Suratul Hijr ni Sura ya Makka. Nayo ina Aya 99. Imeanza kwa harufi za kutamkwa
zenye kueleza kwamba Qur'ani imejengeka kwa harufi hizi hizi mnazo zitumia
katika maneno yenu, na juu ya hivyo ni Muujiza kwenu, hamwezi kuleta kama
hii. Kwani aliye iteremsha ni Mwenyezi Mungu, Aliye takasaika, na Akatukuka.
Na hizo harufi pia ni kama kuwazindua wale wanao ipuuza Qur'ani, inawalingania,
inawaita, waisikilize. Asaa wakanufaika, na wakahidika kumfuata Mwenyezi
Mungu.
Sura hii tukufu inabainisha ili watu wazingatie yaliyo wapata kaumu
zilizo tangulia, na khabari za Manabii walio kwisha pita, na yaliyo
wapata kutokana na watu wao. Na pia Sura hii inaonyesha ishara za Mwenyezi
Mungu katika ulimwengu, katika mbingu zilizo nyanyuliwa na zenye sayari
ziilizo hifadhiwa, na ardhi iliyo tandikwa, na kukunjuliwa, na milima iliyo
simama imara, na pepo zenye kubeba maji, na zenye kupandishia miti. Na
Sura hii pia inaashiria mpambano wa mwanzo katika maumbile ya asli baina
ya maluuni Iblisi na Adam na mkewe, na kuendelea mpambano huo baina ya
kheri na shari mpaka imalizike dunia. Kisha tena malipo ya shari Siku ya
Kiyama, na malipo ya kheri. Na baada ya hayo Mwenyezi Mungu anasimulia
visa vya Manabii wawili, Ibrahim na Luut'i, na watu wa Al Hijr. Na Sura
inaeleza cheo cha Qur'ani, na hali ya washirikina katika kuipokea, na impasavyo
Nabii kwa mnasaba wa ukafiri wao, navyo ni kufikisha ujumbe wake, na kuutangaza,
na kumuabudu Mwenyezi Mungu mpaka ifike amri ya yakini.
KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
1. Alif Lam Ra. (A.L.R). Hizi ni Aya za Kitabu
na Qur'ani inayo bainisha.
***
2. HUENDA ikawa walio kufuru wakatamani wange
kuwa Waislamu.
***
3. Waache wale, na wastarehe, na iwazuge tamaa.
Watakuja jua.
***
4. Na hatukuuangamiza mji wowote ule ila ulikuwa
na muda wake maalumu.
***
5. Hawawezi watu wowote kuitangulia ajali yao,
wala kuchelewa.
***
6. Na walisema: Ewe uliyeteremshiwa Ukumbusho!
Hakika wewe ni mwendawazimu.
***
7. Mbona hutuletei Malaika ikiwa wewe ni miongoni
mwa wasemao kweli?
***
8. Sisi hatuwateremshi Malaika ila kwa sababu
ya haki, na hapo hawatapewa muhula.
***
9. Hakika Sisi ndio tulio teremsha Ukumbusho huu,
na hakika Sisi ndio tutao ulinda.
***
10. Na hakika tulikwisha watumia Mitume mataifa
ya mwanzo.
***
11. Na hakuwafikia Mtume ila walimkejeli.
***
12. Na kama hivi ndivyo tunavyo ingiza katika
nyoyo za wakosefu.
***
13. Hawayaamini haya, na hali ya kuwa umekwisha
wapitia mfano wa watu wa kale.
***
14. Na lau tungeli wafungulia mlango wa mbingu,
wakawa wanapanda,
***
15. Basi wangeli sema: Macho yetu yamelevywa,
bali sisi wenyewe tumerogwa.
***
16. Na hakika tumeweka katika mbingu vituo vya
sayari, na tumezipamba kwa wenye kuangalia.
***
17. Na tumezilinda na kila shetani afukuzwaye.
***
18. Isipo kuwa mwenye kusikiliza kwa kuibia,
naye hufuatwa na kijinga cha moto kinacho onekana.
***
19. Na ardhi tumeitandaza na humo tumeweka milima,
na tumeotesha kila kitu kwa kiasi chake.
***
20. Na tumekujaalieni humo vitu vya maisha yenu,
na ya hao ambao nyinyi sio wenye kuwaruzuku.
***
21. Na hakuna chochote ila asili yake inatokana
na Sisi; wala hatukiteremshi ila kwa kipimo maalumu.
***
22. Na tunazipeleka pepo za kupandishia, na tunateremsha
kutoka mbinguni maji, kisha tukakunywesheni maji hayo. Wala si nyinyi mnayo
yaweka.
***
23. Na Sisi ndio tunao huisha na tunao fisha.
Na Sisi ndio Warithi.
***
24. Na tunawajua walio tangulia katika nyinyi,
na tunawajua walio taakhari.
***
25. Na hakika Mola wako Mlezi ndiye atakaye wakusanya.
Hakika Yeye ni Mwenye hikima na Mjuzi.
***
26. Na tulimuumba mtu kwa udongo unao toa sauti,
unao tokana na matope yaliyo tiwa sura.
***
27. Na majini tuliwaumba kabla kwa moto wa upepo
umoto.
***
28. Na Mola wako Mlezi alipo waambia Malaika:
Hakika Mimi nitamuumba mtu kwa udongo unao toa sauti, unao tokana na matope
yaliyo tiwa sura.
***
29. Basi nitakapo mkamilisha na nikampulizia
roho yangu, basi mumwangukie kumsujudia.
***
30. Basi Malaika wote pamoja walimsujudia,
***
31. Isipo kuwa Iblisi. Yeye alikataa kuwa pamoja
na walio sujudu.
***
32. (Mwenyezi Mungu) akasema: Ewe Iblisi! Una
nini hata hukuwa pamoja na walio sujudu?
***
33. Akasema: Haiwi mimi nimsujudie mtu uliye
muumba kwa udongo unao toa sauti, unao tokana na matope yenye sura.
***
34.(Mwenyezi Mungu) akasema: Basi toka humo,
kwani hakika wewe ni maluuni!
***
35. Na hakika juu yako ipo laana mpaka Siku ya
Malipo.
***
36. Akasema (Iblisi): Mola wangu Mlezi! Nipe
muhula mpaka siku watapo fufuliwa.
***
37. (Mwenyezi Mungu) akasema: Hakika wewe ni
katika walio pewa muhula
***
38. Mpaka siku ya wakati maalumu.
***
39. Akasema: Mola wangu Mlezi! Ilivyo kuwa umenitia
makosani, basi nahakikisha nitawazaini hapa duniani na nitawapoteza wote,
***
40. Ila waja wako walio safika.
***
41. Akasema: Hii Njia ya kujia kwangu Iliyo Nyooka.
***
42. Hakika waja wangu, wewe hutakuwa na mamlaka
juu yao, isipo kuwa wale wapotofu walio kufuata.
***
43. Na bila shaka Jahannamu ndipo pahali pao
walipo ahidiwa wote.
***
44. Ina milango saba; na kwa kila mlango iko
sehemu walio tengewa.
***
45. Hakika wachamngu watakuwa katika Mabustani
na chemchem.
***
46. (Wataambiwa:) Ingieni kwa salama na amani.
***
47. Na tutaondoa chuki iliyo kuwamo vifuani mwao,
wawe ndugu juu ya viti vya enzi wameelekeana.
***
48. Humo hayatawagusa machofu, wala hawatatolewa
humo.
***
49. Waambie waja wangu ya kwamba Mimi ndiye Mwenye
kusamehe, Mwenye kurehemu.
***
50. Na kwamba adhabu yangu ndio adhabu iliyo
chungu!
***
51. Na uwape khabari za wageni wa Ibrahim.
***
52. Walipo ingia kwake na wakasema: Salama! Yeye
akasema: Hakika sisi tunakuogopeni.
***
53. Wakasema: Usiogope. Sisi tunakubashiria kijana
mwenye ujuzi.
***
54. Akasema: Mnanibashiria nami uzee umenishika!
Basi kwa njia gani mnanibashiria?
***
55. Wakasema: Tunakubashiria kwa haki; basi usiwe
miongoni mwa wanao kata tamaa.
***
56. Akasema: Na nani anaye kata tamaa na rehema
ya Mola wake Mlezi ila wale walio potea?
***
57. Akasema: Hebu nini amri yenu, enyi wajumbe?
***
58. Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwa kaumu
ya wakosefu!
***
59. Isipo kuwa walio mfuata Luut'i. Bila ya shaka
sisi tutawaokoa hao wote.
***
60. Ila mkewe. Tunakadiria huyo atakuwa miongoni
watao bakia nyuma.
***
61. Basi wale wajumbe walipo fika kwa Luut'i,
***
62. Alisema (Luut'i): Hakika nyinyi ni watu msio
juulikana.
***
63. Wakasema: Bali sisi tumekuletea yale waliyo
kuwa wakiyafanyia shaka.
***
64. Na tumefika kwako kwa Haki, na hakika sisi
tunasema kweli.
***
65. Basi ondoka na ahli zako usiku ungalipo,
nawe ufuate nyuma yao, wala yeyote kati yenu asigeuke nyuma. Na mwende
mnapo amrishwa.
***
66. Na tukamfunulia hukumu hiyo, ya kwamba hata
wa mwisho wao hao ikifika asubuhi atakuwa kesha katiliwa mbali.
***
67. Na wakaja watu wa mji ule nao furahani.
***
68. Akasema: Hakika hawa wageni wangu, basi msinifedheheshe.
***
69. Na mcheni Mwenyezi Mungu, wala msinihizi.
***
70. Wakasema: Sisi hatukukukataza usimkaribishe
yeyote?
***
71. Akasema: Hawa binti zangu, ikiwa nyinyi ni
watendaji.
***
72. Naapa kwa umri wako! Hakika hao walikuwa
katika ulevi wao, wakihangaika ovyo.
***
73. Ukelele ukawatwaa wakipambaukiwa.
***
74. Na tukaigeuza nchi juu chini, na tukawanyeshea
mvua ya mawe ya udongo wa Motoni.
***
75. Hakika katika hayo zipo ishara kwa waaguzi.
***
76. Na miji hii ipo kwenye njia inayo pitiwa.
***
77. Hakika katika hayo ipo ishara kwa Waumini.
***
78. Na hakika watu wa Kichakani walikuwa wenye
kudhulumu.
***
79. Kwa hivyo tukawaadhibu. Na nchi mbili hizi
ziko kwenye njia ilio wazi.
***
80. Na bila ya shaka wakaazi wa Hijr waliwakanusha
Mitume.
***
81. Na tuliwapa ishara zetu, nao wakazipuuza.
***
82. Nao walikuwa wakichonga majumba katika milima
kwa amani.
***
83. Basi ukelele ukawatwaa asubuhi.
***
84. Hayakuwafaa waliyo kuwa wakiyachuma.
***
85. Na hatukuziumba mbingu na ardhi na vilivyomo
ndani yake ila kwa ajili ya Haki. Na hakika Kiyama kitafika. Basi samehe
msamaha mzuri.
***
86. Hakika Mola wako Mlezi ndiye Muumbaji Mjuzi.
***
87. Na tumekupa Aya saba zinazo somwa mara kwa
mara, na Qur'ani Tukufu.
***
88. Usivitumbulie macho yako vitu tulivyo waneemesha
makundi fulani kati yao, wala usiwahuzunikie. Na wainamishie bawa lako
(la huruma) Waumini.
***
89. Na sema: Hakika mimi ni mwonyaji mwenye kubainisha.
***
90. Kama hivyo tuliwateremshia walio gawa,
***
91. Ambao wakaifanya Qur'ani vipande vipande.
***
92. Basi Naapa kwa Mola wako Mlezi! Tutawahoji
wote,
***
93. Kwa waliyo kuwa wakiyatenda.
***
94. Basi wewe yatangaze uliyo amrishwa, na jitenge
na washirikina.
***
95. Hakika Sisi tunatosha kukukinga na wanao
kejeli.
***
96. Hao wanao fanya kuwa pamoja na Mwenyezi Mungu
yupo mungu mwingine. Basi, watakuja jua!
***
97. Na Sisi tunajua kwa hakika kuwa wewe kifua
chako kinaona dhiki kwa hayo wayasemayo.
***
98. Basi mtakase Mola wako Mlezi kwa kumhimidi,
na uwe miongoni wanao msujudia.
***
99. Na muabudu Mola wako Mlezi mpaka ikufikie
Yakini.
***
Ukitaka kusoma Sura nyengine Rejea uliko toka
Ukiwa una shauri au maelezo juu ya tarjuma hii, andika kwa anwani hii qurani-tukufu@geocities.com