Taurati, na wakiyafahamu vilivyo, kisha makusudi wakiyageuza na hali wanajua kuwa ni kweli, na kuwa vitabu vya Mwenyezi Mungu vilivyo teremshwa haijuzu kuvigeuza.

Rudi kwenye Sura

 76. Na kilikuwapo kikundi kingine miongoni mwa wanaafiki wao wakikutana na walio amini husema kwa kuwakhadaa: Tunaamini kuwa nyinyi mnafuata Haki, na kuwa Muhammad ni Nabii aliye tajwa sifa zake katika Taurati. Na wakiwa peke yao na wenzao hulaumiana kwa kughafilika kwa baadhi yao, kwa vile ndimi zao zilivyo teleza katika kuwakhadaa Waumini kuwapa maneno ambayo yatawapa faida makhasimu zao, na wala si lazima katika udanganyifu, wakawatajia yaliyomo katika Taurati ya kueleza kwa sifa kuja kwa Muhammad na kwa hivyo itakuwa hoja juu yao Siku ya Kiyama.

Rudi kwenye Sura

 77. Hivyo basi haiwapitikii watu hawa na wale kuwa Mwenyezi Mungu hana haja ya kupata hoja kama hizo? Kwani Yeye anajua wanacho kificha na wanacho kidhihirisha.

Rudi kwenye Sura

 78. Na miongoni mwa Mayahudi kipo kikundi cha wajinga wasio jua kusoma, wasio jua chochote kutokana na Taurati ila uwongo unao wafikiana na matamanio yao, wanao wapachikia pachikia makohani wao, na wakaona katika mawazo yao kuwa hayo ni kweli iliyotoka Kitabuni.

Rudi kwenye Sura

 79. Basi hao makohani wataangamia na watapata adhabu kwa vile wanavyo andika vitabu kwa mikono yao, kisha wakawaambia wajinga wasiojua kusoma kuwa: Hii ni Taurati iliyo toka kwa Mwenyezi Mungu. Kusudi lao ni kuwa wapate kwa hayo pato la upuuzi la kidunia, wanunue upuuzi huu kwa kuuza Haki na Kweli. Basi ole wao kwa wanayo mzulia Mwenyezi Mungu, na ole wao kwa yale matunda wanayo yachuma kwa uzushi wao!

Rudi kwenye Sura

 80. Na katika khitilafu zao ni haya wanayo yapata kwa makohani ya kuwa Moto hautawagusa Mayahudi hata wakifanya maasia namna gani ila kwa muda wa siku chache tu. Basi waambie ewe Muhammad!: Nyinyi mmeagana na Mwenyezi Mungu kwa hayo, hata mkawa mmetumaini kuwa Mwenyezi Mungu havunji ahadi yake, au mnamzulia uwongo tu?

Rudi kwenye Sura

 81. Ukweli wa mambo ni kuwa nyinyi mnamzulia Mwenyezi Mungu uwongo. Kwani hukumu ya Mwenyezi Mungu inapitishwa kwa viumbe vyake vyote sawa sawa, hapana farka baina ya Yuhudi na asiye kuwa Yahudi. Wenye kutenda maovu, na maovu yakawazunguka hao waovu mpaka njia za kuokoka zote zikazibwa, basi hao ndio watu wa Motoni na huko watudumu milele.

Rudi kwenye Sura

 82. Na wale walio amini na wakatenda mema hao ndio watu wa Peponi, kwa sababu wao wameamini na wakatimiza iliyo wajibisha Imani yao, nayo ni vitendo vyema, basi wao watakaa Peponi daima milele.

Rudi kwenye Sura

 83. Mbali na haya yote, nyinyi jamaa wa Kiyahudi, mnaendelea kuyashughulikia madhambi na kuvunja ahadi, na kupindukia mipaka aliyo kuwekeeni Mwenyezi Mungu.  Kumbukeni tulipo chukua ahadi kwenu katika Taurat kuwa hamtamuabudu ila Mwenyezi Mungu, na mwatendee wema wazazi na jamaa na mayatima na masikini, na mnapo zungumza na watu mtumie maneno mazuri ya kuleta masikilizano baina yenu nao wala sio ya kukutenganisheni, na mtimize yaliyo kuwa waajibu juu yenu, nayo ni Sala, na Zaka.  Na kumbukeni ulikuwaje mwendo wenu katika ahadi hiyo? Vipi mlivyo ivunja na mkajipuuza nao, isipo kuwa wachache tu ndio walio ifuata Haki?

Rudi kwenye Sura

 84. Na kumbukeni tulipo chukua ahadi kwenu katika Taurat kuwa hamtakuwa mkimwaga damu zenu, wala hamtafukuzana katika majumba yenu.  Na ahadi hiyo mnakubali kuwa ipo katika Kitabu chenu na mnashuhudia kuwa ni kweli.

Rudi kwenye Sura

 85. Nanyi wenyewe kwa wenyewe mnauwana, na mnatoana majumbani, nyinyi kwa nyinyi: hawa wanawauwa hawa na hawa wanawauwa hawa; hawa  wanawafukuza hawa majumbani mwao na hawa wanawafukuza hawa. Na  huku mkisaidiana katika vitendo vya dhambi na uadui. Baada ya hayo wakitokea baadhi yenu wakatekwa na hao mnao shirikiana nao mnajishughulisha kwenda kuwakomboa hao mateka.  Mkiulizwa nini  kilicho  kupelekeeni  kuwakomboa, mnajibu kuwa vitabu vyenu vinakuamrisheni kukomboa mateka wa Kiyahudi.  Jee, vitabu hivyo havikukuamrisheni msimwage damu ya ndugu zenu? Havikukuamrisheni msiwatoe watu majumbani mwao? Hivyo nyinyi mnat'ii sehemu ya yaliyo kujieni katika Kitabu na mnayakataa mengineyo?  Basi jaza ya mwenye kutenda hayo katika nyinyi si lolote ila kupata hizaya katika maisha ya duniani, na Siku ya Kiyama Mwenyezi Mungu, anaye vijua vyema vitendo vyao na siri zao, atawapeleka kwenye adhabu iliyo kali kabisa.
Kabla ya Uislamu zilikuwapo katika mji wa Madina kabila mbili za Kiarabu ambazo zilikuwa na uadui baina yao, nazo ni Aus na Khazraj. Na pia zilikuwako kabila za Kiyahudi nazo ni Banu Quraidha na Banu Nnadhir. Banu Quraidha walifungamana na Aus, na Banu Nnadhir walifungamana na Khazraj. Ilikuwa kabila mbili za Kiarabu zikipigana, zile kabila za Kiyahudi nazo huingia vitani, kila kabila upande wa rafiki zake, na zikiuwana na wenzao wa dini moja nao, na wakifukuzana makwao. Lakini kila moja katika kabila mbili hizo za Kiyahudi zikishughulika baadaye kuwakomboa mateka walio tekwa na rafiki zao wa Kiarabu. Wakiulizwa kwa nini mnawakomboa na hao walikuwa wakipigana nanyi upande wa maadui zenu? Wao wakisema: Mwenyezi Mungu ametuamrisha katika Taurati tuwakomboe mateka wa Kiyahudi. Na wanajifanya hawajui kama Mwenyezi Mungu amewaamrisha vile vile wasiuwane wala wasitoane majumbani mwao. Kwa hivyo ndio wanaamini sehemu ya Kitabu na wanaikataa nyengine.

Rudi kwenye Sura

 86. Na hayo ni kwa kuwa wamekhiari mapato ya hii dunia ipitayo kuliko neema za Akhera zitakazo dumu. Katika haya wamekuwa kama mtu aliye uza Akhera yake kwa ajili ya kununua dunia. Basi hawatapunguziwa adhabu ya Jahannam, wala hawatapata wa kuwaokoa nayo.

Rudi kwenye Sura

 87. Enyi Mayahudi, kumbukeni vile vile, ule msimamo wenu wa upotovu na wenye dhambi kwa mnasaba wa Musa na Mitume mingine tulio watuma. Kwani tulimtuma kwenu Musa na tukampa Taurati, na kumfwatia yeye tuliwaleta Mitume kadhaa wa kadhaa wengineo. Miongoni mwao ni: Isa bin Maryamu ambaye tulimpa miujiza na tukamuunga mkono kwa Roho Mtakatifu, naye ni Jibril Mjumbe muaminifu wa Ufunuo.  Nanyi kila akikujilieni Mtume asiye wafikiana na matamanio yenu mnatakabari na hamtaki kumfwata. Mitume wengine mliwakataa na kuwaambia waongo, na wengine mliwauwa khasa.

Rudi kwenye Sura

 88. Hali kadhaalika msimamo wenu kwa Mtume wetu Muhammad, Nabii wa mwisho.  Mlimwambia  alipo kuiteni msilimu: Nyoyo zetu zimefunikwa kwa vifuniko visivyo  achilia kupenya huo wito wako. Basi sisi hatuelewi kitu chochote unacho sema! Wala nyoyo zao hazikufunikwa kama wanavyo dai, lakini wamepanda kiburi tu, na wakakhiari upotovu kuliko uwongofu. Basi Mwenyezi Mungu amewalaani kwa ukafiri wao, na amedhoofisha yakini yao na imani yao.

Rudi kwenye Sura

 89. Na Mtume wetu alipo wajia na Qur'ani, nayo ni Kitabu kilicho toka kwa Mwenyezi Mungu kinacho thibitisha Taurati walio teremshiwa wao, na wakajua kutokana na hiyo Taurati ukweli uliomo katika Kitabu hichi (Qur'ani) walikataa kwa inadi na uhasidi tu, kwa sababu yamekuja hayo kutokana na Mtume asiye kuwa wa taifa lao la Wana wa Israili, juu ya kuwa kabla yake walipo kuwa wakipambana na makafiri washirikina ikiwa mpambano wa vita au majadiliano, wakitaja kuwa Mwenyezi Mungu atakuja wanusuru wao kwa kumtuma Nabii wa mwisho aliye bashiriwa katika Kitabu chao, na ambaye sifa zake zimewafikiana kabisa moja kwa moja na sifa za Muhammad.(1) Jueni basi laana ya Mwenyezi Mungu iko juu ya watu wa namna hii wenye inda na ukanushi.
(1)   (Mwenyezi Mungu alimwambia Musa: "Mimi nitawaondokeshea nabii miongoni mwa ndugu zao mfano wako wewe...mtu asiye sikiliza maneno yangu atakayosema yule kwa jina langu, nitalitaka kwake."
--Kumbukumbu la Torati 18.18-22.
Maana ya haya ni: Taurati inasema kwamba Nabii Musa aliambiwa na Mungu kwamba atawaletea Nabii kutokana na ndugu za Wana wa Israili, yaani Waarabu. Na asiye mfuata Nabii huyo Mwenyezi Mungu atamuadhibu.)

Rudi kwenye Sura

 90. Kiovu mno walicho ziuzia nafsi zao na roho zao! Na hayo ni kwa udhalimu wao, na kuona maya na kufanya uadui tu. Matamanio yao na chuki zao za kikabila, na ugozi walio nao, ndio ulio wapelekea kukataa tulio yateremsha Sisi, kwa kuonea uchungu vipi Mwenyezi Mungu kumpa ujumbe wake Mtume asiye tokana na wao.  Wanamkatalia Mwenyezi Mungu kuwa ni  mwenye kukhiari atakavyo nani wa kumteremshia fadhila yake miongoni mwa waja wake. Kwa hivyo wamejipalilia wenyewe ghadhabu juu ya ghadhabu kwa kufuru zao na inadi zao na uhasidi wao.  Na makafiri kama hawa watapata adhabu ya kuwadhalilisha na kutia uchungu.

Rudi kwenye Sura

 91. Hizi ndizo dhamiri walizo nazo ndani ya nafsi zao. Lakini mbele za watu wakijitetea kuwa wao hawaiamini Qur'ani wanapo takiwa waamini, kwa kuwa wao hawaamini ila yale walio teremshiwa wao tu, na wanayakataa mengineyo.  Na hakika wanasema uwongo kwa hayo madai yao kuwa wanaamini yaliyomo katika Taurati, kwani kwa kukitaa Kitabu hichi cha Qur'ani kinacho thibitisha Kitabu chao, ndio kuwa maana yake wanakataa Kitabu chao chenyewe, na kwa kuwa wao waliwauwa Manabii walio kuwa wanawaitia yale walio teremshiwa.  Na wao kuwauwa hao ni dalili ya kukata kuwa hawauamini Ujumbe wao.

Rudi kwenye Sura

 92. Bali hakika nyinyi Mayahudi mlikanusha kwa uwazi Vitabu vyenu, na mkarejea katika ushirikina katika zama za Musa mwenyewe. Kwani Musa alikujieni na hoja zilizo wazi, na miujiza inayo hakikisha ukweli wake, lakini kiasi ya kukupeni mgongo tu alipo kwenda kusema na Mola wake Mlezi nyinyi mkaingia kuabudu ndama, na mkarajea katika ukafiri wenu wa kuabudu masanamu, na nyinyi mkawa mlio dhulumu mlio potea.

Rudi kwenye Sura

 93. Na alipo kuleteeni Taurati mkaziona amri ngumu ziliomo ndani yake, mkaona mizito mizigo yake na mkaitilia shaka, Mwenyezi Mungu alikuonyesheni Ishara ya ukweli wa Kitabu hicho na faida ya mafunzo yake kwenu.  Akaunyanyua Mlima wa T'uur juu ya vichwa vyenu hata ukawa kama kiwingu, na mkadhani kuwa utakuangukieni. Hapo mkaonyesha kukubali na kut'ii. Tukachukua ahadi yenu kuwa hamtaghurika na pumbao katika kufuata yaliyomo katika Kitabu hichi. Mkasema: Tumeamini na tumesikia.  Lakini vitendo vyenu vimefichua  uasi wenu, na kwamba imani haijaingia katika nyoyo zenu. Wala hayumkini kuwa imani imeingia katika nyoyo za watu walio shughulishwa na mapenzi ya kumuabudu ndama. Imani yenu hiyo mnayo dai basi imekusozeni kwenye maovu.

Rudi kwenye Sura

 94. Na nyinyi mmedai kuwa Mwenyezi Mungu atakupeni nyinyi tu neema za Pepo baada ya kufa, wasipate watu wote wengineo. Ikiwa basi kweli mnaamini hayo myasemayo basi yafaa myapende mauti. Hebu yatamanini myapate upesi zisije kutaakhari hizo starehe mnazodai.

Rudi kwenye Sura

 95. Lakini kwa hakika mambo yalivyo, wao hawayatamani mauti kabisa kwa dhulma walio ifanya, ambayo haifichikani kwa Mwenyezi Mungu.  Yeye anawajua kuwa wao ni waongo kwa hayo wanao dai. Neema za Siku ya Kiyama zitakuwa ni za wachamngu, si za wafanyao maovu kama wao.

Rudi kwenye Sura

 96. Bila ya shaka yoyote utawakuta wao ndio wamewashinda watu wote kwa pupa waliyo nayo kuwania maisha ya dunia ya kila namna, ya utukufu na unyonge.  Na hiyo pupa yao inashinda ya makafiri washirikina (mapagani) wasio amini kufufuliwa wala Pepo. Kwa hivyo wanapenda lau kuwa wangelizidishiwa umri wakaishi hata miaka elfu. Na hata wangeliishi vipi hawawezi kuepuka adhabu ya Mwenyezi Mungu inayo wangojea. Kwani Yeye ni Mjuzi wa hao madhaalimu, na atawaonjesha malipo ya vitendo vyao wanavyo vitenda

Rudi kwenye Sura

 97. Na baadhi yao wanadai kuwa wanakupinga na wanakikataa Kitabu chako kwa kuwa ati wao ni maadui wa Jibril anaye kufikishia hichi Kitabu. Basi sema ewe Nabii uwaambie: Anaye kuwa Jibril ni adui wake, basi vile vile huyo ni adui wa Mwenyezi Mungu, kwa sababu Jibril haji na Kitabu hichi kwa nafsi yake, bali anakiteremsha kwa amri ya Mwenyezi Mungu. Na Kitabu hichi kinathibitisha Vitabu vilivyo tangulia kutoka mbinguni.. na kinathibitisha Kitabu chenu wenyewe..na hii Qur'ani (inayo teremshwa na Jibril kutoka kwa Mwenyezi Mungu) ni Uwongofu na Bishara njema kwa Waumini.

Rudi kwenye Sura

 98. Basi yeyote anaye kuwa ni adui wa Jibril, au Mikail, au Malaika yeyote au Mtume yeyote, miongoni mwa Malaika na Mitume wa Mwenyezi Mungu, ambao hawafanyi kitu wala hawapeleki ujumbe ila kama vile Mwenyezi Mungu anavyo waamrisha, basi mtu huyo anakuwa ni adui wa Mwenyezi Mungu, na anakuwa kafiri anamkataa Mwenyezi Mungu.   Na Mwenyezi Mungu ni adui wa makafiri.

Rudi kwenye Sura

 99. Na Jibril hateremshi kwenye moyo wako ila  Ishara na hoja zilizo wazi, ambazo haiwezekani kwa mwenye kutafuta haki kikweli ila aziamini tu. Na hapana mwenye kuzikataa Ishara kama hizo ila wale wafanyao inda na inadi, ambao wametokana na mwenendo wa maumbile walio umbwa nao.

Rudi kwenye Sura

 100.  Na kama (hawa Wana wa Israili) walivyo kuwa vigeugeu katika itikadi na imani, hali kadhaalika walikuwa vigeugeu katika ahadi na mapatano wanayo choka nayo. Walikuwa kila wanapo fungamana na Waislamu au wengineo kwa maagano hutokea kikundi miongoni mwao wakavunjilia mbali maagano hayo. Kwani wengi wao hawaamini utukufu wa ahadi na utakatifu wa maagano.

Rudi kwenye Sura

 101. Na alipo wajia Mtume aliye toka kwa Mwenyezi Mungu aliye wafikiana sawa sawa na sifa zilizo tajwa katika Vitabu vyao, naye ni Muhammad, rehema na amani iwe juu yake, kikundi kimojapo kutokana nao kilikataa hayo yaliyo tajwa katika Vitabu vyao kumkhusu Mtume huyu, kama kwamba halikutajwa jambo hilo humo wala wao hawajui lolote katika hayo.

Rudi kwenye Sura

 102. Na wao hakika waliyasadiki waliyo yazua mashetani wao na wapotovu wao juu ya ufalme wa Suleiman, walipo dai kuwa Suleiman hakuwa Nabii wala si Mtume aliye teremshiwa ufunuo (Wahyi) kutoka kwa Mwenyezi Mungu, bali alikuwa ni mchawi tu anaye tegemea msaada wa uchawi wake. Na kwamba ni uchawi wake huu ndio ulio mjengea ufalme wake na ukamwezesha aweze kuwatawala majini, na ndege, na upepo. Kwa hivyo walimsingizia ukafiri Suleiman, na hali Suleiman hakukufuru, lakini hao mashetani waovu ndio walio kufuru. Wao ndio walio zua uzushi huu, wakaingia kuwafunza watu uchawi wao na walio pokea katika mabaki yaliyo teremka katika  Baabil (Babilonia) kwa Malaika wawili, Haaruta na Maaruta. Na hawa Malaika wawili hawakuwa wakimfundisha mtu yeyote mpaka wamwambie: Sisi ni mtihani uwe ni majaribio kwenu, tunakufundisha mafunzo ambayo yanaweza kuleta fitna na ukafiri, basi jifunze lakini tahadhari usiitumie ilimu hii. Na lakini watu hawakunasihika kwa nasiha hii, na wakatumia hayo waliyo jifunza kwa hao Malaika wawili ya kumgombanisha mtu na mkewe.  Naam, hawa mashetani waovu wamekufuru walipo zua katika uzushi wao na hadithi zao za uwongo wakafanya hayo ndio wasila na udhuru wa kuwafundishia Mayahudi uchawi. Na wao hao wachawi hawawezi kumdhuru yeyote, lakini Mwenyezi Mungu ndiye Yeye anayeweza kumletea mtu madhara pindi akipenda. Na hayo ya uchawi wao yanawadhuru hao wanao jifunza katika dini yao na dunia yao, na wala hawapati faida yoyote. Na wao wanajua kweli ya kujua ya kwamba anaye elekea upande huu hana sehemu yoyote katika neema za Akhera.  Na kama wamebakia na ujuzi wowote yafaa wajue kuwa haya waliyo yakhiari kwa ajili ya nafsi zao ni hadi ya kuwa maovu.

Rudi kwenye Sura

 103.   Na  lau  kuwa  wao wameiamini Haki na wakauogopa ufalme na uwezo wa Mola wao Mlezi, basi Mwenyezi Mungu angeli walipa malipo mema, na hayo bila ya shaka yoyote yangeli kuwa ni bora zaidi kuliko  wanayo yapata katika hadithi zao za uwongo na dhamiri zao mbovu wanazo zidhamiria, lau kuwa wanabagua linalo kuwa na manufaa wakaacha lenye madhara.

Rudi kwenye Sura

 104. Enyi mlio amini!  Tahadharini na hawa Mayahudi. Msimwambie Mtume pale anapo kusomeeni ufunuo: "Raa'ina" kwa kukusudia akuwekeni  pahala pa uangalizi wake, yaani (Tuchunge, Turai), na akupeni muda katika kusoma kwake mpaka mzingatie na mhifadhi. Kwani watu makhabithi  miongoni  mwa Mayahudi husaidiana kutaka kukuigeni na kupindua  ndimi  zao  kwa  neno  hilo mpaka likawa neno la matusi wanalo lijua wao.(1)   Na  wao  humkabili  Mtume kwa neno hilo kwa kumfanyia maskhara. Lakini nyinyi tumieni neno jingine wasilo weza Mayahudi kulipatia njia ya kufanya ukhabithi wao na maskhara yao. Tumieni neno: "Ndhurna" yaani "Tuangalie". Na sikilizeni vyema anayo kusomeeni Mtume. Na Mwenyezi Mungu anawadundulizia adhabu kali kwa Siku ya Kiyama hawa wanao mfanyia maskhara Mtume.
(1) Katika lugha ya Kiyahudi ya Kiebrania lipo neno "Rai'nu" ambalo limejengwa na neno "Ra'" kwa maana ya "Shari" na neno "nu" linaonesha jamii, wingi. Na maana ya neno lote ni kuwa "Wewe ni shari yetu", wakikusudia kumwambia Mtume hayo.

Rudi kwenye Sura

 105. Na yafaa mjue kuwa hawa makafiri wa Kiyahudi na washirikina waabuduo masanamu hawakutakieni ila mdhurike tu, wala hawapendelei iteremke kheri yoyote kwenu kutoka kwa Mola wenu Mlezi. Na Mwenyezi Mungu hathamini chochote wanacho kipenda wala wanacho kichukia.  Kwani Mwenyezi Mungu humteua amtakaye kwa kumkhusisha kumpa rehema yake, na Mwenyezi Mungu ni mwenye fadhila kubwa.

Rudi kwenye Sura

 106. Nao walikutaka wewe Muhammad, uwaletee miujiza, ishara, ile waliokuja nayo Musa na Manabii wa Wana wa Israili. Sisi yatutosha kuwa tumekutia nguvu kwa kukuletea Qur'ani. Na Sisi tunapo acha nguvu kumpa Nabii anaye kuja nyuma kwa muujiza wa Nabii aliye tangulia, au tukawasahaulisha watu athari za muujiza ule, basi Sisi humletea huyu Nabii aliyekuja baadaye muujiza, kuwa ni Ishara, au Aya, iliyo bora zaidi au mfano wa ile ili kuwa ni dalili ya ukweli wake. Na Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu. (Na hapana Ishara, Muujiza au Aya, iliyo kubwa na bora na yenye kudumu kuliko hii Qur'ani.)

Rudi kwenye Sura

 107. Na Yeye, Mwenyezi Mungu, ndiye mwenye ufalme wa mbingu na ardhi katika mikono yake. Na nyinyi watu hamna mlinzi wa kukusaidieni, wala tegemeo la kukunusuruni isipokuwa Yeye.

Rudi kwenye Sura

 108. Na kwa kule kumtaka kwenu Mtume wenu Muhammad miujiza fulani pengine  ilikuwa mnawaiga Wana wa Israili wa zama za Musa, walipo mtaka awaletee miujiza maalumu. Kutaka kwenu huku kunaficha nyuma  yake inda na kumili kwenye ukafiri, kama kulivyo kuwa kule kutaka  kwa  Wana wa Israili kumtaka Mtume wao. Na mwenye kufuata nyayo za inda na ukafiri akaacha usafi  wa  kutaka  Haki na Imani basi huyo ameipotea Njia iliyo sawa iliyo nyooka.

Rudi kwenye Sura

 109. Na wengi miongoni mwa Mayahudi wametamani kukurejesheni, enyi Waislamu, kwenye ukafiri baada ya kuwa nyinyi mmekwisha amini. Na haya juu ya kuwa wao imekwisha wadhihirikia kutoka na hicho hicho Kitabu chao kuwa nyinyi mpo juu ya Haki.  Na hayakuwa hayo ila ni kuwa wanakuhusuduni na wanaogopa utawala usiwatoke mikononi mwao mkapewa nyinyi. Basi nyinyi wapuuzeni, na wasameheni, na waachilieni mbali mpaka Mwenyezi Mungu akuonyesheni lipi jengine la kuwafanyia,  kwani Yeye ni Muweza wa kukupeni ushindi juu yao, na Yeye ni Muweza wa kila kitu.

Rudi kwenye Sura

 110. Na hifadhini mambo ya Dini yenu: Shikeni Sala, toeni Zaka, na vitendo vyote vyema mnavyo fanya kujitangulizia nafsi zenu, na sadaka mnazo toa, malipo yake mtayakuta kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu anayajua vyema myatendayo; ujuzi wake ni ujuzi wa mwenye kutazama akaona.

Rudi kwenye Sura

 111. Na katika upotovu wa Mayahudi na Wakristo na matamanio yao ya uwongo, ni yale madai ya kila mmoja wao kuwa hataingia Peponi ila mwenye kufuata dini yao. Hebu watakeni wa kutoleeni ushahidi wa hayo madai yao kama kweli wanasema kweli.

Rudi kwenye Sura

 112. Na wala hawatapata ushahidi wa hilo. Kwani kweli ilivyo ni kuwa Mwenyezi Mungu Mtukufu amewaandalia neema za Pepo, na atawalipa malipo Siku ya Kiyama, na atawalinda na khofu na huzuni, hao ambao wanao msafia niya Mwenyezi Mungu na wanafuata Haki, na vitendo wavitendavyo ni vyema.

Rudi kwenye Sura

 113. Na ajabu iliyopo ni kuwa kama wanavyo fanyia uadui Uislamu, wanafanyiana uadui wenyewe, wao kwa wao. Mayahudi husema: Wakristo hawana lolote la haki. Na Wakristo nao wanasema mfano wa hayo, na huku wote wawili wanatoa ushahidi wao kutoka hivyo hivyo vitabu vyao vya Biblia wanavyoviamini wao wote.  Na wale washirikina wa Kiarabu wasio jua chochote katika vitabu vilivyo teremshwa kwa Mayahudi na Wakristo husema maneno kama hayo. Na kwa hakika wote hao pamoja wamesema kweli, kwani hapana kikundi kimojapo katika wao kilicho kuwamo katika Haki. Na hayo yatabainika pale Mwenyezi Mungu atapo wahukumu Siku ya Kiyama katika zile khitilafu zao wanazo khitilafiana.

Rudi kwenye Sura

 114. Katika yanayo dhihirisha uadui wa wao kwa wao na uadui wao wote kwa Waislamu, ni kule baadhi ya mataifa yao yalivyo kuwa yakiharibu mwahala mwa ibada ya mataifa mengineo, na vile wale washirikina walivyo kuwa wakiwazuia Waislamu wasiingie Msikiti Mtakatifu wa Makka. Na hapana kabisa mwenye kudhulumu zaidi kuliko azuiaye asitajwe Mwenyezi Mungu katika pahala pa ibada, na akafanya juhudi kutaka kupaharibu. Watu hao watapata hizaya duniani, na Akhera watapata adhabu kubwa. Haiwafalii wao kufanya ukhalifu kama huu muovu, bali iwapasavyo ni kulinda utakatifu wa pahala  pa ibada, wala wasiingie humo ila kwa unyenyekevu na kukhofu, wala wasizuilie kutajwa jina la Mwenyezi Mungu ndani yake. (Na ufisadi kama huu, bali ni mkubwa zaidi,  ni wa wale wanao ghusubu mali za wakfu ya misikiti.)

Rudi kwenye Sura

 115. Ikiwa washirikina waliwazuia Waislamu kusali katika Msikiti Mtakatifu wa Makka, hawatoweza kuwazuia kusali na kumuabudu Mwenyezi Mungu. Kwani jiha zote na pande zote za dunia ni za Mwenyezi Mungu. Na hakika bila ya shaka  Mwenyezi Mungu anampokelea Muislamu Sala zake, na anamkabili kwa radhi yake pande zote anapo fanya ibada yake. Kwani Mwenyezi Mungu ni mwenye wasaa, hawadhikishi waja wake, na Yeye ni Mwenye kuijua vyema niya ya mwenye kumuelekea.

Rudi kwenye Sura

 116. Basi huyo ambaye mambo yake ni kama hivi, na vyote viliomo ulimwenguni vinat'ii amri yake, vinanyenyekea kwa atakalo, basi Yeye huyo yuko juu mno, na mtukufu mno hata hahitajii kuwa na dhuriya au kujipa wana, kama wanavyo zua hawa Mayahudi na Wakristo na washirikina mapagani.

Rudi kwenye Sura

 117. Vipi awe na haja ya uzazi au atafute mwana huyo aliye anzisha kuumba mbingu na ardhi bila ya kuwa na kiigizo chochote kabla yake, na akavifanya vyote viliomo humo vimt'ii Yeye kwa kila atakalo, na visiweze kumuasi? Yeye akitaka kitu basi husema tu: Kuwa! Kikawa.

Rudi kwenye Sura

 118. Washirikina wa Kiarabu walikakamia katika inadi yao kumfanyia  Muhammad,  wakamtaka  kama  wale kaumu zilizo tangulia zilivyo wataka Manabii wao. Wakasema kuwa hawatomuamini ila Mwenyezi Mungu aseme nao, na awaletee ishara, au muujiza wa kuuona utakao onesha ukweli wake. Haya ni kama walivyo sema Wana wa Israili kumwambia Musa: Hatukuamini mpaka tumwone Mwenyezi Mungu na aseme nasi.  Na kama masahaba (wanafunzi) wa Isa walipo mtaka awateremshie chakula kutoka mbinguni.  Na haya yote ni kuwa nyoyo za makafiri na wapinzani wenye inda katika kila umma zimefanana. Haki haidhihiriki ila kwa wale ambao kuona kwao kumesafika, na akili zao zimeelekea kufuata Yakini, na kuitaka Haki.

Rudi kwenye Sura

 119. Na Sisi tumekutuma ufikishe Haki iliyo yakini ili uwape bishara njema Waumini, na uwaonye makafiri. Na waajibu wako ni kufikilisha tu ujumbe wetu, wala wewe hutosailiwa kwa kukosa Imani hao wasio kuamini, ambao wataingia Motoni.

Rudi kwenye Sura

 120. Basi usijikere nafsi yako kwa kutaka kuwaridhi hao wapinzani wa Kiyahudi na Wakristo. Kwani hao hawatakuwa radhi nawe mpaka ufuate mila yao hao ambao wanadai ati ndio wenye uwongofu.  Na kabisa hapana uwongofu ila uwongofu wa Mwenyezi Mungu ulioko katika Uislamu. Na mwenye kufuata matamanio ya watu hawa baada ya kuijua Haki tuliyo kuteremshia wewe, basi Siku ya Kiyama hatapata mlinzi wa kumsaidia mbele ya Mwenyezi Mungu, wala hatapata wa kumnusuru na adhabu.

Rudi kwenye Sura

 121. Tena kipo kikundi katika Mayahudi na Wakristo walio wataalamu katika vitabu vyao vya asli, na wakavisoma vilivyo, na wakafahamu mageuzo yaliomo ndani yake, hao wanauamini ukweli wa mambo, na kwa hivyo wanaiamini hii Qur'ani. Na wenye kukikataa Kitabu kilicho teremka kutoka kwa Mwenyezi Mungu hao ndio wenye kukhasiri.

Rudi kwenye Sura

 122. Enyi Wana wa Israili! Aminini na mkumbuke neema kubwa niliyo kupeni kwa nilivyo kutoeni kwenye dhulma ya Firauni na nilivyo mzamisha baharini, na nilivyo kupeni Manna na Salwa, na nikakuleteeni Manabii kutokana miongoni mwenu, na nikakufunzeni Kitabu, na mengi mengineyo ya utukufu niliyo kupeni.  Pia nikakunyanyueni kwa wakati fulani kuliko watu wote kwa vile nilivyo wateuwa Manabii kadhaa kutokana nanyi.

Rudi kwenye Sura

 123. Na iogopeni adhabu ya Mwenyezi Mungu katika siku ambayo hapana mtu ataye weza kumtetea mwenziwe kwa lolote, wala fidia haitakubaliwa, wala maombezi hayatafaa kitu, wala makafiri hawatapata mtu wa kuwanusuru na Mwenyezi Mungu.

Rudi kwenye Sura

 124. Na kumbukeni pale Mwenyezi Mungu alipo mjaribu babu yenu Ibrahim kwa kumtwisha amri fulani. Naye Ibrahim alizitimiza hizo amri vilivyo. Mwenyezi Mungu akamwambia:  Mimi nataka kukufanya wewe uwe Imamu, yaani Mwongozi, wa watu, nao wawe wakikufuata wakishika nyayo zako.  Ibrahim akamtaka Mola awajaalie katika vizazi vyake wawe pia Maimamu kama yeye. Mwenyezi Mungu akamjibu kuwa haya hawatayapata wanao dhulumu, na hivyo kaashiria kuwa mnamo dhuriya za Ibrahim watatokea walio wema na walio wabaya.

Rudi kwenye Sura

 125. Na kadhaalika kumbukeni hadithi ya Ibrahim na mwanawe Ismail walipo ijenga ile Nyumba Takatifu ya Makka, Alkaaba. Katika kisa hichi pana funzo linalo fika mbali kwa mwenye moyo wa kuzingatia. Basi kumbukeni tulipo ifanya Nyumba hii ni pahala wanapo kwenda viumbe kutoka kila pahala duniani na kukusanyika. Na tukaifanya kuwa ni pahala pa usalama na amani kwa kila mwenye kutaka hifadhi. Na pia tulivyo amrisha kuwa pahala alipo kuwa akisimama Ibrahim kuijenga hiyo Nyumba pafanywe ni msala, yaani pahala pa kusalia. Na tukaagana na Ibrahim na Ismail waihifadhi Nyumba hiyo isipate kitu ambacho hakistahiki na utakatifu wake, na waitayarishe kwa matayarisho yanayo silihi kwa wanao kusanyika huko, wale wanao kwenda kut'ufu, na wanao kaa kwa ibada ya ii'tikafu, na wanao sali.

Rudi kwenye Sura

 126. Na kumbukeni Ibrahim alipo mwomba Mola wake Mlezi ajaalie mji utakao kuwapo hapo kwenye nyumba ya Alkaaba uwe mji wa amani, na awaruzuku matunda ya ardhi na kheri zake watu wake watao muamini Mwenyezi Mungu na Siku ya mwisho.  Mwenyezi Mungu alimjibu kuwa hatamnyima riziki hata kafiri muda wa uhai wake mfupi, kisha Siku ya Kiyama atakwenda ingia katika adhabu ya Jahannam, na mwisho wa watu hao ni muovu mno.

Rudi kwenye Sura

 127. Na alipo kuwa Ibrahim na mwanawe Ismail wananyanyua misingi ya Alkaaba na huku wakimwomba Mwenyezi Mungu:  Mola Mlezi  wetu, Ewe Muumba wetu, na Muanzishi wetu! Tupokelee hii kazi yetu tuifanyayo kwa usafi wa niya kwa ajili yako, kwani Wewe ni Mwenye kusikia maombi yetu, ni Mwenye kujua ukweli wa niya yetu.

Rudi kwenye Sura

 128. Mola Mlezi wetu!  Tuwezeshe na utujaalie tuwe wenye kukusafia niya Wewe, na miongoni mwa vizazi vyetu wajaalie watoke watu wenye kukusafia Wewe. Na tufundishe njia za ibada yetu kukuabudu Wewe katika Nyumba hii takatifu na pembezoni mwake, na pokea toba yetu tunapo sahau au tunapo kosea. Hakika Wewe ni mwingi wa kupokea toba za waja wako, na Msamehevu kwao kwa fadhila yako na rehema yako.

Rudi kwenye Sura

 129. Mola Mlezi wetu! Waletee kutokana na vizazi vyetu Mtume miongoni mwao atakaye wasomea Aya zako na atawafundisha yale utakayo mfunulia yeye katika Kitabu na ilimu zenye manufaa na sharia zenye hikima, na awatakase kutokana na tabia mbovu. Hakika Wewe ndiye Mwenye kushinda, Mwenye nguvu, Mwenye hikima katika uyatendayo na unayo yaamrisha na unayo yakataza.
Mwenyezi Mungu hakupeleka Mtume kutokana na vizazi vya Ismail ila Muhammad s.a.w. Kwake yeye ndiyo dua hii imepokelewa na Mwenyezi Mungu kwa kutumwa kwa vizazi vya Ismaili na wanaadamu wote.

Rudi kwenye Sura

 130. Aliyo yafanya Ibrahim na aliyo yaomba kwa Mwenyezi Mungu ni mambo mazuri mno. Hali kadhaalika mila aliyo ifuata ni mila iliyo kwenda sawa kabisa. Na hapana anaye jitenga na mila ya Ibrahim ila mwenye kuudharau utu wake mwenyewe na akili yake. Hakika Mwenyezi Mungu alimteuwa yeye Ibrahim katika dunia, na pia Akhera ni miongoni mwa watu wema walio karibishwa.

Rudi kwenye Sura

 131. Yeye Ibrahim aliitikia amri ya Mola wake Mlezi pale alipo mtaka asilimu, yaani anyenyekee. Akasema: Namnyenyekea Mola Mlezi wa walimwengu wote, majini, watu na Malaika.

Rudi kwenye Sura

 132. Na Ibrahim hakutosheka na hayo tu, bali aliwausia wanawe wende mwendo wa uwongofu kama wake. Na mjukuu wake Yaakubu akamuiga, naye akawausia wanawe kadhaalika wafuate mwenendo huo huo. Aliwabainishia wanawe ya kwamba Mwenyezi Mungu amewateulia  Dini ya Tawhidi, ya Mungu Mmoja. Na akachukua kwao ahadi kuwa hawatakufa ila nao ni Waislamu, wenye kuthibiti juu ya Dini hii.

Rudi kwenye Sura

 133. Na nyinyi Mayahudi mlidai kuwa nyinyi mnakwenda mwendo wa Dini aliyo kufa nayo Yaakubu.  Kwani nyinyi mlikuwapo pale mauti yalipo mjia Yaakubu hata mkajua kuwa alikufa katika mila gani? Basi zindukaneni mjue ya kuwa Yaakubu na wanawe walikuwa Waislamu wenye kumuamini Mungu Mmoja, wala wao hawakuwa Mayahudi kama nyinyi, wala hawakuwa Wakristo. ("Uyahudi" umeanza kuitwa hivyo baada ya Yuda, mwana wa Yaakubu. "Ukristo" ni baada ya Isa Masihi, Yesu Kristo. Ama "Uislamu", yaani unyenyekevu kwa Mwenyezi Mungu, ni Dini ya maumbile, ipo milele.)  Na mjue ya kuwa Yaakubu alipo kabiliwa na mauti aliwakusanya wanawe na akawaambia: Mtaabudu nini baada yangu? Na wao wakajibu: Tutamuabudu Mungu wako na Mungu wa baba zako Ibrahim na Ismail na Is-hak, Mungu Mmoja; na kwake Yeye tunanyenyekea.

Rudi kwenye Sura

 134. Tena imekuwaje enyi Mayahudi kujadili mambo ya watu hawa?  Hao ni watu walio kwisha pita na njia yao. Tena wao peke yao watavuna yale  waliyo yatenda katika maisha yao. Nyinyi, basi, hamtaulizwa kitu juu ya vitendo vyao, na wala nyinyi hamtapata faida yoyote katika hayo. Nanyi hamtavuna ila yale matunda ya vitendo vyenu mnavyo vitenda nyinyi wenyewe.

Rudi kwenye Sura

 135. Lakini wao hawaachi kuendelea katika ghasia na inda zao. Kila kikundi katika hao hudai kuwa ni dini yao wao tu ndiyo iliyo sawa.  Mayahudi hukuambieni:  Kuweni Mayahudi mpate kuhidika na kuongokewa kwenye njia sawa. Na Wakristo nao wanasema:  Kuweni Wakristo ndio mpate kuongoka kwenye haki iliyo nyooka. Nyinyi wajibuni kuwa sisi hatufuati hii wala hii kwa sababu dini zote hizo mbili zimekwisha potoka na zimeacha ile asli yake ya kweli, na zimeingia ndani yake ushirikina (upagani), na ziko mbali kabisa na mila ya Ibrahim.  Bali sisi tunaufuata Uislamu ndio ulio ifanya mila ya Ibrahim kuwa safi iliyo safika.

Rudi kwenye Sura

 136. Waambieni: Sisi tunamuamini Mwenyezi Mungu, na tunaamini Qur'ani iliyo teremshwa kwetu, na kadhaalika tunaamini waliyo teremshiwa Ibrahim, na Ismail, na Is-hak, na Yaakub na watoto na wajukuu zao, na tunaiamini Taurati ile Mwenyezi Mungu aliyo mteremshia Musa ambayo iliyo kuwa haijakorogwa, na Injili aliyo teremshiwa Isa na Mwenyezi Mungu, ambayo haikukorogwa, na walio pewa Manabii wote kutokana na Mola wao Mlezi.  Sisi hatutafautishi hata mmoja kati yao, tukawa tunawakanusha baadhi na kuwaamini wengineo. Na katika haya sisi tunakuwa ndio  Waislamu wenye kunyenyekea amri ya Mwenyezi Mungu.

Rudi kwenye Sura

 137. Wao wakiamini imani inayo wafikiana na imani yenu basi kweli wameongoka.  Lakini wakikakamia katika inadi yao na kukataa kwao basi hao wamo katika ushindani usio koma, na hawana masikizano nanyi. Mwenyezi Mungu atakutosheni kukulindeni na shari yao, ewe Nabii. Na atakupumzisha na ghasia zao za inadi na upinzani wao. Kwani Yeye ni Mwenye kuyasikia wayasemayo, na Mwenye kuyajua hata yaliomo vifuani mwao.

Rudi kwenye Sura

 138. Waambieni: Hakika Mwenyezi Mungu ametuongoa sisi kwa uwongofu wake mwenyewe, na ametuonyesha hoja zake. Na hapana mbora zaidi kwa uwongofu na hoja kuliko Mwenyezi Mungu.  Na sisi hatumnyenyekei ila Mwenyezi Mungu. Na wala hatufuati ila anavyo tuongoa na kutuongoza Yeye. (Hilo ndilo pambo, au batizo, au kutia rangi kwa Mwenyezi Mungu--S'ibghatu Llahi).

Rudi kwenye Sura

 139. Waambieni: Mnajadiliana nasi katika mambo ya Mwenyezi Mungu mkidai kuwa Yeye hakuteuwa Manabii ila kutokana nanyi tu? Na Mwenyezi Mungu ni Mola Mlezi wenu na Mola Mlezi wa kila kitu; hawapendelei kaumu fulani akawatupa wengine. Rehema yake humfikia amtakaye, na huwalipa watu wote kwa vitendo vyao, bila ya kuangalia nasaba yao na ukoo wao. Na Yeye ametuongoa kwenye Njia Iliyo Nyooka katika vitendo vyetu. Na ameturuzuku tumsafie niya na vitendo Yeye.

Rudi kwenye Sura

 140. Waambieni:  Mnajadiliana nasi katika mas-ala ya Ibrahim, na Ismail, na Is-hak, na Yaakub na watoto na wajukuu zao, mkidai kuwa wao walikuwa Mayahudi au Wakristo kama nyinyi, na ilhali Sisi hatukuiteremsha Taurati na Injili wanazo zitegemea Mayahudi na Wakristo ila baada ya hawa.   Na Sisi tulikwisha waelezeni khabari ya hayo.  Jee, nyinyi mnajua zaidi au Mwenyezi Mungu?  Bali hakika Mwenyezi Mungu amekwisha waambieni nyinyi hayo katika vitabu vyenu. Basi msiifiche kweli iliyo andikwa katika hivi vitabu vyenu.  Na nani dhaalimu mkubwa zaidi kuliko yule anaye ificha kweli inayo toka katika kitabu chake ambayo naye anaijua. Na Mwenyezi Mungu atakulipeni kwa upotovu mnao ushikilia, kwani Mwenyezi Mungu haghafiliki na mnayo yatenda.

Rudi kwenye Sura

 141.  Tena imekuwaje nyinyi Mayahudi na Wakristo kuyajadili mambo ya watu hawa? Kwani watu hawa wamekwisha pita na njia zao. Wao watapata malipo ya a'mali yao waliyo itenda katika uhai wao, wala nyinyi hamtaulizwa juu ya a'mali zao, wala hamtafaidika kwa lolote katika hayo. Nanyi hamtapata malipo ila kwa vitendo mnavyo vifanya nyinyi wenyewe.

Rudi kwenye Sura

 142. Hakika wale wachache wa akili walio potezwa na pumbao lao wasiweza kufikiri sawa na kuzingatia miongoni mwa Mayahudi, na Wakristo, na washirikina na wanaafiki, watachukizwa kuwaona Waumini wameacha kukielekea kibla cha Beitul Muqaddas (Yerusalemu) walicho kuwa wakikielekea kwanza katika Sala. Na wao wakiona kuwa hicho kinastahiki zaidi kuliko kibla kingine, yaani cha Alkaaba.  Basi waambie, Ewe Nabii! Jiha zote ni za Mwenyezi Mungu. Hapana upande ulio bora kuliko mwengine kwa dhati yake, lakini Mwenyezi Mungu ndiye mwenyewe anachagua  upande autakao uwe ni kibla cha Sala. Na Yeye kwa mapenzi yake huuongoa kila umma katika wanaadamu kufuata njia iliyo sawa anayo ikhiari Yeye na anayo ikhusisha Yeye. Na sasa umekuja Ujumbe wa Muhammad unafuta risala zote zilizo tangulia, na Kibla cha sasa cha Haki ni hichi cha Alkaaba iliyopo Makka.

Rudi kwenye Sura

 143. Na kwa ajili ya kutaka huku ndio tukakuongoeni kwenye Njia Iliyo Nyooka kabisa, na tukakujaalieni muwe Umma wa katikati ulio bora kwa muujibu tulivyo iwafikisha Dini sahihi na vitendo vyema, ili muwe wenye kuthibitisha Haki kwa mnasaba wa sharia zilizo tangulia, na ili Mtume awe mlinzi juu yenu, akikupeni nguvu kwa uwongozi wake kwa muda wa uhai wake, na kwa kufuata njia yake na mwendo wake baada ya kufa kwake.  Ama kibla cha Beitul Muqaddas tulicho amrisha kifuatwe kwa muda fulani tulikifanya kuwa ni mtihani kwa Waislamu ili watambulikane wanao t'ii wakielekee kwa ut'iifu, na wenye kuchukuliwa na mori wao wa Kiarabu kwa kufuata nyao za Ibrahim tu waivunje amri ya Mwenyezi Mungu na kwa hivyo wapotelee njia ya upotovu.  Na ilikuwa ile amri ya kuelekea Beitul Muqaddas ni katika mambo magumu ila kwa wale ambao wamejaaliwa kupata hidaya ya Mwenyezi Mungu. Ikawa kufuata amri hii miongoni mwa nguzo za Imani. Mwenye kuelekea kibla cha Beitul Muqaddas katika zama ilipo amrishwa hayo hakupoteza Imani yake na ibada yake kwa upole na rehema ya Mwenyezi Mungu.

Rudi kwenye Sura

 144. Na Sisi tulikuona vipi unazichungua mbingu asaa uteremke Wahyi (ufunuo) wa kugeuza Kibla cha Beitul Muqaddas ufuate cha Alkaaba ambacho unakipenda, kwa kuwa ndicho Kibla cha Ibrahim, baba wa Manabii, na baba wa Mayahudi na Waarabu. Na hapo pana Maqaamu Ibrahim, alipokuwa akisimama Ibrahim. Kwa hivyo hichi ni Kibla kilicho kusanya wote, ijapokuwa kinaacha kibla cha Mayahudi. Basi hivi sasa Sisi tunakupa lile ombi lako. Kwa hivyo katika Sala zako elekea Masjidil Haraam (Msikiti Mtakatifu). Na nyinyi Waumini, kadhaalika, elekeeni huko popote pale mlipo. Watu wa Kitabu wanao udhika kwa kukiacha kwenu Kibla cha Beitul Muqaddas wanajua katika vitabu vyao kuwa nyinyi ni watu wa Alkaaba. Na wanajua kuwa amri ya Mwenyezi Mungu inawakhusisha watu wa kila sharia na kibla chao. Na hii ni haki inayo tokana na Mola wao Mlezi. Lakini wao wanataka kukufitinisheni na kukutilieni shaka katika Dini yenu. Na Mwenyezi Mungu si mwenye kughafilika nao, na Yeye atawalipa kwa wayatendayo.

Rudi kwenye Sura

 145. Na hakukua kutoridhika kwao Watu wa Kitabu nanyi ni kwa kudanganyikiwa ambako kwaweza kuondoka kwa hoja, bali kuudhika huko ni kwa inadi na kiburi. Kwa hivyo Ewe Mtume! Hata ukiwaletea kila hoja ya kukata kuwa Kibla chako ndicho cha kweli, hawakubali kukifuata Kibla chako. Ikiwa Mayahudi wangali wanatumai kuwa bado utarejea kwenye kibla chao, na wanatoa hiyo ni shuruti ya kusilimu kwao, basi watavunjika moyo, wala wewe hutofuata kibla chao. Na hao watu wa Kitabu kila kikundi chao kina kibla chake mbali. Wakristo hawafuati kibla cha Mayahudi, wala Mayahudi hawafuati kibla cha Wakristo,  na kila mmoja kati yao anawaona wengine hawamo katika haki. (1).  Basi wewe thibiti hapo hapo kwenye Kibla chako, wala usiyaendekeze matamanio yao. Kwani mwenye kuyafuata matamanio yao baada ya kwisha pata ujuzi kuwa wao ni wapotovu, na kujua kuwa yeye yuko katika haki, basi huyo ni katika walio dhulumu na wenye kubobea katika dhulma.
(1) Wanasema wafasiri kuwa Mayahudi wanaelekea kwenye Mwamba katika Beitul Muqaddas na Wakristo wanaelekea Mashariki.

Rudi kwenye Sura

 146. Na hakika Watu wa Kitabu wanajua kuwa huku kugeuza Kibla ni jambo la haki, na wanakutambua kuwa wewe ndiye Nabii aliye sifiwa katika vitabu vyao, na miongoni mwa sifa hizo kuwa atasali kuelekea Alkaaba. Na kujua kwao Unabii wako na kukijua Kibla chako ni sawa sawa wanavyo wajua watoto wao kwa uwazi kabisa. Lakini baadhi yao wanaificha kweli hii juu ya kuwa wanajua, kwa kufuata pumbao na chuki zao za upotovu kuwania mila zao kwa ajili ya kulinda madaraka yao, na wanatafuta hila za kukupotoeni nyie.

Rudi kwenye Sura

 147.   Na hakika Haki ni anayo kutolea Mwenyezi Mungu Mtukufu sio wanayo kupotoshelea watu wa Kitabu.  Basi kuweni na yakini nayo, msiwe watu wenye kutia shaka shaka na kubabaika.  Na katika hiyo Haki ni hii amri ya Kibla, basi endeleeni nayo wala msiwabali wapinzani.

Rudi kwenye Sura

 148. Hakika Kibla hicho tulicho kuelekeza ndicho Kibla chako na Kibla cha Umma wako.  Na hali kadhaalika kila umma una kibla chake unako elekea katika sala yao kwa mujibu wa sharia zilizo kwisha pita. Wala katika haya hapana kupikuana kwa ubora, na ama kupikuana kwa ubora ni kwa kutenda vitendo vya ut'iifu na a'mali za kheri.  Basi kimbilieni kwenye kheri na mshindane kwa hayo.  Mwenyezi Mungu atakuhisabuni kwa hayo, kwani Yeye atakukusanyeni nyote Siku ya Kiyama kutoka kokote mtapo kuwako. Wala hatamchopoka hata mmoja. Kila kitu kimo mkononi mwake, na katika hivyo ni amana, kuhuisha, kufufua na kukusanya.

Rudi kwenye Sura

 149. Basi katika Sala zako popote pale ulipo uelekee Msikiti Mtakatifu, ukiwa upo mjini au umo safarini, popote wendapo. Na hakika haya bila ya shaka ndiyo ya Haki yanayo wafikiana na hikima ya Mola wako Mlezi aliye pamoja nawe. Basi wewe na umma wako yatamanini haya. Kwani Mwenyezi Mungu atakulipeni malipo mema kabisa. Na Mwenyezi Mungu ni mwenye ujuzi wala hapana katika vitendo vyenu vilivyo fichikana naye.

Rudi kwenye Sura

 150. Jilazimishe kuifuata amri ya Mwenyezi Mungu katika mambo ya kuelekea Kibla, na kuwa na pupa nayo wewe na umma wako. Na uelekeze uso wako uelekee upande wa Msikiti Mtakatifu popote wendapo katika safari zako. Na elekeeni huko popote mtapo kuwapo pande zote za dunia, mkiwa mko safarini au mpo mjini, ili ukatike ule ushindani wa hoja za hao walio khalifu na wanao jadiliana nanyi ikiwa hamkufuata amri hii ya kugeuza Kibla. Mayahudi watasema: Vipi Muhammad anapo sali anaelekea Beitul Muqaddas, na Nabii alielezwa katika vitabu vyetu ni kuwa moja katika sifa zake anaelekea Alkaaba?  Na washirikina wa Kiarabu watasema: Vipi anadai kuwa mila yake ni mila ya Ibrahim, naye hafuati Kibla chake? Juu ya vyote hakika hao walio dhulumu walio potoka wakaiacha Haki kutoka pande zote mbili hawatoacha majadiliano yao na upotovu wao, bali watasema: Hakugeuka kuelekea Alkaaba ila kuwa anafuata ile ile dini ya kishirikina ya kaumu yake, na kuupenda ule mji wake. Basi nyinyi msiwabali hao, kwani uchochezi wao hauto kudhuruni. Nanyi niogopeni Mimi, msiikhalifu amri yangu. Kwa amri hii tumetaka kuitimiza neema juu yenu, na Kibla hichi tulicho kuelekezeni ndicho kipelekee kuthibiti kwenu katika uwongofu na kupata tawfiki.

Rudi kwenye Sura

 151. Na hivi kukuelekezeni kwenye Msikiti Mtakatifu na kwa kuwa tumekutumieni Mtume aliye tokana nanyi, akikusomeeni Aya ni katika  kukutimizieni  neema yetu, kama tulivyo kutimizieni ile neema - nayo ni Qur'ani - na akusafishieni nafsi zenu zitoke uchafu wa ushirikina na tabia na ada mbovu mbovu, na anakusemezeni kwa njia ya kukufunzeni maarifa ya Qur'ani na ilimu zenye nafuu, na kukufunzeni mambo ambayo mlikuwa hamyajui. Kwani mlikuwa katika ujinga na upotovu ulio mpofu wa kijahilia.

Rudi kwenye Sura

 152. Basi enyi Waumini! Nikumbukeni kwa kunit'ii, na Mimi nitakukumbukeni kwa kukupeni thawabu. Na nishukuruni kwa neema nilizo kuvikeni, wala msizipinge neema hizi kwa kuyaasi yale niliyo kuamrisheni.

Rudi kwenye Sura

 153. Na tafuteni kujisaidia, enyi Waumini, katika kila linalo kupateni, kwa kusubiri na kushika Sala.  Sala ndio msingi wa ibada zote. Hakika Mwenyezi Mungu kwa uwezo wake wenye nguvu yu pamoja na wanao subiri. Yeye ndiye mlinzi wao, na Yeye ndiye anaye wanusuru daima.

Rudi kwenye Sura

 154. Na subira haipelekei ila kwenye kheri na kufanikiwa kote kuwili, duniani na Akhera. Basi msikae nyuma mkaacha kwenda kupigana Jihadi kwa ajili ya Mwenyezi Mungu.  Wala msiogope kufa katika Jihadi, kwani mwenye kufa katika Jihadi huyo si maiti, hakufa, bali yuhai maisha ya juu kabisa, ijapo kuwa hawa tunao waona wahai hawatambui hayo.

Rudi kwenye Sura

 155. Subira ni ngao na silaha ya Muumini ambayo kwayo hushindia kila shida na mashaka. Na nyinyi zitakuja kupateni shida nyingi. Tutakujaribuni na kukufanyieni mitihani kwa vitisho vya maadui, kwa njaa, na uchache wa vifaa, na kupungukiwa mali, na watu kufa, na kupotea mazao.  Na hapana la kukulindeni katika mtihani huu mkali ila Subira.  Basi Ewe Nabii! Wape bishara nzuri wanao subiri kwa moyo na ulimi.

Rudi kwenye Sura

 156. Wale ambao kwamba yanapo wateremkia machungu ya kuwaumiza wanaamini ya kuwa hakika kheri yote na shari inatokana na mwenyewe Mwenyezi Mungu, na ya kwamba amri yote ni ya Mwenyezi Mungu. Hao husema: Sisi ni milki ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, na sisi ni wenye kurejea kwake Yeye. Sisi hatuna letu jambo lolote. Na Yeye ni mwenye kustahiki kushukuriwa kwa anacho toa, na juu yetu kusubiri wakati wa kujaribiwa, na kwake Yeye ndiyo zipo thawabu na malipo.

Rudi kwenye Sura

 157. Basi hao wenye kusubiri, wenye kumuamini Mwenyezi Mungu, wanapewa bishara njema kuwa watapata maghfira na ihsani ya Mwenyezi Mungu, na wao ndio wenye kuongoka njia ya kheri na uwongozi mwema.

Rudi kwenye Sura

 158. Na kama alivyo kuwa Mwenyezi Mungu ametukuza hadhi ya Alkaaba akaifanya iwe ndiyo Kibla cha Sala, hali kadhaalika ametukuza shani ya vilima viwili viliopo Makka, navyo ni Safaa na Marwa, akavifanya miongoni mwa mahala pa kufanyia ibada ya Hijja.  Basi imewajibikia baada ya kuizunguka Alkaaba kwa kut'ufu, kwenda huku na huku baina ya vilima viwili hivyo mara saba. Kwenda huko kunaitwa  Sa'yu.   Na  baadhi yenu labda walikuwa wakiona vibaya kufanya  hivyo  kwa  kuwa  kilikuwa  kitendo cha siku za jahiliya kabla ya kuja Uislamu. Lakini kweli iliopo ni  kuwa hiyo  ni  ada ya Kiislamu ya tangu zamani. Basi hapana ubaya wowote kufanya Sa'yu baina ya vilima viwili hivi kwa mwenye kunuwiya Hijja na Umra. Na Muumini na afanye jambo la kheri kama awezavyo, kwani hakika Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa ayatendayo, na Yeye atamlipa kwa a'mali yake.

Rudi kwenye Sura

 159. Hao wanao kukatalieni Dini yenu wako makundi mawili: kundi moja ni katika Watu wa Kitabu wanao ijua Kweli, lakini wanaificha kwa kujua na kwa inda. Na kundi jengine ni la washirikina ambao nyoyo zao ni pofu, kwa hivyo hawaioni Kweli, na badala ya Mwenyezi Mungu Mmoja wakawa wanaabudu miungu myengineo. Basi Watu wa Kitabu walio jua ushahidi wa ukweli wako wanajua haki ya Dini yako, lakini kisha wanazificha hizo dalili ili watu wasijue. Mwenyezi Mungu atawapatiliza ghadhabu yake, na atawaepusha rehema yake, na kila wanao omba katika Malaika, na Wanaadamu na Majini watawaapiza wasipate rehema ya Mwenyezi Mungu.

Rudi kwenye Sura

 160. Wala hapana atakaye vuka na laana hiyo katika wao ila aliye tubu na akatenda mema kwa kuacha kuficha Haki, akayadhihirisha aliyo kuwa akiyaficha katika sifa za Mtume na Uislamu. Mwenyezi Mungu atakubali toba yake na atamfutia dhambi zake, kwani Yeye ndiye anaye kubali toba ya waja wake kwa huruma na rehema yake.

Rudi kwenye Sura

 161. Ama wale walio kakamia na ukafiri, na wakafa bila ya toba wala majuto, jaza yao ni laana ya Mwenyezi Mungu, na Malaika na watu wote.

Rudi kwenye Sura

 162. Na wataendelea katika laana hii na katika Moto, wala hawatapunguziwa adhabu, wala hawatapewa muhula wala haitoakhirishwa. Hata wakiomba muhula na kuakhirishwa hawataitikiwa.

Rudi kwenye Sura

 163. Hakika Mungu wenu anaye stahiki kuabudiwa pekee ni Mmoja. Hakuna mungu mwenginewe, wala hapana utawala ila wake. Tena Yeye amesifika kuwa ni Mwenye rehema, basi Yeye ni Rahim, Mwenye Kuwarehemu waja wake katika kuwaumba na kuwafanya walivyo.

Rudi kwenye Sura

 164. Na zipo dalili nyingi na Ishara kwa kila mwenye akili juu ya kuwapo kwake na Ungu wake.  Miongoni mwa hizo ni hizi mbingu mzionazo zinazo pitiwa na sayari kwa nidhamu bila ya kuzahamiana wala kugongana, zikiuletea ulimwengu huu joto na nuru. Na pia hii dunia yenye bara na bahari, na kupishana usiku na mchana, pamoja na manufaa yake. Katika Ishara na dalili hizo ni kuzingatia marikebu zipitazo baharini zikibeba watu na vifao vyao, na hapana aziendeshao hizo ila Mwenyezi Mungu. Ni Yeye ndiye anaye zituma pepo zinazo leta mvua. Na mvua ikateremka ikahuisha wanyama na ikanywesha ardhi na mimea. Na hizo pepo kwa mivumo yake ya kila namna, na mawingu yaliyo tundikwa baina ya mbingu na ardhi: Jee, yote haya yamesimama kwa uangalifu namna hii na kwa hukumu kama hizi wenyewe tu? Au vimeundwa na Mwenye Kujua Mwenye Uwezo?

Rudi kwenye Sura

 165. Na juu ya dalili zilio wazi baadhi ya watu walio potelewa na akili wamewafanya miungu mingine isiyo kuwa Mwenyezi Mungu, wakiwat'ii na kuwaabudu kama Mwenyezi Mungu na wakawafanya mfano wa Mwenyezi Mungu. Muumini humuelekea Mwenyezi Mungu tu, na kumt'ii kwake hakuna ukomo. Ama hao ut'iifu wao kwa miungu yao hulegalega wakati wa shida. Hapo basi humkimbilia Allah Subhanahu. Na walio jidhulumu nafsi zao lau wangezingatia adhabu itakayo wapata Siku ya Malipo, utakapo dhihiri Ufalme wa Mwenyezi Mungu, na ut'iifu ukawa wake tu wangeli achilia mbali ukhalifu wao na wangeli sita kutenda dhambi zao.

Rudi kwenye Sura

 166. Siku hiyo wafuasi watatamani wakubwa wao wawaokoe na upotofu, nao watawakataa na kujitenga nao wakisema: Hatukukwiteni mtut'ii katika kumuasi Mola wenu Mlezi. Hilo ni pumbao lenu tu na uovu wa vitendo vyenu. Makhusiano baina yao na mapenzi waliyo kuwa nayo duniani yatakatika siku hiyo, na watakuwa maadui wao kwa wao.

Rudi kwenye Sura

 167. Na hapa wafuasi itawabainikia kuwa walipotea walipo wafuata viongozi wao katika upotovu,  na watatamani warejee duniani wawakatae viongozi wao kama wao walivyo wakataa siku ya leo. Vitendo vyao viovu vitadhihiri wajute, lakini wapi! Vimekwisha watumbukiza Motoni, na wala hawatatoka humo.

Rudi kwenye Sura

 168. Enyi watu!  Kuleni vyakula alivyo kuumbieni Mwenyezi Mungu katika ardhi vilivyo halali, visivyo harimishwa, vilivyo vizuri, vinavyo pendwa na nafsi. Wala msimfuate Shetani anaye kupendezeni kula chakula cha haramu, au kuharimisha kilicho halali. Nyinyi mmeujua uadui wa Shetani kwenu, na umebainika ubaya wa anayo kuamrisheni.

Rudi kwenye Sura

 169. Shetani anakupambieni kiovu kwa dhati na chenye madhara kwa afya yenu, na kibaya ili mkitende. Kwa sababu yake mnafuata dhana na mawazo yasio na msingi.  Mkamsingizia Mwenyezi Mungu kuhalalisha na kuharimisha bila ya dalili ya ilimu na yakini.

Rudi kwenye Sura

 170. Wapotovu walio acha njia ya uwongofu wamezoea kuyashika waliyo yarithi kwa baba zao katika itikadi na vitendo. Wanapo itwa wafuate uwongofu wa Mwenyezi Mungu husema: Hatuachi tuliyo yakuta kwa baba zetu. Katika ujinga mkubwa kabisa ni kukhiari kufuata wazee kuliko kumt'ii Mwenyezi Mungu na kufuata uwongofu wake. Kefu basi inapo kuwa baba zao hawanacho wakijuacho katika Dini, na hawana mwangaza wa kuwanawirisha uwongofu na Imani?

Rudi kwenye Sura

 171. Na mfano wa kuwaita hao makafiri wanao pinga haki na uwongofu na wasiitikie wala wasifahamu wanaitiwa nini ni mfano wa mchunga kondoo anapo wasemeza hayawani. Hawafahamu kitu wala hawasikii ila sauti, wala hawaelewi kinginecho. Basi hao kadhaalika kwa mintarafu ya Haki ni viziwi wa kusikia, vipofu wa kuona, mabubu wa kusema. Hawatamki jema, wala hawatoi la akili.

Rudi kwenye Sura

 172. Na Sisi tumewaruhusu watu kula kila kilicho halali (1) tulicho waumbia katika ardhi. Na tumewakataza wasifuate nyayo za Shetani. Wakifanya hivyo watakuwa wameongokewa, lakini wakikataa basi Sisi tunawakhusisha Waumini tu kwa uwongofu wetu, na tunawabainishia wao kilicho halali na haramu. Basi enyi Waumini! Mmeruhusiwa kula kila chakula kitamu kilicho chema, sio kichafu. Basi mshukuruni Mwenyezi Mungu aliye kuwekeeni wazi neema ya kumakinika kwa vitu vizuri na kukuhalalishieni, na kwa neema ya ut'iifu na kufuata amri yake ili ibada zenu zitimie.
(1) Qurani imeutangulia utibabu wa kisasa kwa kukataza kula mzoga, kwani kifacho kwa ukongwe au ugonjwa husabibishwa na sumu inayo mdhuru mlaji. Kadhaalika cha kunyongwa au maradhi huinajisi damu, na ndani yake huwamo vingi vya kudhuru kama jasho na mkojo. Na nguruwe husabibisha maradhi ya khatari kama TRICHINOSIS ambayo khatimaye huharibu moyo na mapafu na husabibisha mauti.

Rudi kwenye Sura

 173. Sio yaliyo harimishwa wanayo zua Washirikina na Mayahudi. Lakini mlicho harimishiwa nyinyi Waumini ni nyamafu, mzoga, yaani mnyama asiye chinjwa, na mfano wake katika kuharimishwa ni nyama ya nguruwe, na nyama ambaye wakati wa kuchinjwa ametajiwa jina lisilo kuwa la Mwenyezi Mungu, kama vile miungu ya uwongo au mfano wake. Juu ya hivyo mtu akilazimika kwa dharura (1) kula kidogo katika vilivyo katazwa kwa ajili ya njaa, na hakupata kinginecho, au kwa kulazimishwa, basi hana makosa juu yake. Lakini ajitenge na mwendo wa kijaahili, kutaka kula vilivyo katazwa kwa kutamani tu, na wala asipite kiasi kula kuliko cha kuondoa njaa tu.
(1) Hali ya dharura inaruhusisha kinacho harimishwa, kwa sababu mauti ya yakini yanashinda madhara yanayo weza kustahamilika, na kwamba mwenye kulazimika kwa dharura haimfalii kupindukia mpaka wa dharura, wala asikiuke kile alicho lazimika kukila.

Rudi kwenye Sura

 174. Miongoni mwa watu wanao jua aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu kipo kikundi kinacho ficha baadhi ya maandishi ya ufunuo kwa ajili ya sababu fulani za kilimwengu.  Mayahudi, mathalan, wakificha mengi yaliyo kuja katika Taurati ya kueleza sifa za Mtume kwa kukhofu wasije wakasilimu watu wa mila yao na kwa hivyo utukufu wao ukaondoka na wakapoteza mapato yao na vyakula vyao vitamu. Na hakika chakula chao wakilacho kwa njia hii ni kama kula moto, kwani hayo yatawapelekea kuingia Motoni. Mwenyezi Mungu atawatupilia mbali Siku ya Kiyama, wala hatawasafisha  uchafu wao, na mbele yao kuna adhabu ya kuumiza kweli.

Rudi kwenye Sura

 175. Hao ndio wenye madhambi walio khiari upotovu wakaacha uwongofu, na kwa hivyo wakastahiki adhabu ya Akhera badala ya kupata msamaha. Watakuwa kama mwenye kununua baat'ili kwa haki, na chenye upotovu kwa chenye uwongofu. Hakika hali yao ni ya kustaajabisha, kwa kuwa wanavumilia kufanya mambo ambayo hayana budi kuwapelekea kwenye adhabu, na tena wakawa wenyewe wakayaonea uzuri hayo yanayo wapeleka huko!

Rudi kwenye Sura

 176. Nao yamewapasa malipo waliyo kadiriwa kwa kukikataa Kitabu cha Mwenyezi Mungu alicho kiteremsha kwa haki na kweli. Na wamekhitalifiana kwacho khitilafu kubwa iliyo wapelekea kupenda kujadiliana na kujitenga na Haki, na kufuata pumbao, wakakigeuza na kukifisidi na kukifasiri kinyume na maana yake ya hakika.

Rudi kwenye Sura

 177. Watu wamekithirisha maneno juu ya Kibla kama kwamba wema wote ni hayo tu.  Hivi sivyo. Kuelekea upande fulani, mashariki au magharibi, sio msingi wa Dini na kupata kheri, lakini kupata wema ni mambo kadhaa wa kadhaa, baadhi yake ni nguzo za itikadi sahihi, na baadhi yake ni katika misingi ya tabia njema na ibada. La kwanza: kumuamini Mwenyezi Mungu, na Siku ya kufufuliwa na kukusanywa na kuhisabiwa na yatakayo tokea Siku ya Kiyama; na kuamini Malaika, na Vitabu vilivyo teremka kwa Manabii, na kuwaamini wenyewe Manabii. Na pili: kutoa mali kwa kupenda na kuridhia nafsi kuwapa mafakiri katika jamaa, na mayatima, na wenye shida ya haja, na wasafiri walio katikiwa safari yao wasipate cha kuwafikishia wendako, na walio lazimika kuomba kwa haja walio nayo, na kugomboa watumwa. ( Walio fungwa na kutawaliwa na dhaalimu ni watumwa pia. )Tatu: kushika Sala. Lane: kutoa Zaka iliyo lazimishwa. La tano: kutimiza ahadi bilhali wal maal. La sita: kustahamili maudhi yanayo teremkia roho na mali, mnapo pambana na adui zama za vita. Basi wenye kukusanya imani hizi na vitendo hivi vya kheri ndio walio sadikisha Imani yao, na wao ndio wanao jilinda na ukafiri na mambo machafu na wakayaepuka.

Rudi kwenye Sura

 178.  Katika  Sharia  tulizo  walazimisha  Waumini  ni hukumu za mauwaji ya makusudi.  Tumewaandikia  kisasi  kwa mauwaji. Na  wala  msichukulie dhulma za kijahiliya (1), walipo kuwa wakimuuwa muungwana asiye uwa kwa ajili ya mtumwa, na wakimuuwa mwanamume asiye uwa kwa ajili ya mwanamke, na mkuu asiye uwa badala ya mwenginewe aliye uwa, akaachiliwa aliye uwa khasa.(Kwa kila ukoo kujiona bora). Yatakikana yule aliye uwa auwawe yeye, akiwa ni muungwana, au mtumwa, au mwanamke. Msingi wa sharia ya kisasi ni kuondoa kufanyiana uadui kwa kumuuwa yule yule aliye uwa ili kuuzima moto wa kulipizana na kuondoa uadui. Walio uliwa mtu wao wakiacha kisasi, wakapendelea kuwasamehe wenzao, watakuwa na haki ya kupewa fidia kwa maiti wao. Na wao inatakikana wawe wasemehevu bila ya kumkahirisha aliye uwa. Na juu ya mwenye kuuwa alipe fidia bila ya kujikurupusha. Katika hukumu ya mauwaji kama tulivyo ilazimisha pana wepesi kwa Waumini ukilinganisha na hukumu ya Taurati inayo lazimisha kisasi tu, na kama ilivyo kuwa ni rehema ukilinganisha na watakavyo wenginewe kuwa muuwaji aachiliwe bure bila ya kumtaaradhi. Basi mwenye kuivuka hukumu hii baada ya hayo atapata adhabu chungu duniani na Akhera.
(1)Waarabu zama za jahiliya walikuwa hawafanyi usawa baina ya watukufu na wanyonge. Akiuliwa mwongozi hawatosheki na kumuuwa muuwaji bali huyo huachwa akenda kulipizwa kisasi kwa mwongozi wa kabila ya muuwaji. Kwao roho si sawa, na damu si sawa. Uislamu haukukubali haya, lakini ukapasisha Kisasi, roho kwa roho, mwenye kuuwa huuwawa. Muuwaji yeyote awaye atauliwa akiwa muungwana, mtumwa au mwanamke. Haya ni kwa ajili ya usawa katika damu; hapana mwenye damu tukufu na damu isiyo tukufu. Na inafahamika kwa ishara kuwa nafsi kwa nafsi. Na hii ni sharia ya milele, ilikuwako katika Taurat, na Injil na Qur'ani. Na Mwenyezi Mungu Mtukufu amesema: "Na tuliwaandikia kuwa nafsi kwa nafsi..." (taz. Almaida ). Na Mtume s.a.w. amesema: "Damu za Waislamu ni sawa." Na amesema: "Nafsi kwa nafsi". Zingatia: Uislamu kwa sharia ya kisasi ina nadhari nyengine, sio kama kanuni za kutungwa. Imewapa wenye kuuliwa mtu wao haki ya kutaka muuwaji auwawe, kuondoa fitna na umwagaji wa damu mkubwa. Imewapa haki ya kusamehe au kulipwa kisasi, wala haizuilii serikali kumfedhehi aliye uwa ikiona hivyo ni maslaha. Uislamu hauzingatii sababu ya kuuwa, kwani mwenye kuuwa amedhulumu hata ikiwa sababu gani. Na huenda ukitafuta sababu akaonewa huruma mkosa, na kumpuuza mkoswa. Na hayo hupelekea mchafuko wa watu kuchukua kisasi mkononi mwao, na kuzalikana makosa juu ya makosa ya kuuwa, kwa kutoridhika wale walio uliwa mtu wao. Nadharia hii ya Kiislamu sasa inadurusiwa katika vyuo vikuu vya Ulaya.

Rudi kwenye Sura

 179. Hakika rehema ya Mwenyezi Mungu kwenu ni kubwa kwa hii hukumu ya kisasi. Kwa fadhila ya kisasi jamii yenu ina hakika kupata maisha ya amani na salama. Haya ni kwa kuwa mwenye kutaka kuuwa  akijua  kuwa naye atauwawa atajizuia kutenda alilo kusudia. Kwa hivyo yeye na yule ambaye angeli uwawa wanahifadhika. Lakini ikiwa kama ilivyo kuwa zama za ujahili akiuliwa mkuu kwa kuuliwa mtu mdogo, na asiye na kosa badala ya mwenye makosa - hapo inakuwa ni kuzua fitna, na kuondoka utulivu na amani. Wenye akili nawazingatie faida ya sharia ya kisasi. Hayo yatawapelekea watambue upole wa Mwenyezi Mungu kwao kuendea  njia ya uchamngu, na kuzifuata amri za Mwenyezi Mungu Subhanahu.

Rudi kwenye Sura

 180. Kama tulivyo weka sharia ya kisasi kwa maslaha ya umma na kuhifadhi jamii, vile vile tumeleta sharia ya maslaha ya ukoo na kuulinda, nayo ni Sharia ya Wasiya. Basi mwenye kuona kuwa amekabiliwa na mauti naye akawa na mali basi yatatikana awawekee katika mali yake fungu la wazazi wake na jamaa zake, wale jamaa ambao hawamrithi. Katika hayo afuate mwendo unao pendeza na unakubaliwa na wenye akili. Asiwe akampa tajiri na akamwacha fakiri, bali amfadhilishe yule mwenye haja zaidi, wala asiweke sawa ila wale wenye pato sawa. Na faridha hiyo ni haki iliyo mwajibikia mwenye kupenda uchamngu na kufuata amri za Dini.

Rudi kwenye Sura

 181.  Ukitoka  wasiya  basi huo  ni haki iliyo  waajibu,  haijuzu kuugeuza na kuubadilisha ila ikiwa wasiya huo umeacha  uadilifu. Mwenye kubadilisha haki akageuza wasiya muadilifu ulio sawa baada ya  kujua hukumu hii basi huyo amepanda madhambi yatakayo  mletea adhabu. Mwenye kuusia hana kosa kwa yatakayo tokea baada yake, wala hakudhani kuwa atakuwapo atakaye fanya hayo, wala yeye hapatilizwi kwa hayo. Mwenyezi Mungu, hakika, ni Mwenye kusikia na kujua, wala hapana linalo fichikana kwake.

Rudi kwenye Sura

 182. Ama ikiwa wasiya umeacha haki na njia iliyo sawa tuliyo kwisha ibainisha, kwa mwenye kufanya wasiya kumharimisha   fakiri akampa tajiri, akawawacha jamaa zake akawapa mafakiri wasio rithi watu mbali, basi mwenye kwenda mwendo wa kheri akamrejeza mwenye kufanya wasiya ende sawa, basi hapana dhambi kwa kuugeuza wasiya kwa namna hiyo. Na Mwenyezi Mungu hamchukulii kitu kwa hayo, kwani Mwenyezi Mungu ni Msamehevu, Mwenye kurehemu.

Rudi kwenye Sura

 183.    Na kama tulivyo kuwekeeni sharia za Kisasi na Wasiya kwa ajili ya maslaha ya jamii zenu, na kuhifadhi mambo ya ukoo, kadhaalika  tumeweka  sharia za Saumu ili kuzitengeneza nafsi zenu, ziweze kujikinga na matamanio, na kukutukuzeni kuliko wanyama walio baki wanao fuata hisiya za matamanio yao tu. Na huku kufaridhishwa Saumu ni kama walivyo faridhishwa kaumu zilizo tangulia.  Basi  msilione kuwa ni jambo zito mno hili, kwani watu wote walilazimishwa  haya.  Kulazimishwa Saumu ni kwa ajili ipate kuleleka roho ya  uchamngu,  na ili muwe watu madhubuti, na nafsi zenu ziongoke sawa.

Rudi kwenye Sura

 184. Mmeamrishwa  mfunge siku chache za kuhisabika, na lau Mwenyezi Mungu angependa angeli kufanyieni muda mrefu. Wala hatukulazimishini katika Saumu jambo msilo liweza. Aliye mgonjwa wa maradhi yanayo dhuriana na kufunga, au aliomo safarini, basi anaweza kula na alipe akisha pona au akirejea safarini. Ama asiyekuwa mgonjwa wala si msafiri, lakini hawezi kufunga ila kwa taabu kwa sababu ya udhuru kama ukongwe, na maradhi yasiyo tarajiwa kupona, yeye pia anaweza kula, na juu yake amlishe masikini ambaye hamiliki hata chakula  cha siku moja yake. Na mwenye kujitolea kwa ridha yake kufunga zaidi kuliko faradhi itakuwa ni bora zaidi kwake. Kwani Saumu daima ni bora kwa mwenye kujua ukweli wa ibada.

Rudi kwenye Sura

 185. Na siku hizi ni za mwezi wa Ramadhani (1) mwezi wenye daraja tukufu kwa Mwenyezi Mungu ndipo ilipo teremshwa Qur'ani ili kuwaongoa watu wote kwa hoja zake zilizo wazi zinazo fikishia kheri, na zenye kutenga baina ya Haki na baat'ili kwa nyakati zote na vizazi vyote.  Basi mwenye kuuwahi mwezi huu naye ni mzima, si mgonjwa, yupo mjini si msafiri, yampasa afunge Saumu. Na aliye mgonjwa anaye dhurika kwa kufunga au alioko safarini anaweza kula, na juu yake kuzilipa zile siku alizo kula kwa kufunga utapo ondoka udhuru. Kwani Mwenyezi Mungu hataki kuwapatisha watu mashaka na taklifa  bali Yeye anapenda kuwafanyia watu sahala. Na Mwenyezi Mungu amekubainishieni Mwezi wa Saumu, na amekuongoeni ili mpate kutimiza siku za kufunga, na mumtukuze Mwenyezi Mungu kwa uwongofu alio kuongoeni, na akakupeni tawfiki njema.
(1)  Imethibiti  kwa  matibabu ya kisasa kuwa Saumu kwa namna ya Qur'ani  ina  faida nyingi, katika hizo ni kuwa inasaidia katika kutibu  maradhi ya sukari, inatengeneza matumbo, inapunguza maumivu ya viungo, na maradhi ya moyo, inapumzisha nyama za mwili, na inasafisha uchafu mwingi wenye madhara,  na pia inakuwa ni kinga kwa maradhi mengi mengineyo. Je, vipi kwa mtu asiye jua kusoma na kuandika ayajue yote haya?

Rudi kwenye Sura

 186. Na Mimi nawajua vyema waja wangu, na najua wanayo yafanya na wanayo yawacha. Na Ewe Muhammad! Wakikuuliza waja wangu wakasema: Hivyo Mwenyezi Mungu yupo karibu nasi hata ajue tunayo yaficha na tunayo yatangaza na tunayo yawacha?  Waambie: Mimi ni karibu nao zaidi kuliko wanavyo dhani. Na dalili ya hayo ni kuwa ombi la mwenye kuomba linafika wakati huo huo, na Mimi ndiye ninaye pokea hayo maombi wakati huo huo vile vile. Ilivyo kuwa Mimi nimewaitikia maombi yao basi na wao waniitikie Mimi kwa kuamini na kut'ii, kwani hiyo ndiyo njia ya kuongoka kwao na kusibu kwao.

Rudi kwenye Sura

 187. Mwenyezi Mungu amekuhalalishieni usiku wa kufunga kuingiana na wake zenu, na wao kuchanganyika nanyi katika maisha na katika malazi. Ilikuwa ni mazito kwenu kujitenga nao, na sasa mmepunguziwa hizo taabu. Mwenyezi Mungu anajua kuwa mlikuwa mkijipunguzia starehe ya nafsi zenu na mkijidhulumu kwa kujizuia msiingiane na wake zenu hata usiku wa Ramadhani. Sasa amekusameheni na kukupunguzieni mikazo. Sasa basi msione vibaya kuchanganyika nao, na stareheni kwa aliyo kuhalalishieni Mwenyezi Mungu, na kuleni na mnywe usiku wa Ramadhani mpaka mwone mwangaza wa alfajiri unapo tokeza kutokana na kiza cha usiku. Hapo tena fungeni na mtimize Saumu mpaka linapo kuchwa jua.
    Na ilivyo kuwa Saumu ni katika ibada zinazo taka mtu kujiepusha na matamanio ya roho na kuingiana na wanawake wakati wa mchana, basi kadhaalika katika ibada ya kukaa Itikafu msikitini inahitaji kujitenga na kuacha kustarehe na wake zenu wakati huo mnapo kuwapo katika Itikafu. Na haya ya sharia za Saumu na Itikafu alizo kuwekeeni Mwenyezi Mungu yashikeni baraabara msikaribie kuyavunja. Na Mwenyezi Mungu ameyaweka wazi haya kwa watu kwa namna hii ili wapate kuyaogopa na waepukane na matokeo yake.

Rudi kwenye Sura

 188. Mmekatazwa siku zote kula mali ya watu kwa njia isiyo ya haki. Mali ya mtu si halali kwenu ila kwa moja ya njia alizo wekea Sharia Mwenyezi Mungu, kama vile mirathi, au kutunukiwa kwa kupewa na mwenye mali, au kwa mkataba ulio sahihi wenye kuhalalisha kumiliki. Na huenda mmoja wenu hutafuta njia za kumpokonya mwenziwe haki ya mali yake kwa kupeleka kesi mahkamani ili yeye kwa kushirikiana na mahakimu au makadhi na kuleta ushahidi wa uwongo, au uwongo dhaahiri, au kutoa rushwa, wapate kula mali kwa dhulma. Huo ni uovu mno kwa wanao tenda, na malipo yao ni mabaya sana.

Rudi kwenye Sura

 189. Na watu wanakuuliza khabari za mwezi, unaanza mwezi mchanga kama uzi, kisha unakua mpaka unatimia kaamili. Tena unapungua mpaka unakuwa kama ulivyo anza. Haukai katika hali moja kama jua. Nini maana ya kugeuka huku hata inakuwa kila siku 29 au 30 unakuja mwezi mpya?
    Waambie: Huku kutokea hivi kuandama mwezi na kugeuka yapo ndani yake maslaha ya Dini na dunia pia. Hizi ni alama za  kuonyesha nyakati (1) za mambo ya maisha yenu. Zinaonyesha nyakati za Hija, ambayo ni moja katika Nguzo za Dini yenu. Na lau kuwa mwezi ungeli baki namna moja tu kama jua, msingeli tambua nyakati za maisha yenu na Hija zenu. Wala huko kutojua hikima ya kugeuka mwezi kusikupelekeeni kutilia shaka hikima ya Muumba. Wala sio wema kuziingilia nyumba kwa nyuma, kinyume na wafanyavyo watu wote. Lakini wema ni kumchamngu katika nyoyo na kumsafishia niya, na kuziingilia nyumba kwa kupitia milangoni kama wafanyavyo watu wote. Na mtake Haki na dalili iliyo sawa. Basi takeni radhi ya Mwenyezi Mungu, na muiogope adhabu yake na kwa hivyo ndio mtaraji kufanikiwa kwenu, na kufuzu kwenu na kuepuka adhabu ya Moto.
(1) Uislamu unahisabu mwezi unapo andama na kugeuka kwa watu kupimia nyakati za ibada, na pia kwa mambo yao ya kidunia, kwa sababu hayo ni mambo ya kuonekana, na kwa hivyo taarikhi inajuulikana kwa ya mwezi. Mwezi kwa hakika ni kama kioo kinacho onyesha mwangaza wa jua huku duniani. Mwezi ukiwa kati baina ya jua na dunia hauonekani, na baadae mwezi mchanga unaandama na wakaazi wa dunia wanajua kuwa mwezi mpya umeanza. Ukifika mwezi katika upande unao kabiliana baina ya jua na dunia ndio unapo kuwa wakati wa mbaamwezi, mwezi mpevu. Khalafu unaendelea kupungua kama ulivyo kuwa kwanza ukizidi kukua. Kwa hivyo taarikhi inaanza tangu pale ulipo kuwa mwezi mchanga. Pale unapo onekana mwezi mchanga kama uzi ndio mwezi umeandama, huonekana upande wa magharibi, hata kwa dakika chache baada ya kuchwa jua nao hupotea. Hivyo hivyo siku baada ya siku  huhisabiwa  mpaka  zipite siku 29 au 30.

Rudi kwenye Sura

 190. Na katika kumcha Mwenyezi Mungu ni kustahamili mashaka katika kumt'ii Yeye, na mashaka makubwa kabisa juu ya nafsi ni kuwapiga vita maadui wa Mwenyezi Mungu. Lakini wakikuvamieni, basi piganeni na hao wavamizi. Na mmepewa ruhusa kuurudi uvamizi wao, lakini nyinyi msivamie kwa kuanza nyinyi, au kwa kumuuwa asiye kupigeni vita wala hana mahusiano na vita; kwani Mwenyezi Mungu hawapendi wavamizi.

Rudi kwenye Sura

 191. Wauweni walio kuanzeni vita popote mnapowakuta, na watoeni Makka, wat'ani wenu ambao wamekulazimisheni kuutoka. Wala msione vibaya, kwani walio kufanyieni nyinyi ni maovu zaidi kuliko kuuwa msikitini, nako ni kuwafitini Waumini katika Dini yao kwa kuwaadhibu huko Makka mpaka wakauacha mji wao kuhifadhi Dini yao. Na huu Msikiti Mtakatifu una utakatifu wake, basi msiuvunje kwa kupigana ndani yake. Lakini wakikupigeni vita ndani yake basi nanyi pia wauweni, na nyinyi kwa fadhila ya Mwenyezi Mungu, mtashinda. Na malipo ya makafiri ni kufanyiwa wanayo wafanyia watu.

Rudi kwenye Sura

 192. Wakirejea wakaacha ukafiri, wakafuata Uislamu basi Uislamu humuitikia anaye uelekea. Na Mwenyezi Mungu atawasamehe ule ukafiri wao wa zamani kwa fadhila yake na rehema yake.

Rudi kwenye Sura

 193. Wapigeni vita walio taka kukuuweni na kukugeuzeni muache Dini yenu kwa maudhi na mateso  mpaka ing'oke mizizi ya fitina na isafike Dini iwe ya Mwenyezi Mungu tu. Wakiuacha ukafiri wao basi wamejiokoa nafsi zao na wataepukana na adhabu. Hapo basi haifai kuwafanyia uadui. Uadui hufanyiwa mwenye kuidhulumu nafsi yake akaiteketeza kwa maasi na akaacha uadilifu kwa maneno na vitendo.

Rudi kwenye Sura

 194. Na pindi wakikushambulieni katika mwezi mtukufu msiache kupigana nao, kwani huo ni mtukufu kwao kama ulivyo kuwa mtukufu kwenu. Ikiwa wao watauvunja utukufu wake basi nanyi wakabilini kwa kuzilinda nafsi zenu katika huo mwezi. Na katika mambo matukufu na matakatifu pana sharia ya kisasi na kutendeana mfano kwa mfano. Anaye kushambulieni katika matakatifu yenu nanyi jilindeni na uadui huo kwa mfano wake. Na mcheni Mwenyezi Mungu, msikiuke mipaka katika kulipiza kisasi. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuwanusuru wachamngu.

Rudi kwenye Sura

 195. Kupambana na makafiri kunahitaji kutoa roho kama ilivyo kutoa mali. Basi toeni kwa kuandaa vita, na jueni kuwa kupigana na hawa ni kupigana katika Njia ya Mwenyezi Mungu. Basi msikae tu. Toeni mali kwa ajili yake, kwani mkitofanya na mkafanya ubakhili adui atakupandeni na atakudhilini. Hapo itakuwa kama mlio jitokomeza wenyewe kwenye maangamio. Tendeni lilio kuwajibikieni kwa uzuri na vilivyo, kwani Mwenyezi Mungu hupenda anapo fanya jambo mtu alifanye vizuri.
Aya 190 mpaka 195 zinaeleza sharia ya vita katika Uislamu. Nazo zinaeleza kwa matamshi yalio wazi haya yafuatayo:
*1. Ruhusa ya kupigana imetolewa kwa ajili ya kujilinda na uvamizi wa vita wa vitendo khasa, au zikidhihiri dalili kuwa maadui wanataka vita. Vita havikulazimishwa kwa ajili ya vita wala kwa sababu ya kutaka kuwasilimisha watu kwa kuwauwa na kuwapiga  vita.
*2. Kunakatazwa kuvamia au kuanza uadui kwa njia yoyote ile. Basi hapana ruhusa kufanyiwa uadui asiye pigana, wala hapana ruhusa kuvuka mipaka ya uadui wakati wa vita: basi hauliwi asiye chukua silaha, wala hakhusiani na vita bali ni mwenye kukumbwa tu na vita. Wala hauliwi mwenye kusalimu amri na akatupa silaha. Wala hapana ruhusa kuwavunjia watu nyumba zao, huko ni kupita mpaka.
*3. Mzingatie fadhila iliyo onyeshwa kwa kuamrishwa kuchamngu. Basi msivunje heshima ya wanawake kuwanajisi, hata washirikina wakifanya hayo. Wala msiwakatekate walio uwawa hata ikiwa makafiri wakiwafanyia hayo Waumini. Washirikina walimfanyia hayo Bwana wa Mashahidi, Hamza, wala Mtume s.a.w. hakutoa ruhusa kumfanyia hayo maiti yeyote, bali alikataza akasema:"Tahadharini msiwakatekate maiti".
*4. Vita vinakwisha wakiacha washirikina kuwafitini Waumini katika Dini yao, na Dini inakuwa inataka akili na nyoyo zimwelekee Mwenyezi Mungu kwa uhuru.
*5. Hapana vita katika mwezi mtukufu, nayo ni miezi ya Hija na Umra. Ikiwa washirikina watapigana katika miezi hiyo, basi Waumini nao yawapasa wapigane.
*6. Kuacha kutoka kwenda pigana  na maadui wanauwa pasina nasi kupigana nao ni kuipoteza kheri na wema. Kwa haya inadhihiri kuwa vita vya Islamu vina fadhila katika sababu zinazo pelekea kuanza kwake, na vina uadilifu katika kuviendesha. Viwapi hivi na vita vya mataifa mengine ya zamani na ya sasa! Vita vyao hao ni vya uchafu, na vita vya Islamu ni vya Haki na vyenye fadhila.

Rudi kwenye Sura

 196.Timizeni Hija na Umra kwa ajili ya Mwenyezi Mungu kwa ukamilifu, wala yasiwe makusudio yenu ya kidunia kama kutaka umaarufu na kadhaalika. Mkiharimia Hija na Umra akakuzuieni adui njiani basi mtatoka katika Ihram yenu kwa kunyoa nywele. Lakini kabla ya hayo mchinje mnyama aliye mwepesi kumpata, kama mbuzi au ngamia au ng'ombe, na kumtoa sadaka kwa masikini. Wala msinyoe mpaka mtimize haya. Mwenye kuharimia akapata maudhi katika nywele zake kwa maradhi au wadudu hapana ubaya kunyoa. Juu yake hapo atoe fidiya kwa kufunga siku tatu, au kutoa sadaka kuwalisha masikini sita chakula cha kutwa, au kuchinja mbuzi na kumtoa sadaka kwa masikini. Na ikiwa mpo katika amani na salama na hakukutokeleeni adui njiani, na mkakusudia Hija na Umra, na mkajistarehesha kwa kufanya Umra kwanza mpaka ufike wakati wa Hija ndio mharimie, basi inakupaseni kuchinja mbuzi kwa ajili ya masikini na mafakiri wa Makka. Asiye pata mbuzi au hamiliki bei yake afunge siku tatu hapo Makka, na siku saba akisha rejea kwao. Haya ni kwa aliye kuwa hana watu wake Makka. Kwa mwenye watu wake Makka hapana kitu akijistarehesha.

Rudi kwenye Sura

 197. Na Hija inakuwa katika miezi mnayo ijua, kwani jambo hili ni maarufu kwenu tangu zama za Ibrahim a.s. nayo ni miezi ya Mfungo Mosi, Mfungo Pili na Mfungo Tatu. Mwenye kuazimia faridha ya  Hija katika miezi hii na akaingia basi afuate vilivyo adabu zake. Katika adabu za Hija ni kuwa mwenye kuharimia ajiepushe na kuingiana na wakeze, na kufanya maasi ya kutukanana na mengineyo, kujadiliana na kubishana na Mahujaji wenziwe, na ajiepushe na kila linalo pelekea chuki na khasama ili atoke katika Ihramu yake naye hali ana hishima yake. Ajitahidi kufanya kheri na kutafuta malipwa kwa Mwenyezi Mungu kwa kutenda mema, kwani Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyajua hayo na ni Mwenye kulipa vitendo vyema. Na mchukue zawadi za Akhera yenu kwa kuchamngu na kufuata amri za Mwenyezi Mungu na kuyaepuka ayakatazayo. Hiyo, basi ndio zawadi bora.  Na kuweni wenye kuhisi khofu ya  Mwenyezi Mungu katika yote mnayo yafanya na mnayo yawacha kwa mujibu wa akili na hikima njema. Katika vitendo vyenu vyote msichanganyishe hata chembe na mambo ya pumbao au makusudio ya kidunia.

Rudi kwenye Sura

 198. Na walikuwako miongoni mwenu ambao wakiona vibaya kufanya biashara na kutafuta riziki wakati wa msimu wa Hija. Basi mnaambiwa kuwa hapana ubaya kwenu hayo, bali mnaweza kuchuma maisha kwa njia ziliyo ruhusiwa na sharia, na mtafute fadhila na neema za Mwenyezi Mungu. Wakitoka Mahujaji A'rafat baada ya kusimama huko, na wakafika Muzdalifa katika mkesha wa Idi ya Kuchinja, wamtaje Mwenyezi Mungu hapo Masha'ril Haram, napo ndipo kwenye kilima cha Muzdalifa, kwa kusoma Tahlili na kuitikia Labbaika na kusoma Takbir. Na wamtukuze Mwenyezi Mungu wakimhimidi na kumshukuru kwa vile alivyo waongoa kwenye Dini ya Haki na ibada iliyo nyooka katika Hija na Umra, na ilhali kabla ya hapo walikuwa katika walio potea njia ya uwongofu.

Rudi kwenye Sura

 199. Makureshi walikuwa hawasimami na watu wengine katika A'rafat juu ya kuwa wakijua kuwa baba yao Ibrahim akisimama hapo. Na hayo ni kwa kujitukuza wasiwe sawa na wengineo na hali wao ati ni watu wa Nyumba ya Mwenyezi Mungu na ni wakaazi wa katika pahala patakatifu. Wakidai kuwa hayo ni kuitukuza Makka wasitoke kwenda A'rafat ambako si kutakatifu kama Makka. Mwenyezi Mungu akawalazimisha wazing'olee mbali hizo ada za kijinga, na wasimame katika A'rafat, na watoke huko kama watokavyo watu wote. Kwani hapana yeyote aliye bora kuliko mwengine katika utendaji wa ibada. Na inawapasa wamwombe Mwenyezi Mungu maghfira katika mwahala humu mwenye baraka. Hayo ndiyo yana maelekeo zaidi Mwenyezi Mungu kuwasamehe dhambi na makosa yao, na akawarehemu kwa fadhila yake.

Rudi kwenye Sura

 200. Mkisha maliza a'mali za Hija na ibada zake wacheni mliyo kuwa mkiyafanya zama za ujahili ya kutafakhari kwa baba zenu na kukumbusha mambo yao, bali makumbusho yenu na kutukuza kwenu kuwe kwa Mwenyezi Mungu kama mlivyo kuwa mkiwakumbuka baba zenu, bali mtajeni Yeye kwa wingi zaidi kuliko wazee wenu, kwani Yeye ndiye Mwenye kuzitawala neema zenu na neema za baba zenu vile vile. Na humu mwahali mwa Hija ndio khasa mwahala mwa dua na kuombea fadhila na kheri na rehema zitokazo kwa Mwenyezi Mungu. Na walikuwako baadhi ya Mahujaji wakifupiza dua zao kwa mambo na kheri za dunia tu. Hao hawapati sehemu yoyote ya Akhera.

Rudi kwenye Sura

 201. Na wapo watu ambao Mwenyezi Mungu amewawezesha nyoyo zao zikapelekea kuomba kheri ya dunia na Akhera, na wakamwomba Mwenyezi Mungu awaepushe na shari na adhabu ya Moto.

Rudi kwenye Sura

 202. Hawa wanapewa kama walivyo jaaliwa kuyachuma kwa kumwomba na kumtegemea Mwenyezi Mungu.  Na Mwenyezi Mungu humlipa kila mtu kama anavyo stahiki, na ni Mwepesi wa kuhisabu na kulipa.

Rudi kwenye Sura

 203. Na mtajeni Mwenyezi Mungu kwa Takbiri na vinginevyo katika siku maalumu, nazo ni siku za kutupa mawe (1) hapo Mina, nazo ni taarikh 11 na 12 na 13. Na si lazima kwa Haji kukaa siku tatu hizi Mina akitupa mawe, bali anaweza kufupiza siku mbili, kwani msimamo wa kheri ni kuchamngu, si idadi. Na daima mcheni Mwenyezi Mungu, na jueni kuwa kwake Yeye mtakusanywa na muulizwe mliyo yatenda.
(1) Hayo mawe ni changarawe hutupwa mwahala maalumu katika Mina katika siku ya kuchinja (Idd) na siku tatu zifwatiazo.

Rudi kwenye Sura

 204. Ilivyo kuwa kumcha Mwenyezi Mungu ndio msingi, basi khasara ni ya wale watu ambao dhamiri walio nayo nyoyoni mwao ni mbali na maneno yanayo tamkwa na ndimi zao. Wamepewa utamu wa kupanga maneno, hukufurahisha kauli yao katika kujivutia manufaa ya maisha ya kidunia, na kuunga mkon