21- MWISHO

Nalianza risala hii kwa kunukulu maneno aliyoyasema Father John Mackenzie. Sioni bora kuliko kumalizia kwa kuyanukulu maneno ya Mkristo mwingine, Geoffrey Parrindar, aliyeandika katika kitabu chake Jesus in the Quran (Yesu katika Qur'ani). Amesema:

Inadhaniwa, bila ya kuzingatia vilivyo, ya kwamba imani zote zinazoaminiwa kwa dasturi, kuwa msingi wake ni Biblia. Fikra za kumfikiria Mungu zenye asli ya vitabu vya mbinguni, yafaa zisafishwe na yale mawazo ya Kigiriki yaliyozipamba.  Tena pia ikiwa ilimu ya "Thiolojia" (Ilimu ya Ungu) iambatane na ulimwengu wa leo, basi ni lazima ielezwe kwa njia yenye maana.  Maneno kama Mwana wa Mungu, Utatu na Uwokofu yapasa yapewe sura nyingine na maana nyingine.  Mawazo ya unabii, na ufunuo, lazima yachunguliwe upya kwa vile ya kuwa hakika bila ya shaka yo yote Mwenyezi Mungu amemfunulia Muhammad katika Qur'ani.  Tena yapasa tuonyeshe ukarimu zaidi na mafahamiano mema zaidi kwa watu wa dini nyenginezo.  Sisi mara nyingi tunafedheheshwa vile walivyo kuwa Waislamu wanatuonyesha mfano bora kwa Watu wengine wa Kitabu.  Siku zote Wakristo yahitaji wakumbuke maneno ya Yesu, "Kwa nini kuniita, Bwana, Bwana, na hamfanyi niyasemayo?"