18- MISINGI YA KIPAGANI

Kwa mujibu wa mafunzo ya Mtume Muhammad s.a.w. Imani sio maana yake kuamini mwengineo atakubebea mzigo wako.  Hapana awezae kukuokoa, ila kwa kuwa anakuongoza njia ya sawa tu.  Uokofu uko mikononi mwako mwenyewe.  Qur'ani inasema:

Wala mbebaji hatabeba mzigo wa mwingine.

(Qur'ani) Az Zumar 39.7

Basi anayefanya chembe ya wema atauona, na anayefanya chembe ya uovu atauona.

(Qur'ani) Az Zilzaal 99.7-8

Si padri, wala kuhani, wala shekhe, wala Yesu, wala Muhammad, atakayetubebea dhambi zetu au kutufutia dhambi zetu.  Imani kama hiyo ni imani ya uvivu na kujidanganya mwenyewe, kuamini kuwa mateso au kifo cha mtu mwengine kinatosha kutufutia dhambi zetu sisi.  Yesu hakufundisha hayo.  Tumekwisha ona ushahidi wa kutosha katika Biblia kuwa imani hiyo sio aliyofunza Yesu, wala Manabii wote waliotangulia.  Tumenukulu ushahidi kutoka Yeremia 31.29-30, kutoka Ezekieli 18.19-20, kutoka Yohana 9.1-3 na kutoka Mathayo 18.3.  Mafunzo ya imani ya kuwa Yesu kachukua dhambi za watu kwa kifo chake msalabani kayazua Paulo kwa kuyanukulu kutokana na imani za kikafiri za kipagani zilizoenea katika Mashariki ya Kati na Ulaya Mashariki tangu karne za kabla ya kuja Yesu.  Attis katika Frigia, Adonis katika Syria, Dionisa au Bakkus katika Ugiriki, Mithra katika Iran na Osiris na Horus katika Misri, walikuwa miungu ya uwongo, miungu ya bandia, iliyokuwa na visa vile vile vya uokozi, na kufutia dhambi kwa kufa kwao na kufufuka kwao kutokana wafu kama inavyosimuliwa yaliyompitia Yesu. Kwa mfano Attis, mungu wa kipagani wa Frigia, anaambiwa alizaliwa na bikra Nana, na akiitwa Mwana wa Pekee na Mwokozi.  Aliuliwa chini ya mti wa msonobari kwa kumwagwa damu yake, na damu  yake ikiaminiwa kuwa ilitia rutba katika ardhi na ikaleta maisha mapya kwa wanaadamu.  Kifo chake kilitokea taarikh 24 mwezi wa Machi. akafufuka kutoka wafu, na kifo chake na kufufuka kwake kulisherehekewa na wafuasi wake kila mwaka.
Adonis, mungu bandia wa Syria, vile vile alizaliwa na bikra. Yeye pia aliteswa na akafa kwa kuokoa wanaadamu, na akafufuka kutoka wafu katika nyakati zile zile za Pasaka.
Dionisa au Bakkus wa Ugiriki akiitwa Mwana wa Pekee wa mungu Jupita.  Alizaliwa na mama bikra 25 Desemba!  Kwa wafuasi wake alikuwa ni Mwokozi.  Alijiita mwenyewe Alfa na Omega, yaani wa mwanzo na wa mwisho.  Kisa cha mateso yake kikisherehekewa kila mwaka, na mateso yenyewe ni kufa, kuteremka jahannam na kufufuka.
Osiris, mungu bandia wa Misri, naye alizaliwa 29 Desemba na mama aliyekuwa bikra.  Alisalitiwa na mtu mmoja aitwae Tifeni na akauliwa.  Alizikwa na akabaki katika jahannam muda wa siku mbili au tatu na masiku yake, na tena akafufuka kutoka wafu.
Mithra alikuwa mungu-jua wa Waajemi (Wairani).  Pia naye kazaliwa na bikra 25 Desemba. Krismasi na Pasaka ndio sikukuu zao muhimu kabisa, kama zilivyokuwa za dini nyenginezo za kikafiri, kipagani. Hawa Wamithra walikuwa na tambiko (sakramenti) saba; muhimu kabisa katika hizo ni ubatizo, na Ekaristi (Misa), ambapo hao washirika hula mkate na hunywa mvinyo, kwa kuwa ndio wanakula nyama ya Mithra, na kunywa damu yake.
Mwenye kujua ukweli huu lazima ajiulize nafsi yake kuwa Mtakatifu Paulo na wakuu wa Kanisa wenginewe wamepata tambiko za kufutiwa dhambi kwa damu ya Yesu, kuzaliwa kwake mwisho wa Desemba, kufa kwake na kufufuka kwake, na Pasaka, na Misa, na Utatu, kutokana na yeye Bwana Yesu, au kutokana na mila za kikafiri zilizokuwapo kabla ya Yesu huko Ugiriki, Misri, Syria na Iran?
Leo Tolstoi, Mkristo wa kweli na muaminifu wa Kirusi, ameandika katika risala yake aliyoita An Appeal to the Clergy (Ombi kwa Mapadri):

"Ikiwa Utatu, na kuchukua mimba bila ya toa (Immaculate Conception), na kuokoka binaadamu kwa damu ya Yesu, yamkinika, basi tena hapo kila kitu chamkinika - na hapana haja tena ya kutumia akili."