4- MTAKATIFU  PAULO

Mt Paulo alikuwa Myahudi aliyezaliwa katika mji wa Tarsus katika nchi ijuulikanayo hivi sasa kuwa ni Uturuki.  Alipozaliwa nchi hiyo ilikuwa ni sehemu ya mamlaka ya Dola ya Kirumi.  Kwa hivyo ijapokuwa kwa kabila na dini alikuwa ni Myahudi, kwa uraia alikuwa ni Mrumi.  Paulo hakuwa katika wanafunzi aliowateuwa Yesu katika uhai wake.  Kwa hakika hapana dalili kuonyesha kuwa hata hao wawili waliwahi kukutana.  Linalojuulikana ni kuwa ni mtu aliyepita mipaka katika chuki zake kuwachukia Wakristo, na mwenyewe alijitwika jukumu la kuwasaka Wakristo kila kipembe walipojificha ili wapelekwe kuteswa na kuuwawa.  Yeye alishiriki wakati alipokuwa anarujumiwa kwa mawe Mtakatifu Stefano, shahidi wa mwanzo wa Kikristo.
Alipokuwa yuko njiani anakwenda Dameski (Dimishqi) miaka kadhaa wa kadhaa baada ya Yesu kwisha ondoka duniani, yasemekana kuwa Paulo alijiwa na Yesu ambaye alimwambia maneno fulani. Tangu hapo akaingiwa na hamu kubwa ya kutaka kuwaita watu waingie katika dini ya Kikristo.  Juu ya hivyo huo Ukristo wa Mt Paulo aliodai kuwa umefunuliwa kwake na Yesu mwenyewe, ni namna mbali kabisa na Ukristo waliokuwa wamefunzwa wanafunzi wake Yesu, alioweteuwa mwenyewe na akawafunza katika uhai wake. Kwa hivyo pakatokea mzozano  mkubwa baina ya Paulo na wanafunzi wa Yesu wa asili, ambao walikuwa wanashikilia kufuata sharia ya Musa, kama alivyokuwa akiifuata mwenyewe Yesu.
Kwa kuwa alielewa vyema ilimu na ustaarabu wa Kirumi na Kiyunani (Kigiriki), na kuwa alikuwa ni mtu mwenye akili, Paulo aliweza upesi kuwa ni kiongozi katika wale wanafunzi wa Yesu, ijapokuwa yeye hakika hakupata kumwona Yesu ila katika hiyo ndoto iliyomjia alipoanguka njiani kwa kupigwa jua kali. Kwa uhodari wake aliweza kuathiri sana mawazo na fikra za dini ya Kikristo kama inavyojuulikana hii leo.  Jinsi mawazo yake yalivyotawala na kuenea hata baadhi wanamwona kuwa ni yeye ndiye muanzishaji wa Ukristo. Mafunzo ya imani ya Paulo hayakutegemea sana juu ya maneno na vitendo vya Yesu kama yalivyotegemea juu ya falsafa za Kigiriki, itikadi za Kiyahudi, na itikadi za kipagani (kishirikina) zilizokuwa zimeenea katika eneo lile la dunia wakati ule. Kwa hivyo utaona kuna mkorogo na migongano katika imani ya Mungu mmoja kama alivyokuwa akiamini Yesu pamoja na Mayahudi wote, na imani ya miungu kadhaa kama walivyokuwa wakiamini mapagani wa Kirumi, Kigiriki, Kimisri na Kiajemi katika zama zile.  Utaona mgongano baina ya imani ya wanafunzi wake Yesu kuwa Yesu hakuuliwa msalabani, na imani ya Mayahudi kuwa wamemwua kwa kumtundika msalabani na kwa hivyo kafa kifo cha laana, kama isemavyo Taurati kuwa anayekufa kwa kutundikwa huyo ni mlaanifu. Kwa uhodari mkubwa Paulo alikusanya ya huku akachanganya na ya huku akaunda hii ijuulikanayo kuwa ni Thiolojia (ilimu ya Ungu) ya Kikristo. Yeye alikuwa ni mhubiri mwenye hima na hamasa kubwa, na alikuwa tayari, kama anavyojisifu mwenyewe, afanye lo lote ili makusudio yake yatimie, yaani apate wafwasi wengi kama inavyowezekana.
Barua zake alizokuwa akiwapelekea Wakristo mbali mbali zimo katika Biblia na zinahisabika kuwa ni sehemu ya Agano Jipya. Muhimu katika mafunzo yake ni kuwa mtu anapata haki kwa imani si kwa vitendo, na imani ya kwamba kila mwanaadamu kazaliwa na dhambi ya asili ambayo haifutiki ila aamini kuwa Bwana Mungu kamleta mwanawe wa pekee kuja duniani ili ateseke na auliwe msalabani kuwa kama ni kafara ya hiyo dhambi ya tokea Adam. Hayo yanatosha. Kufuata sharia sio muhimu.  Ni yeye Paulo ndiye aliyeondoa na kubatilisha sharia ya tangu Ibrahim ya kuingia tohara, na kuwa nyama wasiochinjwa, na nguruwe ni haramu.  Sharia zote ambazo Yesu na wanafunzi wake wote walikuwa wakizifuata Paulo alifunza kuwa hazina maana. Haya yalikuwa na maana kabla Yesu hajajitoa mhanga msalabani.  Baada ya hapo litakikanalo ni Imani tu ya uwokozi wa watu kwa kifo cha Yesu msalabani.
Jengine lililoleta ugomvi baina yake Paulo na wanafunzi wa asili wa Yesu ni kuwa mafunzo ya Yesu kwenda kufunzwa kabila nyengine zisiokuwa Wana wa Israili, ndio hao waitwao "Mataifa" katika Biblia. Wanafunzi wa Yesu kwa kufuata amri zake mwenyewe alizohimiza mara kadhaa wa kadhaa walipinga shauri ya Paulo kutaka kuwahubiria dini watu wasiokuwa Bani Israili. Paulo kwa ukaidi wake, na werevu wake mwingi aliwashinda nguvu wanafunzi wa Yesu waliopewa jukumu kuitangaza dini katika taifa la Israili tu.
Paulo aliuliwa kwa kukatwa kichwa karibu na Roma baina ya mwaka 61 B.K. na 68 B.K.