"U'tawa
uliotegemezwa juu ya makosa huwezi kuutetea."
Father John L. Mackenzie
Maana ya neno "Kanisa" ni mkusanyiko wa Wakristo,
au khasa ni mapadri ambao wamejipa kazi ya kutengeneza imani na ibada na vile vile
kutoa huduma maalumu za kidini kwa kufuata yale yanayoaminiwa kuwa ni mafunzo
ya Yesu Kristo. "Kanisa" yaweza kuwa vile vile na maana ya
madhehebu fulani ambayo Mkristo anaikubali na kuifuata, kama vile Kanisa la
Kikatoliki, la Kianglikana, la Kiluteri n.k. Mbali na kuwa neno
"Kanisa" pia lina maana ya kawaida ya kuwa ni jengo la ibada la
Wakristo, kama ulivyokuwa Msikiti kwa Waislamu, na Hekalu kwa wengineo.
Takriban makanisa yote, au madhehebu zote za Kikristo, zinashikilia itikadi
hizi zifwatazo bila ya wasiwasi wo wote au kutaka kusaili cho chote.
Imani kama hizo huitwa
"Dogma", yaani imani za kuaminiwa bila ya kusailiwa kuwa zaingia
akilini au la:
1.
Yupo Mungu Mmoja.
2.
Katika Mungu zipo Nafsi
tatu, Baba, Mwana na Roho Mtakatifu. Nafsi hizi tatu zinaitwa Utatu
Mtakatifu. Zote Nafsi tatu ni sawa, zote ni za milele, yaani hazina
mwanzo wala hazina mwisho. Hizo si miungu mitatu, bali ni Mungu Mmoja.
3.
Baba ni Mungu na ndiye
Nafsi ya kwanza katika Utatu Mtakatifu.
4.
Mwana ni Mungu na ndiye
Nafsi ya pili katika Utatu. Yeye ni Yesu Kristo ambaye ni Mungu aliyekuja kwa
sura ya mtu. Hakuumbwa, lakini alizaliwa na Bikra Maria yapata karibu miaka
elfu mbili iliyopita katika nchi ya Palastina, akasalibiwa, akafa na akafufuka
kutoka wafu siku ya tatu. Kifo chake na mateso yake msalabani yalikusudiwa kuwa
ni kafara ili dhambi za wanaadamu zisamehewe. Hii ndiyo yaitwa Kafara ya
Yesu, na kwa hivyo yeye anaitwa Mwokozi.
5.
Roho Mtakatifu ni nafis ya tatu
ya Utatu Mtakatifu. Baada ya kufa kwa Yesu Kristo, Roho Mtakatifu
aliwateremkia "Mitume" (wale wamishinari wa mwanzo) wa Yesu Kristo,
na huyo Roho anaendelea kuliongoza Kanisa.
6.
Kila mtoto wa kibinaadamu anayo
dhambi, hiyo inayoitwa Dhambi Ya Asili iliyorithiwa kutokana na uasi wa Adam alipovunja
amri ya Mungu kumkataza asile tunda, naye akala yeye na mkewe Hawa.
7.
Ubatizo, ibada ya kummichia mtu
maji, au kwa mujibu wa baadhi ya madhehebu, kumzamisha mtu katika maji, kuwa ni
ishara ya kukubaliwa katika Kanisa, na imani ya Kafara ya Yesu Kristo ni njia
pekee ya kuokoka.
Kwa
kirasmi itikadi hizo zimo katika hiyo iitwayo Imani ya Mitume. Kinyume na dhana
ya wengi kuwa imani hiyo ilianzishwa na hao waitwao Mitume wa Yesu (yaani
wafwasi wake aliowatuma), yajuulikana kuwa ilitungwa baadae sana. Baadhi
ya wataalamu wa Kikristo wanasema ilitungwa mwaka 150 baada ya Kristo, wengine
katika karne yane. Kwa sura hii ilivyo sasa ilianza kutumiwa katika
karne ya nane. Katika Kanisa Katoliki Imani ya Mitume husomwa katika
ibada za Misa, katika kubatiza, na penginepo. Katika makanisa ya Kiprotestani
husomwa katika ibada za Jumaapili.
Aghlabu ya madhehebu za Kikristo zinaikubali imani hii kama hivi ifwatavyo:
Imani ya Mitume
1.
Namuamini Mungu Baba Mwenye nguvu zote,
Muumba Mbingu na ardhi,
2. Na Yesu Kristo, Mwanawe wa pekee, Bwana wetu,
3. Aliyechukuliwa mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu, akazaliwa na Bikira Maria,
4.
Akateseka chini ya Pontias Pilato,
akasalibiwa, akafa, na akazikwa;
5.
Alishuka Jahannamu; siku ya tatu Alifufuka
tena kutoka wafu.
6.
Akapaa Mbinguni, ameketi mkono wa kuume
wa Mungu, Baba Mwenye nguvu zote;
7.
Kutoka huko atakuja kuwahukumu walio
hai na wafu;
8.
Naamini: Roho Mtakatifu,
9.
Kanisa Takatifu Katoliki, ushiriki wa
watakatifu,
10. Kusamehewa dhambi,
11. Kufufuka mwili, na
12. Maisha ya milele.
Angalia
katika 9 hapo juu, neno "Katoliki" lina maana la wote, yaani
Wakristo, sio kwa maana la Kanisa la Roma tu, ambalo ndilo linalotumia jina hilo
kwa ukamilifu wake: Kanisa Katoliki la Roma.
Sasa na tuyachungue mafunzo ya Kanisa kwa mujibu wa mwangaza wa maandishi ya
Biblia ambayo Kanisa la Kikristo kwa jumla linakubali kuwa ni Neno la Mungu
lenye mamlaka yote.