DIBAJI

Kuzozana sio makusudio ya kuandika Risala hii.  Makusudio ya hakika ni kutaka kuwapa mwangaza Wakristo na Waislamu ambao katika sehemu nyingi za ulimwengu inawapasa waishi kama ni wananchi wamoja na jirani.  Inatumainiwa pindi wakinawirika, na kila mmoja akaifahamu vyema misingi ya imani ya mwenziwe, wote watakuja thamini ule msingi mmoja unaowaunga wote kwenye Imani ya asli, nayo ndiyo Dini ya Ulimwengu mzima inayofunza kila mwanaadamu ajisalimu kwa ukamilifu wake kwenye mapenzi ya Mwenyezi Mungu Mmoja wa kweli, kwani hapo ndipo unapotegemea mwendo mwema wa binaadamu.
Kwa bahati mbaya Yesu Kristo (Isa Masihi) hakutuachia mafunzo yake kwa maandishi ya kutegemewa kama alivyofanya Nabii Muhammad. Katika Qur'ani utakuta mafunzo ya Kiislamu yaliyo safi kabisa, yasiyo na chembe ya ila au wasiwasi.  Hatukutii katika Injili mfano wa hayo. Hizo ziitwazo Injili zaweza kulinganishwa na Hadithi za Mtume, bali khasa ni kama Sira Nabawiya, yaani Hadithi za Maisha ya Mtume, ni kama vitabu vya Maulidi.
Inakubaliwa na Wakristo wenyewe kuwa katika maneno na vitendo vya Yesu, kama inavyoelezwa katika Biblia, yamo mengi ambayo si ya kweli, na si ya kutegemewa, kama yalivyokuwepo katika Hadithi za Mtume kabla ya kuchujwa na kun'golewa hadithi na khabari zilizo dhaifu na kuthibitishwa zenye nguvu, Sahihi.  Haikataliki kuwa kwa sababu za kimadhehebu na sababu nyenginezo za mfarakano hadithi nyingi ziliwahi kubuniwa na kusingiziwa kuwa ni za Mtume, hali Mtume hakukhusika nazo kabisa.
Wachunguzi wa haki lazima wakiri kuwa katika kuzichambua na kuzikusanya Hadithi za Mtume Muhammad kulikuwepo mwendo bora zaidi wa kitaalamu kuliko uliokuwapo zilipoteuliwa hizi Injili ziliomo katika Biblia.  Hao wanazuoni wakubwa - Maimamu - waliotumia maisha yao yote katika kukusanya Hadithi, yaani semi na vitendo vya Mtume Muhammad, walifanya kila juhudi waliyokuwa nayo (yaani Ijtihad) wakitumia vipimo vya ilimu (scientific methodology) kuhakikisha ukweli na umadhubuti wa kila kauli na kila kitendo cha Mtume.  Kila Hadithi waisikiayo waliichungua na kuipekua kwa nani imepokelewa, na huyo naye kaipokea kwa nani, na tena kwa nani, mpaka kwa aliyeipata kwa mwenyewe Mtume.  Kila kiungo katika mnyororo wa wapokeaji uwe madhubuti sawa sawa kwa kila njia. Maisha ya kila mmoja ya wapokeaji yalilazimu kusomwa na yadurusiwe, na yachunguzwe kwa uangalifu kamili, mpaka uthibiti bila ya shaka yo yote uaminifu wake wa kupokea na kusimulia khabari kwa kweli bila ya kuzidisha wala kupunguza.  Hiyo peke yake ni ilimu iliyotungiwa vitabu kwa vitabu.  Tena huchunguzwa lugha - jee, ni ndio lugha namna hiyo na mbinu zake kama ilivyokuwa ikitumika Makka na Madina katika zama za Mtume?  Ni kweli ndiyo namna ya lugha alivyokuwa mwenyewe Mtume akijuulikana kutumia?  Pia huchunguzwa kuwa hayo maneno anayoambiwa Mtume kayasema, au vitendo kavitenda, havigongani kwa namna yo yote na mafunzo yaliomo katika Qur'ani? Kwani Qur'ani ndicho kipimo madhubuti kabisa.  Hayagongani na hakika ya mambo yanavyojuulikana kikweli bila ya khitilafu? Kwa njia hizi na nyenginezo ndio hao Maimamu waliokusanya Hadithi za Mtume wakizichuja, na zenye shaka wakizitenga kando, na kuziita Dhaifu, au Ziliobuniwa. Ziliopasi ndio wakaziita Sahihi na nzuri.
Lakini juu ya jitahada kuu waliyoifanya hao wanazuoni wa Hadithi bado juhudi yao ni juhudi ya kibinaadamu, na huenda ikakosea. Kwa bahati njema ipo Qur'ani, amabayo ukweli wake haujapata kutolewa kombo na rafiki wala adui.  Kila mtu ameangusha shingo yake mbele ya ukweli wa Qur'ani kuwa hapana mfano wake kitabu cho chote duniani ambacho kimebakia karne nenda karne rudi bila ya mabadiliko yo yote au machafuzi yo yote.  Hapana neno moja lililoongezwa, wala neno moja lililopunguzwa.  Hii Qur'ani iliopo sasa kwa lugha ya Kiarabu (sio tafsiri za maana yake katika lugha mbali mbali) ndio ile ile Qur'ani ambayo Mtume Muhammad aliyowakariria wafwasi wake miaka 1400 iliyopita, na wao wakaihifadhi kwa moyo na kuiandika, na khalafu yake miaka michache tu baada ya kufa kwa Mtume ikakusanywa pamoja kuwa ni Msahafu kama huu tuuonavyo sisi hii leo.  Huu basi ndio msingi usiolegalega, uliojengewa juu yake mafunzo ya Imani ya Kiislamu. Hichi ndicho kipimo cha kupimia usahihi wa Hadithi au Khabari yo yote ya Mtume, na ndio mwamba ambao juu yake limejengwa jengo la Uislamu.
Katika sahifa zifwatazo itaonekana kuwa nimependelea mno kunukulu maneno kutokana na vitabu mbali mbali.  Huu ndio mtindo wangu ninapoandika juu ya jambo muhimu, na khasa jambo lilio muhimu kupita kiasi kama hili la dini.  Sipendelei kuwa miongoni mwa wale "ambao wanaojadili mambo yaliyomkhusu Mwenyezi Mungu bila ya ilimu, wala uwongofu wala kitabu chenye kutoa mwangaza", kama isemavyo Qur'ani.
Nilipokuwa nikiidurusu Biblia katika upweke wa kizuizini katika magereza ya Tanzania nalijaribu kuyatafuta mafunzo ya kweli ya Yesu na Manabii wa Wana wa Israili waliomtangulia. Miaka kumi na miezi mitano ya kizuizi ikawa ni miaka kumi na miezi mitano ya mafunzo ya kweli kweli ya Biblia.  Kwa juhudi na taabu nikawa nabandua, bandu bandu, kidogo kidogo, magamba yaliyoifunika hiyo niliyokuwa nina yakini nayo - Lulu in'gaayo iliyozikwa chini ya magamba.
Nikaigundua.
Basi sasa nawaomba ndugu zangu wa Kiislamu ambao kuujua kwao Ukristo ni juu juu tu, na rafiki zangu wa Kikristo ambao takriban hawajui lo lote la kweli katika Uislamu (na kwa hakika hata Ukristo wa kweli) waje nami, na katika sahifa hizi zifwatazo tuutafute Ukweli.  Tutauona, kwani Ukweli ni Nyumba iliyojengwa juu ya Mwamba, na mvua itaanguka, na pepo zitavuma, lakini Nyumba haitaanguka.  Huko katika Yerusalemu Takatifu walipopaa wote wawili, Muhammad na Yesu, kwa uvuto wa kiroho mpaka wakafikilia Utukufu wake Mola Mlezi, kuna ishara ya dhaahiri inayotoa mwanga wa kuenea kote kote, ishara ya Ukweli unaomuamrisha Mwislamu na Mkristo kumsujudia Mwenyezi Mungu yule yule ambaye anaabudiwa kwa hamu na unyenyekevu sawasawa katika Msikiti ulio juu ya Mwamba na katika Kanisa la Kaburi Takatifu.  Ukweli huu unatuamrisha tuache mila za binaadamu na tufuate amri za Mwenyezi Mungu.  Ukweli huu unatuamrisha tuache mtindo wa kuigawa Dini katika vikundi vikundi  vya madhehebu na tuushikilie Umoja wa Mungu (Tawhid) unaotuunga sote pamoja.  Mwenyezi Mungu anasema katika Qur'ani:

 Na hakika tulimpa Musa Kitabu ili wapate kuongoka. Na tulimfanya Mwana wa Maryamu na mama yake kuwa Ishara na tukawapa makimbilio kwenda mahali polipoinuka penye utulivu na chemchem za maji.
Enyi Mitume!   Kuleni vyakula vizuri na fanyeni mema, hakika Mimi ni Mjuzi wa mnayoyatenda.
Na kwa yakini huu umma wenu ni umma mmoja, na Mimi ni Mola wenu Mlezi, basi nicheni Mimi.
Lakini walikatiana jambo lao mapande mbali mbali.  Kila kundi likafurahia kwa waliyo nayo.
 Basi waache katika ghafla yao kwa muda.


Tusitangetange ovyo katika vichochoro vya makosa na hali Njia safi Iliyonyooka iko wazi machoni mwetu. Tujifunze ukweli kutokana na kauli ya Mwenyezi Mungu. Tufahamiane na tukubaliane kuwa kila mmoja wetu kwa dhati ya nafsi yake atafanya juhudi  kuutafuta Ukweli, kwani Ukweli ndio utaotupa uzima.

Ali Muhsin Al Barwani