16- MWILI NA DAMU YA YESU
Yesu
alipobashiri kuja kwa huyo "Msaidizi" ambaye atauhakikisha ulimwengu
kwa khabari ya dhambi kwa sababu watu walikuwa hawamuamini yeye, alikuwa
anasema kweli tupu. Kwani yeye alikuwa kawajia Waisraili ambao walikuwa
wakishikilia sana kufuata madhaahiri ya sharia na wakapuuza undani wake.
Wakiitenda sharia ila imani yao ilikuwa chache, na uchamngu wao ulikuwa dhaifu.
Jitahada yake ilikuwa bure kuwahimiza kuwa yapasa vitendo vyao vinavyoonekana
vichanganyike na imani ya roho. Alijaribu kuwafanya wafahamu
khitilafu iliopo baina ya mikazo inayoletwa na wanaadamu na sharia za milele za
Mwenyezi Mungu. Aliwaambia:
Mwaikataa amri ya
Mungu mpate kuyashika mapokeo yenu.
Marko 7.9
Yesu
hakuanzisha sharia yo yote mpya. Kazi yake ilikuwa kuitimiza sharia ya
Musa kwa uchamngu. Lakini baada yake ulizuka mzozano juu ya tafsiri ya sharia.
Kikundi kimoja miongoni mwa wafuasi wake kiliona kuwa maadamu yeye ni Muisraili
aliyefuata sharia na hataki kutengua sharia hata nukta moja, basi ni waajibu
kwa wafuasi wake wote wafuate sharia kwa kila neno, kama yeye, hata katika
mambo ya kutahiri, na kuacha kula nyama za haramu kama nguruwe na
visivyochinjwa kisharia na damu, na kuitukuza Jumaamosi kuwa ni siku ya Sabato.
Hawa ndio wanaitwa Wakristo wa Kiyahudi. Kikundi kingine, na mkubwa wao
ni Paulo, kilichoathirika na upagani wa Kizungu, kiliona uzito kujifunga na
sharia za Musa. Kilitoa hoja kuwa maadamu Yesu hakutoa sharia mwenyewe basi wao
ni huru, kwani Yesu kwa kufa msalabani damu yake imekwisha wakomboa
wanaomuamini na mikazo ya sharia. Sharia ni laana, na Yesu kwa kufa kifo cha
laana msalabani amechukua yeye dhambi za watu, na vile vile ameondoa laana ya
sharia. Liliokuwa la lazima si matendo ya sharia bali kuamini tu kuwa Yesu
amekufa msalabani kwa ajili yao. Huo ni uokofu wa kutosha. Ili imani hii iingie
na isaki katika akili na nyoyo za waumini ikazuliwa hiyo ibada iitwayo
Ekaristi, au Chakula cha Bwana, Ushiriki au Misa takatifu. Katika ibada hii ya
kuonyesha neema ya dhaahiri na ya ndani, au ya kiroho, huliwa kidogo mkate
uliobarikiwa, na hunywewa mvinyo kidogo iliyobarikiwa, kwa kuwa ni mwili na
damu ya Yesu. Injiili inasema:
Nao walipokuwa
wakila, Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake,
akasema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu. Akakitwaa kikombe,
akashukuru, akawapa, akisema, Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo
damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi.
Mathayo 26.26-28
Upton
Sinclair katika kitabu chake A Personal Jesus anatoa maoni yake juu ya
maneno hayo ya Injili tuliyoyanukulu:
"Kutokana na
hayo umetokea mtindo uitwao Ekaristi, Ushiriki, Misa: ibada ya taadhima
isiyokadirika. Badala ya kumtoa mhanga mwana kondoo asiyejifaa kitu, ni
mwili wa Yesu uliotolewa mhanga msalabani, na damu yake iliyomwagwa, na kwa
mageuzo ya ajabu mkate na mvinyo ikawa ni mwili wake na damu yake, na wewe
unakaa kwa unyenyekevu ukila na ukinywa au unamuacha padri akulie na
akunywie. Mamilioni na mamilioni ya maneno yametumiwa katika kuhojiana,
na maelfu ya vitabu vimepigwa chapa juu ya suala hili; vipi mageuzo hayo
yanatokea...Wakatoliki wanaamini hayo wanayoyaita Mahudhurio ya Hakika (Real
Presence); yaani, wanasema kuwa ule mkate na ile mvinyo hakika inakuwa ni mwili
na damu, ijapokuwa sura yao inabaki vile vile kama mkate na mvinyo. Wote
Wakatoliki wachamngu huenda kila wiki waone kitendo hichi kikitendwa na padri,
na tena hapo ndio wanajua kuwa roho zimesalimika na moto wa jahannam.
Mimi sitaki kumuudhi mtu ye yote, na kwa hivyo najitosheleza nafsi yangu kwa
kusema kuwa mimi siamini kuwa Yesu alikuwa akishughulikia mtindo huu."
Marcello Craveri anasema juu ya jambo hili hili katika kitabu chake The Life
of Jesus (Maisha ya Yesu):
"Ikiwa
tunaamini kuwa Yesu ni mwanaadamu, basi hichi Chakula cha Bwana (Misa au
Ekaristi) kinakuwa na sifa ya ibada ya wala-watu; ikiwa tumfanye kuwa ni Mwana
wa Mungu, ile fikra safi na tukufu ya Mwenyezi Mungu ambayo mwenyewe Yesu
akiishika, inaporomoka chini na kuwa ni itikadi ya mungu dhaalimu asiye na
huruma anayetaka daima dawamu Mwanawe mteule atolewe kikoa."
Mtaalamu huyo wa Kitaliana ameendelea kueleza katika kitabu chake kuwa mtindo
huu kwa hakika ameuzua Paulo kufuata mitindo ya kikafiri (kipagani) iliyokuwa
imeenea wakati ule katika pande zile. Anaendelea kusema:
"Maandishi
ya Injili yakajazwa kwa kuongezwa na Paulo, ambaye alibatilisha ukweli wote wa
historia (taarikh) kwa ajili ya kufuata maelekeo ya imani yake, na huku
akitangaza bila ya kuona haya wala aibu kuwa kila kitu amekipata moja kwa moja
kutokana na Yesu mwenyewe. Ni yeye ndiye aliyemfanya Yesu aseme baada ya
kukata mkate: Chukueni, kuleni; huu ni mwili wangu, uliovunjwa kwa ajili
yenu. Na huku akiibariki mvinyo: 'Kikombe hichi ndio agano jipya katika damu
yangu.'"
Ushahidi wa kuwa hadithi hiyo, yaani kuwa Yesu kawataka wanafunzi wake wale
mkate na mvinyo kuwa ndio mwili wake na damu yake, imezuliwa na kubuniwa na
Paulo, umo katika barua yake mwenyewe Paulo aliyowaandikia Wakorintho:
Kwa maana mimi
nalipokea kwa Bwana niliyowapa nanyi, ya kuwa Bwana Yesu usiku ule aliyotolewa
alitwaa mkate, naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu
ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu. Na vivi hivi
baada ya kula akakitwaa kikombe, akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika
damu yangu; fanyeni hivi kila mnywapo, kwa ukumbusho wangu. Maana
kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana
hata ajapo.
1 Wakorintho 11.23-26
Marcello
Craveri anatwambia:
"Paulo, kwa
kuwa aliathirika na dini za mazingaombwe zilizoenea katika jamii za Kigiriki na
Kiasia alimoishi yeye, alimchanganya Yesu pamoja na vile vijiungu vya bandia
viokozi kama Orfia, Dionisa, Attis n.k. - vilivyokuwa vikiabudiwa na mila
hizo.Vijiungu hivi pia viliteseka na vikafa ili viwape watu fursa ya roho zao
kufikilia rehema ya kiungu. Waumini waliingizwa katika dini hizo kwa kupitia
katakismu (yaani kufahamishwa maana ya tambiko), kufunga, na kusafishwa.
Hapo tena hukubaliwa kuwa ni wanachama wa kaumu ya dini na hupata hifadhi ya
mungu. Huweza kuungana au kushirikiana kiroho na huyo mungu mwenyewe kwa kula
nyama ya mnyama mtakatifu ambaye ndiye ishara yake. Nyama na damu ya
mnyama yule huingiza sifa na khulka ya mungu katika roho ya mwenye kula nyama
na kunywa damu. Kadhaalika Paulo aliwaza mawazo yale ya nguvu za uchawi
zinazotokana na ule mkate wa Ekaristi kama wale mapagani makafiri walivyokuwa
wakiwaza katika wale wanyama wao wa muhanga."
Yapasa tukumbuke kuwa Mt Paulo hakuwa mwanafunzi wa Yesu wakati wa uhai wake,
wala hakuweza kudai kuwa waliwahi kukutana ila katika hiyo
"njozi" aliyodai kaiona alipokuwa njiani kwenda Dameski, na Yesu
hayupo tena. Madai yake yote anayategemeza juu ya "ufunuo" huo
alioupata. Kisa hicho kinasimuliwa mara tatu katika kitabu cha Matendo ya
Mitume kiliomo katika Biblia, na kila mara hadithi hiyo inakhtialifiana na nyengine,
kama tulivyokwisha ona.
