Wacha Biblia Iseme
Imetungwa na Sheikh Ali Muhsin
Bismillahi Arrahmani Arrahim
Kwa
Jina La Mwenyezi Mungu Mwingi Wa Rehema Mwenye Kurehemu
SHUKRANI
Kwanza namshukuru Mwenyezi
Mungu kwa kuniongoza Njia iliyonyooka.
Pia nampa ahsante Bw. Kingsley Green, Mwalimu wa
biology wa asli ya Kiaustralia aliyekuwa akisomesha Mazengo
Secondary School, Dodoma,
Tanzania, ambaye kwa kuwa ni
mhubiri alikuwa akija kutuzuru gerezani tulipokuwa tumewekwa kizuizini baada ya
kupinduliwa serikali yetu ya Zanzibar.
Kwake yeye nilijifunza kuisoma Biblia kwa nidhamu.
Hali kadhaalika nawapa ahsante wahubiri wengi wa Kikristo waliokuwa
wakituhubiria nilipokuwako Chuo Kikuu Makerere, na nilipokuwako kizuizini. Kwa
wanafunzi wenzangu na wafungwa wenzangu ambao nikijadiliana nao kirafiki katika
mambo ya dini nina deni kubwa la shukrani.
Ni waajibu wangu kushukuru Shirika la Kimataifa la Msamaha (Amnesty
International) kwa kuniletea vitabu nilipokuwa kizuizini, ambavyo vitabu hivyo
vimenisaidia sana
kunizidishia maarifa juu ya mawazo ya Kikristo ya hivi sasa.
Sina fadhila ya kumlipa Baba yangu mzazi, Sheikh Muhsin bin Ali Barwani (ambaye
kwake ndio nimesoma sana
ilimu za dini ya Kiislamu), na kaka yangu Sheikh Muhammad Muhsin, na mashekhe
na walimu kadhaa wa kadhaa wengineo niliosoma kwao. Miongoni mwa hao ni
Sheikh Abubakar Baakathir, Sheikh Muhammad bin Omar Al Khatib, Sheikh Suleiman
Al Alawy, Sheikh Burhan Mkelle, Sheikh Abdulrahman Muhammad Al Kindy, Sheikh
Said bin Abdulla Lindi, na Sheikh Abdulla Saleh Al Farsy. Pia nawashukuru kwa
kuniongoza kwa nasaha na mifano Habib Omar bin Sumeit, Sayyid Ahmed bin Husein,
Sheikh Abdulla Muhammad Al-Hadhramy, Sheikh Muhammad Abubakar, Sheikh Muhammad
Salim Barwani (Jinja), Sayyid Hamid Mansab na Sheikh Abdulla bin Suleiman Al
Harthy. Sina la kuwalipa ila kuwaombea Mwenyezi Mungu awarehemu, na kama itapatikana faida yo yote kwa walionifundisha basi
thawabu zake zirejee kwao mashekhe na walimu wangu niliowataja na nisiowataja.
Mwishoni siwezi ila kumshukuru mwenzangu wa maisha, mzazi mwenzangu, Azza bint
Muhammad bin Seif, ambaye kwa subira yake na ushujaa wake na imani yake iliyo
kubwa, ndio nikaweza kubeba taabu za kizuizi zaidi ya miaka kumi, huku yeye
peke yake akijitazama mwenyewe na watoto wetu, naye yupo uhamishoni kama ni mkimbizi katika nchi ya ugeni Misri.
Ingelikuwa si yeye na wema wa wahisani wetu wa Kimisri, na khasa katika
wao Dr. Abdoh Sallam, Bw. Fathi Sabri, Dr. Mustafa Momen, Dr. Farid Abul Ezz,
Bw. Hilmy Shaarawy, Bw. Bahgat Disouqy na Dr. Muhammad Abdul-Aziz Is'haq, mimi
nisingekuwa na tamakuni ya moyo hata nikaweza kusoma nilikosoma, kuchungua
nilikochungua, na kuandika nilikoandika nami nimo katika utumwa wa kifungoni.
Taarikh 2 Ramadhani mwaka 1409 A.H. iliyo wafikiana na 7 Aprili 1989, mwenzangu
wa miaka 45, Mama Azza, aliniacha mkono, Mwenyezi Mungu akamkhitari. Shida na
taabu zilizo mpata kwa yaliyo tokea kwetu, na kifungo changu, na maisha ya
ukimbizi kwa robo karne, yalimuathiri afya yake sana na mwisho ndio akanitoka katika umri wa
miaka 63.
Fadhila ya uchapishaji kitabu hichi kwa Kiswahili na kabla yake kwa Kiingereza
inarejea kwa Muislamu mtenda wema, Dr. Moawiyah Shunnar wa Dubai, Mwenyezi Mungu amjaze kila kheri.
