11- KUOKOKA KWA DAMU

Yasemekana kuwa watu wote tangu Adam na Hawa wana dhambi kwa kuwa wazee wao hao walimkosa Mungu kwa kwenda kula mti waliokatazwa.  Kwa hivyo wanamnyima Mungu sehemu ya haki yake. Hapana njia kuepukana na adhabu isipokuwa kwa kumrejeshea Mungu kile alichokhasiriwa na wanaadamu. Hoja iliopo ni kuwa ilivyokuwa wema wote uwezekanao kutendeka tokea hapo ni haki yake Mungu, hapana faida ipatikanayo kwa kutengeneza makosa yakisha tendeka.  Kwa hivyo ni mtu kamili asiye na dhambi kabisa anayekubali kuadhibiwa kwa madhambi ya watu wengine, ndiye awezae kumtuza Mungu kukasirika kwake. Ilivyokuwa ni Mungu tu ndiye asiye na dhambi, basi ni Yeye ndiye yampasa achukue umbo la mwanaadamu ajitolee, ajiachilie ateswe na  auwawe kwa makosa ya viumbe vyake.
Craveri anasema:

"Basi ndio tumezunguka mpaka tumelifikilia wazo la kushutua la mungu anayejiadhibu mwenyewe ili apate kuwasamehe wanaume na wanawake waliomuasi."


Hebu tuangalie hoja zinazotumiwa kutoka katika Biblia za kuleta imani ya kuokoka kwa damu ya Yesu.  Injili ya Marko inasema:

Yesu akawaita, akawaambia, Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa watu wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha.  Lakini haitakuwa hivyo kwenu;  bali anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu, na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote.  Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.

Marko 10.42-45

Kifungu hicho tulichokinukulu ni moja katika ushahidi unaotolewa katika thiolojia (ilimu ya Ungu) ya Kikristo kuthibitisha imani ya kuwa Yesu kaja duniani auwawe na damu yake iwe ni kafara au fidia kwa dhambi za wanaadamu. Hebu natukiangalie vyema kifungu hichi, chasema nini?

  1. Yesu anasema "hakuja kutumikiwa bali kutumika", licha kuabudiwa.
  2. Maneno yasemayo: "kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi" ni wazi kuwa ni mfano, kama usemi: "anayetaka kuwa wa kwanza, atakuwa mtumwa wa wote."  Bila ya shaka hapana atakayeona kuwa Yesu alikusudia kwa neno "mtumwa" ni kiumbe wa kuuzwa na kununuliwa. Hali kadhaalika "kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi" sio maana yake lazima kuuwawa.  Tafsiri ya Biblia The Interpreter's Bible inasema wazi juu ya kauli hiyo ya Yesu kuwa haiwezekani kuitumia kuwa ni ushahidi wa thiolojia ya Paulo ya kuokoka kwa damu.  Kauli hii lazima ichukuliwe kama ni mfano, kama usemi wa kishairi, kama ni mshabaha.  Wako baadhi ya wataalamu wa Kikristo ambao wanasema kauli hii ama iliongezwa na Marko au na mtu mwenginewe baadae, lakini Yesu hakusema hayo.  Lakini wenye kuandika hiyo tafsiri ya Biblia wanaona kwamba maneno hayo kayasema Yesu na yana maana ya mfano kama "vile mashahidi wa Kiyahudi walivyokufa kwa kuwaokoa watu wao (II Macc. 7.37-38; IV Macc. 17.22)"  Ikiwa maana yake ni hivyo wanaona wafasiri wa Interpreter's Bible yaweza kuwa kauli hiyo ni kweli ya Yesu, kama ikichukuliwa maana nyengine haiwezi kuwa ni kweli.

Katika gazeti moja la Misri ilitoka picha ya kuchora ya kuwapiga vijembe wale wanaotetea viti vya bunge.  Picha ilionyesha mazishi. Watu wamechukua jeneza ambalo limezungushwa bendera kubwa ilioandikwa:  "Mtu Anayekufa kwa Ajili Yenu".  Utepe uliotatiza shada la mauwa liliochukuliwa mbele ya jeneza uliandikwa: "Mpaka Makao yake ya Mwisho ya Kupumzika, Kiti cha Bunge."  Na mtu mmoja akisoma: "Mtilieni Voti!"  Katika wale wendao mazikoni mmoja lilimdondoka chozi, mwenzie akamzindua:
"Jizuie, mwanamume wee! Hii na kampeni tu!"
Ikiwa basi Yesu alikufa msalabani kwa ajili ya dhambi za watu, na ikiwa kweli yeye ni Mungu, basi mambo yote hayo ni kama sarkasi tu, mchezo wa kuigiza, au kiini macho.  Kwani hakika Mungu haiwezi kuwa aliona uchungu kwa yale mateso, na kufa kwake kulikuwa hakuna maana, kwani kumbe hakufa.  Mungu hufa?  Yote hayo yaonyesha kuwa ni udanganyifu mkubwa.
Na ikiwa yote hayo yalikuwa yamekwisha kadiriwa tangu mwanzo na kupangwa na kutimiza bishara za kinabii na kwa kupenda kwake Yesu, basi hao waliomtesa na wakamwua yafaa wafikiriwe na watukuzwe kama ni watu wema waliowaletea kheri wanaadamu wote, na wakamsaidia Yesu kutimiza lile alilolijia.  Hao akina Yuda, na Pilato, na lile baraza la wakuu wa Kiyahudi, wote hao ndio vipenzi vya Mungu, waliotimiza mapenzi ya Mungu baraabara.
Kifungu kingine cha maneno ya Biblia kinachonukuliwa mara nyingi kutilia nguvu imani ya kuokoka kwa damu ya Yesu ni hiki kutokana na Luka:

Atukuzwe Bwana, Mungu wa Israeli,
Kwa kuwa amewajia watu wake, na kuwakomboa.
Ametusimamishia pembe ya wokovu
Katika mlango wa Daudi, mtumishi wake.
Kama alivyosema tangu mwanzo
Kwa kinywa cha manabii wake watakatifu;
Tuokolewe na adui zetu
Na mikononi mwao wote wanaotuchukia;

Luka 1.67-71

Bishara  hii ni ya Zakaria alipozaliwa mwanawe Yohana (Nabii Yahya). Lakini ni wazi kuwa anasema ni Bwana Mungu ndiye aliyewaokoa watu wake kwa "kuwasimamishia pembe ya wokovu", naye ni Masihi aliyekuwa akitarajiwa na Mayahudi kuja kuwakomboa kutokana na adui zao wanaowachukia, nao ni watawala wa Kirumi. Kuja huyo mwokozi, anasema Zakaria, ni kutimiza yale maneno waliyoyasema manabii wa zamani.  Ni kuyapotoa maana ya maneno tukifasiri utabiri huu kuwa maana yake ni kuokolewa kwa damu ya Yesu.
Ushahidi mwingine unaodaiwa kuwa ni dalili ya uwokovu kwa damu ni huu:

 Siku ya pili yake (Yohana Mbatizaji) amwona Yesu anakuja kwake, akasema, Tazama, Mwana-kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu!

Yohana 1.29

Hata tukijaalia maneno haya ya Injili ya Yohana ni kweli (kwani hayathibitishwi na Injili zote nyenginezo) basi si kama tunavyomtaja kiongozi ye yote wa kidunia hivi leo kwa kusema: "Muangalieni huyo anayetubebea mizigo yetu yote"? Au tunapomwonya mmoja wetu: "Baba, utajiua nafsi yako kutaka kujitwika mambo ya ulimwengu mzima kwenye mabega yako hayo!" Kuchukua dhambi si lazima iwe maana yake ni kusamehewa dhambi kwa kuuliwa Yesu; bali ni kwa kuyafuata mafunzo yake na kwenda mwendo wake ndio watu watapata uwokovu.  Ni kwa kuyatenda mapenzi ya Mwenyezi Mungu aliyemtuma mtumishi wake Yesu, kuwa ni Nabii na Mtume, kama mwenyewe mara nyingi alivyosema, ndio watu wataokoka.  Ni kwa kutenda mema na yaliyokuwa ya murwa kwa mujibu wa mapendo na sharia za Mwenyezi Mungu ndio kila mtu ataweza kujiokoa nafsi yake. Sifa, bila ya shaka, itamrejea yule mwenye kuonyesha njia, na kwa hakika hivyo ndio amekuwa ni mwokozi wa watu. Mafunzo na maisha yake Yesu ndio muhimu yenye maana, na ndio hayo amejia duniani. Ama mateso yaliyompata ni matukizi yaliyomzukia katika ile kazi yake, wala yeye hakuyapenda; au asingekimbia na kujificha na kumwomba Mungu amwondolee kikombe cha mateso na mauti.  Yatufalia basi kuyatupa kando yaliyo muhimu na yenye maana, na tukan'gan'ganilia yaliyozuka tu?
Kifungu hichi kifwatacho kutokana na Injili ndicho kinachoonekana chenye ushahidi mkubwa wa imani ya kuokoka kwa damu:

Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele. Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye.

Yohana 3.16-17

Hapa yafaa tutambue kuwa hii Injili ya Yohana ni khitilafu kabisa na zile nyengine tatu.  Hii iliandikwa mwishoni kabisa baada ya zile.  Tangu awali haikukusudiwa hii kuwa ni maelezo ya kweli kueleza maisha ya Yesu kama yalivyokuwa, bali ilikusudiwa kuwa ni maoni ya huyo mwandikaji, naye amejaza humo mawazo yake mwenyewe.  Ni dhaahiri kuwa Injili ya Yohana ilikusudiwa kuthibitisha imani ambazo alikuwa zilikwisha mvaa mwandikaji. Wakati ilipoandikwa Injili hii Ukristo wa Paulo ulikuwa umekwisha pata nguvu na huyu mwandikaji alikuwa bila ya shaka ni mfuasi wa Ukristo wa Paulo, sio ule wa Yesu uliokuwa ukifuatwa na wanafunzi wake wa mwanzo. Katika Injili hii ungu wa Yesu unatiliwa mkazo, na Yesu ndio anaitwa "Mwana wa pekee wa Mungu."  Juu ya hivyo hii imani ya kuokoka kwa damu hata katika Injili hii haikusemwa kwa uwazi. Sana sana, itakuwa kama imegusiwa tu.  Ni yule mtu ambaye akili yake tangu hapo imekwisha pikwa ndiye atafasiri maneno haya:
 "Maana Mungu hakumtuma Mwana ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu, bali ulimwengu uokolewe katika yeye," kuwa maana yake ni kwa kufa kwake juu ya msalaba; au akafasiri "kila mtu amwaminiye" kuwa maana yake ni kuamini kuwa kifo chake kitakuwa ni fidia kwa dhambi za watu.
Dr. Hugh Schonfield katika Those Incredible Christians anatueleza kwa vizuri nini thamani ya Injili hii  kama alivyoiandika Yohana katika kusimulia maisha na mafunzo ya Yesu Kristo.  Anasema:

"Basi ndio hivyo katika Injili Yane,  kama katika barua ziliopelekwa kwa Makanisa Saba, si Yesu wa hakika ndio asemae, lakini ni Yohana Mkubwa ndiye anayesema kwa jina lake.  Juu ya hivyo uzushi hapo unaweza kutambulikana, si tu kwa kuwa Kristo wa Injili Yane anajieleza kwa namna ambayo si ya Kiyahudi, lakini zaidi ya hayo kwa sababu ushahidi wa waraka wa kwanza wa Yohana unadhihirisha kuwa Yesu anasema kwa njia anavyoandika huyo aliyebuni hayo yanayodhaniwa kuwa ni maneno yake. Yafaa tuwe na shukrani sana kwa kuwepo waraka huu.  Hapana haja ya kutishika kwa wazo la kuwa Mkristo hodari na hata kuwa ni mwenye mawazo ya kiroho ambaye maandishi yake yametiwa katika mkusanyo wa nyaraka takatifu, kuwa anaweza kuwa na khatia ya udanganyifu mkubwa kama huu. Yafaa iwe wazi kwetu hivi sasa ya kwamba viko vitabu kadhaa wa kadhaa katika Agano Jipya ambavyo ni vya uwongo, na vingine ambavyo vimekusudiwa kupotoa.  Hukumu yetu ya nini jema na nini baya tusiitumilie katika haya maandishi ya kale, katika zama ambazo haikuonekana kuwa ni makosa kuzua, kuongeza, au kugeuza nyaraka kwa sababu ya jambo la kheri. Kwa yakini Yohana alikuwa anaamini kuwa hizo mbinu zake ni za kuhesabiwa kuwa ni za haki na kuwa linaongozwa na Mungu. Hakuwa na shaka hata chembe kuwa alikuwa akiamini ya kwamba yeye kaletwa na Mungu kwa ajili ya kazi hiyo aifanyayo, na kwamba yeye anaongozwa na Roho (Mtakatifu). Yalivyokuwa mambo yote yanamwendea sawa yalizidi kuthibitisha hiyo imani yake."