19- BISHARA YA YESU YATIMIA

Ikiwa Yesu hakutuachia uongozi wa kutosha katika mambo ya dhambi na kuhisabiwa haki, na hukumu, basi ni kwa sababu madhubuti, ambazo yeye mwenyewe amezitaja. (Tazama Injili ya Yohana 16.5-14 kama tulivyokwisha nukulu.)  Tena, lakini alimuelezea hivi huyo ambaye atakuja:  "Naye akiisha kuja, huyo atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki, na hukumu...atawaongoza awatie kwenye kweli yote."Yesu alisema kuwa huyo ajaye ataufundisha ulimwengu khabari ya hukumu.  Yeye mwenyewe hakuweza kuweka mfano wa uhakimu kwa kuwa maisha yake alikuwa mkimbizi anakimbia kuhukumiwa. Historia haitwambii kuwa alikuwapo mwongozi ye yote wa dini baada ya Masihi aliyeshika uhakimu isipokuwa Muhammad.  Muhammad amepitia kila namna ya maisha.  Alikuwa mchunga kondoo, mwananchi wa kawaida, mume, baba, mpigania uhuru, mtawala, mtunga sharia, mwana siasa, hakimu, walii na Mtume wa Mwenyezi Mungu, tena ndiye wa mwisho wa wote.  Amebeba ujumbe uliotoka moja kwa moja kutokana na Mwenyezi Mungu.  Muhammad akihukumu, lakini hukumu yake ilikuwa imelainishwa na rehema, kama inavyoelekea kwa mtu anayehukumu kwa nguvu na uwezo wa Mwenyezi Mungu.  Maisha yake ya kila namna ni ruwaza ya kutosha kwetu sisi sote, kuiga kama tulivyojaaliwa katika maisha yetu.  Yeye alifunza kwa maneno na vitendo. Hakuwa mtu aliyejitenga na ulimwengu akasema maneno matamu lakini maneno yenyewe hayatendeki.  Alikuwa mtu wa vitendo, mtu wa kidunia, na wakati huo huo kwa upande wa kiroho alikuwa na khulka bora kabisa hata mwenyewe Aliyemuumba hakuweza ila kumsifu kwa kumwambia:

Na hakika wewe una tabia tukufu.

(Qur'ani) Al Qalam 68.4

Mara moja Bibi Aisha, mkewe, aliulizwa (na nani amjuaye mtu kuliko mkewe?) nini tabia ya Mtume, alijibu kwa mkato: "Khulka yake ni Qur'ani!"  Hapana sifa kubwa kuliko hii. Mtu huyu aliishi ile dini yake.  Maadui zake wanakubali kuwa hapana kitabu kinachokubaliana na mtu, kuliko Qur'ani inavyokubaliana na maisha ya Mtume Muhammad s.a.w.   Amri zilizotokana na Mungu wake, ndio maisha yake.  Si ajabu basi Yesu kusema kuwa Muhammad atauhakikisha ulimwengu kwa khabari ya haki.
Huyo mtu aliyebashiriwa na Yesu kuwa atakuja ni kuwa atakuwa Mtume wa ulimwengu mzima, kwani zama za Mitume ya kabila fulani na kondoo fulani waliopotea umekwisha.  Huyo ajaye ni Mtume wa watu wote, wa kabila zote, na wa mambo yote.  Huyo ni wa kuuhakikisha ulimwengu, na wa kufunua kweli yote. Hali kadhaalika Mwenyezi Mungu anamwambia Muhammad:

Na hatukukutuma ila kwa watu wote, uwe Mbashiri na Mwonyaji.

(Qur'ani) Saba 34.28

Na sisi hatukukutuma ila uwe ni rehema kwa walimwengu wote.

(Qur'ani) Al Anbiyaa 21.107

 Yesu alisema ana mengi ya kusema, lakini watu wake hawakuwa na uwezo wa kuyachukua wakati ule.  Wataongozwa kwenye kweli yote na huyo ajaye, Roho wa Kweli, ambaye itakuwa fakhari yake kuutangazia ulimwengu baada ya kutimiza ujumbe wake: "Hapana Nabii baada yangu."  Ni yeye huyo ambaye ameitwa na Mwenyezi Mungu: "Khaatamun Nabiyyiina, Mwisho wa Manabii, Muhuri wa Manabii. Waraka ukisha tiwa muhuri hapana ruhusa kuongeza kitu juu yake. Chupa ikitiwa Khaatam, (Seal), ndio imezibwa, huwezi kuongeza kitu tena. Ukiongeza unaghishi, unafanya khadaa.  Qur'ani na mwenendo wa Mtume Muhammad upo kutuongoza sisi katika mambo yetu yote mpaka Siku ya Mwisho.  Hakujuidai  ila lilio haki yake.  Alikataa katakata kufanywa mungu wa bandia.  Daima akisema:  "Mimi ni mwanaadamu tu."  Mwenyezi Mungu alimuamuru aseme:

Sema:  Bila shaka mimi ni mwanaadamu kama nyinyi.  Ninaletewa Ufunuo (Wahyi) ya kwamba Mungu wenu ni Mungu Mmoja tu.  Basi anayetaraji kukutana na Mola wake Mlezi naatende vitendo vyema, wala asimishirikishe ye yote katika ibada ya Mola wake Mlezi.

(Qur'ani) Al Kahf 18.110

Kazi yake, kama ilivyokuwa kazi ya Yesu, ilikuwa kufanya apendavyo Yeye Mwenyezi Mungu aliyemtuma.  Muhammad hakudai kuwa yeye ni muanzishi wa dini mpya.  Bali aliendeleza na akatimiza dini aliyokuja nayo Ibrahim, Musa, Isa (Yesu), na Manaabii wote waliotoka kwa Mwenyezi Mungu.  Wote hao wakitenda mapenzi ya Mwenyezi Mungu.  Na huo ndio Uislamu.  Neno "Islam" lina maana ya Usalama, na maana ya kujisalimu kwa Mwenyezi Mungu, utende lile limpendezalo Mwenyezi Mungu, yaani kutenda mapenzi ya Mungu, kama asemavyo Yesu.  Mwenyezi Mungu anasema katika Qur'ani kuwa hapana kaumu ila walipelekewa Nabii.  Lakini Mtume Muhammad kwa kuwa ni wa ulimwengu mzima, kama alivyobashiri Yesu, na kwa kuwa ni wa mwisho, basi ni mwenye kuthibitisha ukweli wa ujumbe wote uliotoka kwa Mwenyezi Mungu, na mwenye kuondoa makosa yaliyopachikwa na wanaadamu katika dini ya Mwenyezi Mungu.  Kwa kuwa wakati umefika wa kukusanya ulimwengu mzima uwe na Imani moja, na kuelekea kumoja, ndio akaja Mtume Muhammad, kama ni Mtume wa Mwisho wa ulimwengu mzima.  Myahudi mwenye kumkubali kumfuata Mtume Muhammad ndio basi ametimiza maamrisho ya Musa na Ibrahim na Manabii wake wote anaowaamini.  Mkristo anayemkubali Muhammad na akamfuata ndio ametimiza Ukristo wake, na amekubali kweli mafunzo yaliyomo katika Taurati na Injili na khasa ameyafuata maamrisho ya Yesu.  Qur'ani inasema:

Hakika Walioamini na Mayahudi na Wakristo na Wasabai: ye yote atakayemuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho na akatenda mema, basi watapata malipwa yao kwa Mola wao Mlezi, wala haitakuwa khofu juu yao, wala hawatahuzunika.

(Qur'ani) Al Baqara 2.62

Dunia wakati wa Yesu ilikuwa bado haijawa tayari kuweza kupokea fikra ya dini ya kukusanya ulimwengu mzima, dini isiyokuwa ya kabila fulani, au rangi fulani.  Sisi leo tunaona jambo hilo ni la kawaida tu, lakini zama zile kila kikabila kilikuwa na lake. Ndio maana hata Manabii wa kweli waliotokana na Waisraili walimwita Mwenyezi Mungu kwa jina la Mungu wa Israili. Na kweli kila taifa lilikuwa na mungu wake, na ibada zake. Ni khatua kubwa hiyo aliyochukua Yesu kuwaambia wanafunzi wake wende kwa kabila kumi na mbili za Israili. Yesu hakutangaza dini yake ila kwa "kondoo waliopotea wa nyumba ya Israili." Ndio maana akasema kuwa yeye hawaombei walimwengu, bali wale tu aliopewa na Mungu, Wana wa Israili.  Yesu aliogopa kuwa mafunzo yake yakipelekwa kwa mataifa mengine wasio Waisraili yatavurugwa mafunzo hayo kama nguruwe waliotupiwa lulu wangeziponda hizo lulu na kuwararua watu kwa kutojua thamani ya lulu. Lakini Yesu alisema katika Karamu ya Mwisho kuwambia wanafunzi wake kuwa wakati ukifika atakuja atayetimiza kweli yote, atafunza ulimwengu mzima juu ya dhambi, haki na hukumu.
Na kweli tumeiona. Historia iwazi kuwa hapana mtu aliyefunza udugu wa walimwengu kama alivyofunza Mtume Muhammad.  Hapana mtu aliyevunja ubaguzi kama alivyouvunja Muhammad.  Hapana mtu aliyepiga marfuku khitilafu za rangi na kabila na taifa kama Muhammad.  Ndio maana tangu mwanzo wake waliomfuata wakawa pamoja naye kufa kupona, hawakuwa watu wa kabila lake tu la Kikureshi, au taifa lake tu la Kiarabu, bali walikuwamo pia Wazungu, Waafrika na Waasia.  Ni yeye Muhammad ndiye aliyesema:  "Majivuno kwa uungwana wa kikale nayakanyaga chini ya miguu yangu.  Mwaarabu si bora kuliko asiyekuwa Mwaarabu, wala asiyekuwa Mwaarabu si bora kuliko Mwaarabu.  Mwekundu si bora kuliko mweusi wala mweusi si bora kuliko mwekundu, ila kwa uchamngu.  Watu wote ni sawa kama meno ya kitana.  Wote ni wana wa Adam, na Adam ametokana na mchanga."
Hayo ni machache katika maneno yake aliyoyasema juu ya ubaguzi wa rangi na taifa, jambo ambalo mpaka hii leo linawahangaisha wasiomfuata Muhammad.  Tena Mtume Muhammad hakusema tu bali alitenda.
Katika Uislamu hapana waajibu wenye fadhila kama sala za jamaa. Na katika hizo, nyadhifa mbili ndio tukufu:  Imamu na Muadhini.  Mtume mwenyewe alikuwa ndiye Imamu, na akamteua Bilal kuwa Muadhini wa kwanza katika Uislamu.  Bilal alikuwa Muafrika mweusi, aliyekombolewa na Abubakar kutoka utumwani. Mtume hakuona junaha kumwoza Zaid binti wa shangazi lake yeye Mtume, na ilhali huyo Zaid alikuwa kwanza ni mtumwa wa Kiarabu, wake yeye mwenyewe Muhammad, na akamuachia huru. Wala hakuona kiroja kumteua Usama, chotara wa mama wa Kiafrika mweusi, awe Jemadari wa jeshi kuu la Kiislamu kupambana na Warumi, na chini yake walikuwa Masahaba wakubwa wakubwa wa Kikureshi.  Yeye huyo kijana chotara, Usama, alikuwa umri wake miaka 18.
Safari moja walikuja baadhi ya Waarabu wakamtaka Mtume awapatie mume wa Kiarabu wa ukoo mzuri kumwoza binti yao.  Mtume akawaambia:  Mwamuonaje Bilal?  Wale jamaa wakenda zao.  Siku ya pili wakaja tena, na Mtume akawauliza suala lile lile la jana; wakenda zao.  Siku ya tatu wakaja tena, na Mtume akawauliza suala lile lile la jana na juzi, lakini akaongeza: "Mwamuonaje mwanamume katika watu wa Peponi?"  Wakamwoza.  Watu wote wakajua kuwa Muhammad habagui baina ya watu ila kwa uchamngu wao tu.  Masahaba walimtukuza Bilal kama alivyokuwa akitukuzwa na mwenyewe Mtume.
Mwenyezi Mungu wa watu wote, dini ya watu wote, Udugu wa watu wote - hayo yasingeweza kufunzwa ila na mtu kama yule, na kukubaliwa na watu kama wale, kwa zama kama zile.  Si ajabu basi vile Uislamu ulivyotanda kama kwamba ni moto wa nyikani.  Thomas Carlyle, muandishi na mtu mwenye mawazo madhubuti, maarufu wa Kiingereza alisema katika khutba yake kumsifu Mtume Muhammad aliyoitoa London yapata miaka mia mbili iliyopita:

"Taarikh (Historia) ya taifa huwa ina wingi wa matunda, inatukuza roho na inakuwa kubwa pale lile taifa linapoamini. Waarabu wale, yule mtu Muhammad, na ile karne moja - hebu si kama cheche moja  ilioanguka, cheche moja juu ya ulioonekana kuwa ni mchanga mweusi usio na maana?  Lakini lo! kumbe ule mchanga ni baruti inayoripuka, ukawaka ukiangaza mpaka mbinguni, kutoka Delhi (Bara Hindi) mpaka Granada (Uspania)!"


 Si imani tu ndio iliyofanya muujiza, lakini namna ya imani yenyewe, imani ya udugu wa binaadamu wote, na dini ya ulimwengu mzima.  Kutoka Kaskazini mpaka Kusini mwa dunia, kutoka Mashariki mpaka Magharibi, wote wakaifuata imani moja.  Wote wakaelekea Makka. Wote wakawa ndugu, wote wakachanganya damu na tamaduni. Wakawa Umma mmoja, Taifa moja, Taifa la Kiislamu, wafuasi wa Muhammad na Isa na Musa na Ibrahim, na kila Nabii aliyetumwa na Mwenyezi Mungu. Wote walimuamini Mungu Mmoja, asiyezaa wala kuzaliwa, wala hana mfano wake. Wote waliwaamini Manabii walioletwa na Mwenyezi Mungu, na wakaamini ukweli wa asli ya dini zote zilizitoka mbinguni.