Hili
neno Biblia ni neno la Kigiriki, na maana yake ni "vitabu".
Basi Biblia ni mkusanyiko wa vitabu vingi ambavyo ndio vinafanya msingi wa
imani ya Kikristo. Inakubaliwa kuwa vitabu hivi vimeandikwa na watu wengi
mbali mbali, wajuulikanao na wasiojuulikana. Lakini hao waandishi
wanaaminiwa kuwa walipata ufunuo kutokana na Mwenyezi Mungu, na wameandika
walivyoandika chini ya uangalizi na uwongozi wa Mwenyezi Mungu; kwa hivyo
Biblia inaambiwa kuwa ni Neno la Mungu. Biblia ya Wakatoliki, lakini, kidogo
inakhitalifiana na ya Waprotestani. Ya Wakatoliki ina vitabu 73, na ya
Waprotestani ina vitabu 66.
Kwa jumla Biblia imegawika sehemu mbili kubwa, Agano la Kale na Agano
Jipya. Agano la Kale ni vitabu vyote vilivyoandikwa kabla ya kutokea Yesu
Kristo. Vitabu hivi vinaeleza tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu, na Adamu
na Hawa, historia (taarikh) ya wanaadamu na khasa ya Wana wa Israili, sharia
alizopewa Musa na Mwenyezi Mungu, vita vya Mayahudi na jirani zao, mafunzo ya
manabii kadhaa wa kadhaa katika Bani Israili yaliyotokana na Mwenyezi Mungu.
Isipokuwa kwa baadhi ya vitabu ambavyo hawavikubali hili liitwalo Agano la
Kale, kwa jumla, ndio liliokuwa Biblia na mpaka hivi sasa ndio Biblia ya
Mayahudi. Mayahudi hawaikubali kabisa sehemu ya pili iitwayo Agano Jipya
inayokubaliwa na Wakristo.
Agano Jipya ni ile sehemu ya Biblia iliyoandikwa baada ya Yesu
Kristo. Sehemu hiyo inakusanya Injili nne. Hizi ziitwazo Injili ziliomo
katika Biblia ni vitabu vinavyosimulia maisha ya Yesu Kristo na mafunzo yake. Katika
Agano Jipya kipo kitabu
kinachoitwa Matendo ya Mitume, kinachoeleza khabari za wanafunzi wake Yesu
aliowatuma kwenda tangaza dini. Pia kipo kitabu kinacho itwa "Ufunuo"
chenye kueleza mambo ya ajabu ajabu ambayo yasimuliwa kuwa Yohana alifunuliwa
akayaona. Hali kadhaalika zimo barua kadhaa wa kadhaa, nyingi zao ni za Paulo,
walizopelekewa watu fulani fulani kuwafunza mambo ya dini. Hizi barua za Paulo,
Myahudi aliyetanasari, zinategemewa sana na Wakristo, na ndio msingi wa imani
na itikadi zao, hata wengi wapo wanaosema kuwa huu Ukristo tuuonao sasa kwa
hakika uliasisiwa na Paulo.
Vitabu viliomo katika Agano la Kale kama vilivyo hivi sasa labda viliandikwa
baada ya kurejea Mayahudi kutoka utumwani Babilionia, yaani baada ya mwaka 536
kabla ya Kristo. Na vitabu vya Agano Jipya vilikusanywa na kukubaliwa na
wakuu wa Kanisa katika karne ya nne baada ya Kristo (kiasi 367 A.D.) Injili nne
ziliomo katika Agano Jipya, yaani ya Mathayo, ya Marko, ya Luka na ya Yohana,
ndizo zilizoteuliwa na kukubaliwa na wakuu wa Kanisa kutokana na Injili nyingi
sana ambazo zimekataliwa. Neno "Injili" ni neno la Kigiriki, na maana
yake ni "Khabari Njema", kwa kuwa Yesu alikuwa akisema kuwa analeta
Khabari Njema, yaani Bishara. Vitabu ambavyo vingeweza kuwa ni sehemu ya Biblia,
na kwa hakika vikawa vinakubaliwa kwanza na pengine mpaka sasa na baadhi ya
madhehebu za Kikristo, vinaitwa "Apokrifa", yaani
"vilivyofichwa".
Sisi tunaposema Biblia tunakusudia vitabu vinavyotambuliwa na madhehebu kuu za
Kikristo kuwa ndivyo Neno la Mungu tu.